Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia hoja za Kamati zetu tatu ambazo zimewasilishwa mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze sana Wajumbe wote wa Kamati hizi tatu kwa uchanbuzi wao wa makini na niseme kwamba Wizara yetu imepokea mapendekezo, maoni na ushauri ambayo yametolewa na Kamati na tutaufanyia kazi ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijaendelea na kuchangia hoja hii naomba nimpongeze kwa dhati Rais wa Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuiongoza Nchi yetu kwa weledi, kwa kuchukua hatua mahususi za kuhakikisha kwamba analeta ustawi kwa Watanzania za kuhakikisha kwamba anatatua kero za muda mrefu katika baadhi ya maeneo ambayo yameguswa na taarifa ambazo zimewasilishwa na kamati zetu makini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja ya maeneo ambayo Kamati zimezungumzia ni madeni ya muda mrefu ya kwenye mifuko. Mfuko wa PSSF ulikuwa na deni la trilioni 4.600 ambalo lilitokana na deni la tangu mwaka 1999 ambapo Serikali ilipoanzisha mifuko iliamua kuchukua jukumu la kulipia wafanyakazi wote waliokuwa wameajiriwa kabla ya Julai 1999.

Mheshimiwa Spika, tangu Serikali imechukua uamuzi huo mwaka 1999 fedha hizo zilikuwa hazijawahi kulipwa mpaka Disemba 2021chini ya Uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Nampongeza kwa dhati kwa kweli kwa sababu hatua hiyo imeimaarisha sana mfuko wetu wa PSSF. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, alikuta deni la mfuko wa PSSF la bilioni 731 na tayari Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amekwishalipa kiasi cha shilingi bilioni 500. Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan alikuta pia kuna kero kubwa ya baadhi ya waajiri kutopeleka michango ya wastaafu ambayo imesababisha Wabunge kwa vipindi tofauti. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hata Kiti chako umeshakuwa ukizungumzia suala hili la madeni marefu ya waajiri kwenye mifuko ambayo yanasababisha wazee wetu ambao wamefanya kazi wa weledi kulitumikia Taifa hili wanapata usumbufu wa kupata mafao yao. Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alitoa maelekezo na aliyarudia maelekezo yake hata wakati wa Mei Mosi kwamba Wizara yetu ichukue hatua mahususi za kufuatilia madeni hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maelekezo hayo, lakini kama ambavyo hata Ripoti ya CAG kwenye Taarifa ya PAC imebainisha kwamba NSSF walikuwa na michango ya kiasi cha shilingi bilioni 408 ambazo zilikuwa bado hazijakusanywa kutoka kwa waajiri mbali mbali.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelekezo ya Mheshimiwa Rais na kwa kuzingatia kwamba hizi ni hoja za muda mrefu kwa kweli niseme kwamba CAG pamoja na Mheshimiwa Rais ametusaidia kufikiri nje ya box, ametuwezesha tumeunda Kamati Maalumu ya kufatilia fedha hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba nilijulishe Bunge lako Tukufu tangu tumepokea Ripoti ya CAG kutokana na kazi kubwa na nzuri ambayo imefanywa na timu mahususi ambayo tumeiunda tumefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 200.6 kati ya bilioni 408 zilizobaki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafurahi kwamba Bunge lako kwa kweli linazungumza kwa hisia kwa uchungu kwa sababu haya ni maisha ya watu, haya ni maisha ya wazee wetu ambao ndiyo walituwekea misingi sisi leo tunajivuna katika Taifa hili ni kwa sababu kazi kubwa ya hawa wazee wetu mbao ni wastaafu waliifanya kwa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa namna yoyote ile ni lamiza Serikali tutahakikisha kupata fedha zilizobaki ambazo bado hatujakusanya tutahakikisha tunazifanyia kazi…

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Profesa Ndalichako kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jesca Msambatavangu.

TAARIFA

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa maelezo mazuri ya Mheshimiwa Waziri na task force aliyoiunda. Tunafahamu kwamba wamekaa kikao cha Mock LAAC kati ya Septemba na Oktoba ambacho kina-clear out zile hja zote za CAG kwa maelezo haya anayosema kwa task force waliyoiunda. Nataka kujua hiyo task force yake anasema imefanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Spika, mpaka tunakuja sasa hivi kwa Taarifa hii CAG ametuambia wapo wafanyakazi wa Jiji la Tanga walichangishana milioni 8 wakailipa PSSSF ili wapate mafao yao. Kwanza nataka kujua hiyo task force yake inajua kwamba hilo linafanyika, na wamechukua hatua gani, na je? … (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Msambatavangu Taarifa ni moja. Ahsante sana

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, naomba hiyo task force yake imefanya nini kwenye masuala, na wanakusanya hiyo michango kwa Sheria ipi unakwenda kuchukua mchango kwa mtumishi au mstaafu na sio kwa mwajiri.

SPIKA: Mheshimiwa Profesa Ndalichako. Ameuliza swali kwa hiyo hulazimiki kujibu.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, sawa lakini kwa faida ya Wabunge taarifa hii ya Kamati bahati nzuri ime-acknowledge haya ambayo tunayasema. Mafanikio haya yaliyopatikana tungeyaripoti kwenye kamati na Kamati imeonyesha kwamba kulikuwa na deni la milioni 407 na ikasema kwamba wakati Kamati inafanya kazi yake jumla ya bilioni 194 zilikuwa zimekusanywa.

Mheshimiwa Spika, hatulali. Tangu kipindi cha Oktoba tulipotoka kwenye Kamati tumeshakusanya bilioni 6 nyingine. (Makofi)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kwenye eneo lingine.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Profesa Ndalichako kuna Taarifa nyingine kutoka kwa Mheshimiwa Ester Bulaya.

TAARIFA

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, mimi ni Mjumbe wa LAAC, ni jeshi ulilonihamishia hivi karibuni nilikuwana napenda kumpa Taarifa Mheshimiwa Waziri kwamba mpaka juzi kwenye halmashauri michango ambayo haijapelekwa kwenye mfuko bilioni 260 ya watumishi wa Taifa hili. (Makofi)

SPIKA: Haya Waziri Mheshimiwa Profesa Ndalichako.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, dada yangu Ester Bulaya anawaisha shughuli. Anachokisema ndiyo ilikuwa sehemu ambayo naendelea na mchango wangu. Ni kweli kwamba katika halmashauri zetu kumekuwa na michango ambayo haijawasilishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama navyosema tupo kazini kuhakikisha kwamba hii kero ya muda mrefu tunaifanyia kazi. Katika michango ya halmashauri tuliunda na yenyewe hiki kikosi kazi kilikuwa kinashughulikia mfuko wa NSSF lakini na PSSSF tulikuwa na task force nyingine kwa sababu hawa ni watumishi wa umma ambao ilijumuisha Makatibu Wakuu wanaohusikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika TAMISEMI naomba niripoti kwenye Bunge lako kwamba tayari…

SPIKA: Ngoja amalizie.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, tayari tumeingia makubaliano na halmashauri 81 ambazo zina madai ya muda mrefu na halmashauri hizi 81 zimetuwezesha kuwakomboa wastaafu 1425 ambao walikuwa na madeni ya muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia kwa faida ya Watanzania na kwa sababu hili jambo limekuwa ni kero ya muda mrefu nichukue nafasi hii kumwagiza Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF kuzifuatilia halmashauri ya 103 ambazo hazijaweka makubaliano ya namna gani wataleta michango yao. (Makofi)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, nimuombe kaka yangu Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI Mchengerwa mchapakazi mtu bingwa nitakukabidhi orodha ya hawa watu wa TAMISEMI ili waweze kuleta fedha tuweze kulipa mafao wastaafu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri umemaliza mchango wako kuna Mbunge alikuwa anataka kutoa Taarifa, itabidi, maana dakika yake ya mwisho ilikuwa imeshaisha lakini namna unavyosisitiza ni kama vile una jambo la dharura.




TAARIFA

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa mawasilisho ya Waziri. Kuna wastaafu ambao walishastaafu na wakaamua kwenda kukopa fedha kwengine ili waende walipe yale malimbikizo ambapo hawajapeleka pamoja na penati sasa wakishalipa ina maana wanalipwa fedha zao kutoka kwenye mfumo tayari unakuta hawasomeki.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nampa Taarifa kwamba hiyo task force aliyoiunda ihakikishe kwamba inawafatilia wale wote ambao wameshatoa hela zao wakalipa yale malimbikizo kwa hela zao zingine kwa sasa walizopata na penati ili wawatafute wahakikishe kama wanalipa zile fedha zao kihalali warudishiwe zile hela ambazo walikopa kwa…

SPIKA: Haya ahsante sana. Mheshimiwa Waziri Ndalichako.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, kwa faida ya Watanzania kwa sababu suala la wastaafu linaguza wazee wetu na wazee ni nuru ya Taifa. Kwa faida ya wazee wetu niseme kwamba utaratibu ambao upo Kisheria control number ya kulipa michango inapelekwa kwa mwajiri.

Mheshimiwa Spika, sasa kama kuna mwajiri ambaye anampa mtumishi ile control number ili akalipie tupate taarifa tutashughulikia kwa sababu utaratibu wa Kisheria upo kwa hiyo, tumepokea ushauri wake.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge kama wanafahamu waniletee tutafanyia kazi, ni hilo tu. (Makofi)