Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hoja zetu tatu zilizopo mbele yetu. Mchango wangu kwanza utajikita kwenye Azimio la Bunge ambalo lilitolewa mwaka jana kuhusu kuhamisha KADCO kwenda TAA.

Mheshimiwa Spika, hakuna mtu yeyote kwenye Serikali ambaye anapingana na maagizo ya Bunge na sisi kama Serikali tunathamini sana maagizo yanayotolewa na Waheshimiwa Wabunge pamoja na Bunge lako Tukufu. Mara baada ya kikao kile tulianza kujipanga kwenda kuangalia jinsi gani tutaweza kutekeleza agizo hili, lakini kulitokea changamoto kubwa kuhusu Sheria ya TAA ambayo ni sheria ya Executive Agency, Act No.3 ya mwaka 1977 hairuhusu utaratibu wa kutoa hizo fursa moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, baada ya kushauriana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, tuliamua kutengeneza sheria mahususi ya TAA ambayo itaruhusu uendeshaji na uendelezaji kupewa Taasisi za Serikali na Private Sector. Sheria hiyo imepita katika maeneo mbalimbali na ngazi mbalimbali na wadau mbalimbali wametoa maoni. Tarehe 20 mwezi uliopita, Serikali ilitoa maamuzi kwamba sheria hiyo iundwe ambayo itatoa fursa mahususi sasa kwa ajili ya mpango huo wa kuhamisha KADCO kwenda TAA, pamoja na kuipa fursa TAA kuingia mikataba na kampuni za private, pia kuipa fursa TAA kushirikiana na Taasisi mbalimbali za Serikali.

Mheshimiwa Spika, hatua tuliyofikia sasa sheria inaendelea kutungwa na Bunge letu linalokuja la Februari, sheria hiyo itawasilishwa hapa Bungeni ili Waheshimiwa Wabunge waijadili. Naamini kwa hamu waliyonayo sheria hiyo itapita na tutaendelea kufanya mchakato wa kuhamisha KADCO kwenda TAA bila matatizo

Mheshimiwa Spika, tulilazimika kwenda na utaratibu huo kwa sababu tulitaka na sisi tusivunje sheria. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba, KADCO ni Kampuni ya Serikali ambayo ipo chini ya Msimamizi wa Msajili wa Hazina na itaendelea kuwa hivyo hata ikienda huko TAA, kwa sababu, kampuni zote hizi za Serikali zipo chini ya Msajili wa Hazina.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nijikite kwenye hoja za CAG…

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.
SPIKA: Mheshimiwa Mbarawa kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mtemvu.

TAARIFA

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri anazungumza vizuri juu ya jambo la KADCO, kwamba, sasa hivi wanatengeneza sheria ili TAA iweze kuimiliki na hii private company. Tukiwa tunatambua TAA inamiliki viwanja vingine Tanzania hapa ambayo tungeamini na KIA kingekuwa ndani. Kama Kamati, nikiwa Mjumbe wa PAC tunatambua KADCO imemaliza mkataba wake uliokuwepo Tarehe 16 Mwezi Julai, 2023. Sasa, Mheshimiwa Waziri atuambie sasa hivi KADCO inaendelea kuwepo pale kama nani? Ikiwa haina mkataba wowote na mkataba wake umeisha?

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, pengine hii hoja ya KADCO inaleta ugumu kidogo kwa sababu nakumbuka mwaka jana na ninayo Hansard hapa, Bunge lilikuwa kali sana kuhusu jambo hili. Serikali ilikuwa imeshatoa maelezo inaenda kufanyia kazi Maazimio ya Bunge. Hili ni Azimio mojawapo ambalo ni kati ya yale ambayo Bunge limeazimia, Serikali ikaleta taarifa Juni, ikasema jambo hili wameshafikia hatua nzuri kufikia sijui mwezi wa ngapi litakuwa tayari na sasa tena tunaambiwa bado. Sasa naambiwa huko na Wajumbe wa Kamati kwamba mkataba ukwisha. Mkataba umekwisha lakini KADCO bado wapo.

Waheshimiwa Wabunge, wakati huo huo KADCO ni ya Serikali, wakati huo huo haiwezi kukabidhi kiwanja TAA ambayo nayo ni ya Serikali. Sasa, mazingira hayo Mheshimiwa Waziri, leo nitakupa muda wa kutosha tuelewe vizuri hili jambo la KADCO, kwa sababu, lina Azimio maalum la tangu mwaka jana.

Mengine yote najua huko mwishoni nitapata nafasi ya kuzungumza lakini hili la KADCO kelele zilikuwa nyingi na Mheshimiwa AG upo hapa, nitawapa nafasi wewe na Mhehishimiwa Waziri mtueleze vizuri hilo jambo. Kwamba, viwanja vingine vyote vimewezekana kwenda TAA, isipokuwa kiwanja cha KIA kimeshindikana kwa sababu KADCO yupo pale na ni wa Serikali. Sijui ugumu unatokea wapi mpaka mnahitaji sheria mpya ili TAA akabidhiwe KADCO. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri, halafu Mheshimiwa AG.

WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, TAA inaendesha viwanja 54 vya Serikali, KADCO hakipo. Vilevile TAA ni taasisi ambayo ipo chini ya Msajili wa Hazina. KADCO sasa ipo chini ya Msajili wa Hazina. Sasa, kwa Sheria ya TAA ilivyo sasa kama nilivyosema na Sheria ya KADCO ilivyo, hatuwezi kuihamisha KADCO moja kwa moja kuipeleka TAA kwa sasa.

SPIKA: Malizia, nawasha najiandaa.

WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, tuliomba ushauri kwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu kuhusu jambo hili na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ikatwambia kwa jambo lilivyo kwa kuwa kampuni hizi ni tofauti, ile moja ni kampuni ambayo imenzishwa kwa Executive Agency, nyingine imeanzishwa kwa utaratibu mwingine, inabidi muanzishe sheria maalum ambayo itaifanya TAA kuchukua viwanja kwa mfano cha KADCO na viwanja vingine vya private.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala hili ni kweli KADCO muda wake wa uendeshaji umemalizika, lakini na hilo tulilipeleka kwa Mwanasheria Mkuu akasema, hili lazima tuandike waraka kupeleka kwenye mamlaka na tumefanya hivyo, tupo katika hatua za kutolewa maamuzi.

SPIKA: Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, kwanza niunge mkono sehemu ya maelezo iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana na Uchukuzi. Suala la KADCO lina historia ambapo uamuzi wa awali kabisa ulikuwa ni Serikali kuichukua hisa zote kwenye kampuni hiyo. Hilo likakamilika.

Mheshimiwa Spika, hatua ya pili, katika hatua ya kuhamishia TAA kukajitokeza kulikuwa na liabilities za KADCO ambazo hazikuwa sahihi, TAA izirithi. Kwa hiyo, pamoja na Azimio la Bunge hili, vilevile kulikuwa na maamuzi ya Baraza la Mawaziri. Waziri alilazimika kurejesha suala hili kwa kutoa taarifa kwenye mamlaka zinazohusika na baadaye sasa maamuzi yamekwishafanyika kama alivyosema Mheshimiwa Waziri. Kwa sasa, concessional agreement imemaliza muda wake mwezi Julai, lease agreement muda wake utaisha mwezi wa kumi na moja.

Mheshimiwa Spika, kipindi hiki hapa katikati, kabla Bunge hili halijafikia mwisho wiki ijayo, naamini mchakato wa kuletwa Bungeni kusomwa mara ya kwanza kwa Sheria ya TAA ambayo sasa itakuwa imewekea mawanda makubwa ya kuendesha viwanja vyote vya ndege nchini, nafikiri sasa tutakuwa tumefikia kwenye ukamilifu wa Azimio la Bunge la mwaka jana.

Mheshimiwa Spika, nashukuru.

SPIKA: Mwanasheria Mkuu wa Serikali tusaidie, hii KADCO mkataba umeisha, inafanya kazi. Unasema liabilities za KADCO ambazo hamkutaka ziende TAA ndiyo zilizozuia kumalizika huu mkataba. Hizi liability, maelezo ya ukweli kabisa ni kwamba asilimia mia moja KADCO inamilikiwa na Serikali, nipo sahihi? Kama hivyo ndivyo, maana yake Serikali si inamiliki na na hizo liability ama liabilities ameachiwa yule aliyekuwa mmiliki wa KADCO kabla Serikali haijachukua umiliki? (Makofi)

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, kwa sababu KADCO kama kampuni iliyosajiliwa chini ya Sheria ya Makampuni ilikuwa ina hadhi za kisheria. Kwa hiyo, transition iliyofanyika baada ya Serikali kuwa na hisa zote ilikuwa ni kuiweka sasa chini ya muundo wa Serikali ambapo sasa mambo ambayo yanafanyika sasa, nafikiri ni yale ninayosema, hatua mojawapo ni kisheria. Hii ni baada ya ile lease agreement, moja, haitakuwa na mkataba wowote; lakini pili TR ambaye kwa sasa ndiye msimamizi mkuu, nafikiri chini ya Wizara husika, kwa sababu kufikia Februari sheria itakuwa imepita, naamini…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa AG endelea au ulikuwa umemaliza?

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nilikuwa naamini kwamba kwa sababu kuna utaratibu..

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, baada ya ule Muswada, wiki ijayo unaposomwa kwa mara ya kwanza, utakuwa umeshawekwa tayari, utakuwa umeshakuwa umeshakuwa gazetted.

SPIKA: Kwa sasa nani anaendesha kiwanda cha KIA?

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, ni KADCO chini ya usimamizi wa Serikali.

SPIKA: KADCO ambaye mkataba wake umekwisha. (Makofi)

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, Lease agreement haijafikia ukomo.

SPIKA: Hii ndiyo Novemba unayoitaja au ni Novemba mwakani? Maana umesema mwenyewe hapa, Mwezi wa Kumi na Moja na ndiyo leo hapa tupo Tarehe 4 Mwezi wa Kumi na Moja. Ni mwezi huu au ni Mwezi wa Kumi na Moja mwakani?

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, no ni Mwezi wa Kumi na Moja, mwaka huu.

SPIKA: Mwaka huu?

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, ndiyo.

SPIKA: Sasa, kwa kweli kwenye jambo hili mnalipa Bunge wakati mgumu. Kwa sababu kama kampuni hiyo ya KADCO ambayo umiliki asilimia 100 ni wa Serikali na iko chini ya Msajili wa Hazina, Mkataba wake umeisha bado iko site inafanya kazi. Masharti yake ya uendeshaji wa kiwanja, huo mkataba ulishaisha. Uliobaki sasa hivi ni wa lease pekee. Sasa ule wa lease unawaruhusu kweli kuendesha uwanja? Mheshimiwa AG, hii Lease Agreement inawapa wao mamlaka ya kuendesha uwanja baada ya mkataba kuisha? Kwa sababu kisheria mseme hivi, tumewaongeza muda kwa sababu tunataka tubadili sheria. Ukisema mkataba umeisha bado wako pale wanafanya nini? (Makofi)

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, nafikiri tunaongea lugha moja. Kwa sababu ninaposema TR ndiye anayesimamia kama makampuni mengine ambayo yako chini ya Serikali, maana yake Katibu Mkuu mwenye dhamana na Waziri mwenye dhamana wana usimamizi wa moja kwa moja. Hii transition ninayoisema ya kuletwa sheria, maana yake lengo lake kubwa itakuwa ni kuipa ile comprehensive mandate TAA kuweza kuendesha operations za viwanja vyote nchini.

SPIKA: Yaani mimi nakuelewa sana. Aweze huyo TAA kuendesha viwanja vyote, isipokuwa KADCO mpaka anahitaji sheria? Sheria mpya inahitajika kwa ajili tu ya KADCO? Haya Mheshimiwa Waziri malizia mchango wako. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, Mwongozo wa Spika.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, nimewasikia lakini sasa Mheshimiwa Waziri alikuwa ameshasimama na mwongozo unaombwa akiwa hajasimama. Kwa hiyo, nimewaona wacha Mheshimiwa Waziri amalizie halafu nitawapa nafasi. Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kwa ufupi tu kama Mheshimiwa AG alivyosema, sisi tumeshaandika kuomba Serikali ili kwa kipindi hicho tupate angalau hicho kibali tuweze kumpa mpaka hapo sheria mpya itakapotungwa.

MHE. CHRISTOPER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, hiyo Serikalini linaendelea.

MHE. CHRISTOPER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: KADCO, KADCO, KADCO!

MHE. CHRISTOPER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Saashisha Mafuwe.

MWONGOZO WA SPIKA

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, jambo hili hapa ndani linaleta mkanganyiko mkubwa sana. Kule site kwa wananchi lina mkanganyiko mkubwa zaidi. Sasa hivi kuna zoezi linaendelea, kulipa fidia, Mheshimiwa Rais ametoa bilioni 11, wananchi wameelimishwa wameelewa na haikuwa kazi rahisi. Nilikuwa naenda site mimi kuzungumza nao, wakiwa na hasira kubwa mno, wameelewa jambo hili. Sasa, sasa hivi wanasikia tena wanapisha uwanja wao kwa mapenzi kwamba uwanja ni mali ya Serikali, hapa ukisikiliza hii sentensi maana yake ni kwamba KADCO sasa haijulikani ni ya nani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Mwongozo wako, ikiwezekana Serikali ipewe muda ndani ya wiki hii, Jumatatu au Jumanne walete tamko ili kuondoa confusion, kwa sababu tukiliacha hivi kule site litatuletea vurugu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukisikiliza maelezo ya Mheshimiwa Waziri pamoja na Mwanasheria ni dhahiri kwamba KADCO inaelea mahali, haina mwenyewe. Sasa ili tupate sentensi tusichanganye wananchi. Kama sisi humu ndani vinatuchanganya kule site itakuwaje? Mtatupa kazi kubwa na zoezi lile linaloendela kule.

Mheshimiwa Spika, naomba sana utupe Mwongozo wako lifikie mwisho, tupate sentensi ya Serikali itakayoeleweka kwa wananchi, kwamba KADCO ni nani?

SPIKA: Haya ahsante sana. Mheshimiwa Ole-Sendeka.

TAARIFA

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kutoa taarifa. Bunge hili ni Bunge lililopo kwa mujibu wa Katiba na Maazimio ya Bunge yanapaswa kuheshimiwa, kwa sababu Bunge linapofanya maazimio na sehemu ya pili Serikali ipo, kwa maana ya Waziri Mkuu, Mawaziri na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri, maelezo yote yaliyotolewa na Attorney General ambae ninamheshimu sana, pamoja na Profesa ambaye ninamheshimu sana, kwa kweli hayana sababu yoyote (hayatoi sura nyingine) isipokuwa Serikali kupuuza kutekeleza Azimio la Bunge. Hakuna lugha nyingine ya kistaarabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine lililo kubwa zaidi, nchi hii tuna uzoefu, kuna taasisi nyingi za Serikali ambazo shughuli zake zimetoka kutoka taasisi hii kwenda taasisi nyingine, taasisi zote hizi mbili ziko chini ya TR, mnashindwa nini leo kuihamisha, ili kama mnataka kubinafsisha tena TAA au viwanja vinavyosimamiwa na TAA, mje muuze tu kwa bei ya jumla, kama ndiyo mmeamua kuelekea huko, kwa sababu kuna hatari, nami nataka niwaambieni…

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

SPIKA: Sekunde 30, malizia.

MHE. CHRISTOPER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, haya, namalizia. Jamani naomba muone hali ni mbaya sana. Tumesomesha vijana wengi, darasa alilokuweko Dkt. Tulia Ackson na alilokuwepo Prof. Mbarawa kuna wenzenu mlisoma nao, kama ninyi mmeweza kuongoza taasisi hizi kubwa, hivi kweli hamna Watanzania wanaoweza kumudu kuendesha hivyo viwanja vya ndege mpaka muwe na mawazo yote ya kukabidhi kila kitu ughaibuni? Naomba niwaambie hayawafurahishi wapiga kura wetu na haifurahishi Taifa. KADCO iondoke, ikabidhiwe TAA na viwanja vya ndege viongozwe na Watanzania wenyewe. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, Mwongozo wa Spika.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tutulie kidogo, tutulie kidogo. Mheshimiwa AG hebu nisaidie, nani alikuwa anamiliki hicho kiwanja kabla KADCO hawajaja? Maana siyo KADCO waliojenga, ama ni KADCO wamejenga? Nani alikuwa anamiliki hicho kiwanja kabla ya KADCO? Waziri au nani anataka kujibu?

SPIKA: Waheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, Kiwanja cha KADCO kwanza kilikuwa Kiwanja cha Serikali, I mean Kiwanja cha KIA.

SPIKA: KADCO haina kiwanja ni kiwanja cha KIA.

WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika ni kiwanja cha KIA…

SPIKA: Kiwanja cha KIA.

WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, Kiwanja cha KIA kilikuwa Kiwanja cha Serikali, halafu wakati wa ubinafsishaji, ikaundwa kampuni ambayo kuna baadhi ya watu wa private sector waliingia. Mwingereza nafikiri kampuni ya Kiingereza MacDonald pamoja na Kampuni ya South Africa. Baada ya kuona ule utaratibu uliowekwa siyo wa kuridhisha, Serikali ikaamua kuununua na wakalipa hiyo hela na ikatoa maelekezo huku nyuma kwamba kiwanja hicho kirejeshwe kwa TAA lakini kwa nini hakikuweza kurejeshwa kwa wakati huo wote.

Mheshimiwa Spika, sasa, KADCO sasa hivi ilivyo ni kampuni ya Serikali chini ya asilimia 100 na KADCO sasa hivi inaendeshwa na Mtanzania, haiendeshwi na watu wa nje na wafanyakazi wale wote ni Watanzania.

SPIKA: Sasa, nisaidie jambo jambo moja halafu tuendelee mbele Waheshimiwa Wabunge. Hii KADCO, maelezo yanayotoka ndiyo yanayotupa wasiwasi kama Bunge. KADCO asilimia 100 ni ya Serikali, kwa nini hii mijadala huwa inakuja na kwenda? KADCO asilimia 100 ni ya Serikali, TAA asilimia 100 ni ya Serikali, shida iko wapi ili Bunge tusaidie kwenye hiyo shida, tukwamue huo mkwamo ambao unatokea kati ya KADCO na TAA. (Makofi/Kicheko)

WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, tunakoelekea sasa hakuna mkwamo, kwa sababu kama alivyosema Mwanasheria Mkuu wa Serikali, wiki hii italetwa sheria ya kusomwa mara ya kwanza ambayo itaweka mawanda yote kwa ujumla ya kuondoa KADCO kwenye TAA.

MJUMBE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Sasa unajua hizi taarifa zimetukutia katikati kwamba na mkataba umeisha na hapa tuko Bungeni na sisi tutakuwa sehemu ya huu mchakato, tutakuwa sehemu, Serikali hebu itufafanulie huyu KADCO atafanyaje kazi, anaendeleaje kufanya kazi wakati mkataba haupo? Mwanasheria Mkuu wa Serikali, tufafanulie hilo tutoke hapa tukijua kwamba huo uwanja wa Watanzania uko salama pamoja na KADCO kuendelea kuendesha wakati mkataba haupo.

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, nafikiri ufafanuzi wa kwanza ni kuomba subira kama ilivyo subira yavuta kheri kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Spika, hakuna ubishi juu ya umiliki wa uwanja kwa Serikali, vilevile, hakuna ubishi juu ya uamuzi wa Serikali ku-take over. Pia, hakuna ubishi juu ya Azimio la Bunge hili la mwaka jana la shughuli zote za KADCO kuhamishiwa TAA. Sasa Taarifa ya Serikali kwamba, Baraza limekwishaamua na Serikali inaleta hapa Muswada, Muswada ambao kwa mujibu wa taratibu mnajua kwamba Bunge hili ndiyo litakuwa na dhamana ya kuujadili na kuupitisha.

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kinachoweza kufanyika labda wiki ijayo Serikali iweze kuleta maelezo ya kuelezea hiyo transitional arrangements zilizosalia.

SPIKA: Sawa. Sasa Waheshimiwa Wabunge, nitamruhusu Mheshimiwa Mgungusi halafu kwenye hoja hii tutafanya maamuzi sasa halafu tusonge mbele. Mheshimiwa Mgungusi.

TAARIFA

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Nafikiri kwa kifupi, mimi sijaona nia ya dhati, tuseme Wizara ya Uchukuzi, kama siyo Serikali juu ya sakata hili la KADCO na KIA. Maelezo ya Mheshimiwa Waziri na AG, yanazungumzia mchakato ulivyokuwa mgumu kuhamisha KADCO kwenda TAA ambazo zote zinasimamiwa na TR. Hatukuazimia kwamba KADCO iende TAA, hoja yetu ni ule Uwanja wa KIA ndiyo wakwetu, Uwanja wa KIA uende TAA, hauhitaji sheria na mchakato. Kwa hiyo, mchakatao ufuatwe namna ya ku-dissolve KADCO au KADCO kampuni tanzu ya TAA, hilo ni jambo la kisheria la baadae. Issue yetu ilikuwa siyo KADCO kama lilivyo, Uwanja wa KIA mara moja uende TAA ndiyo ilikuwa ajenda hata mwaka jana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la nyongeza tu, nasema nia ya dhati haipo kwa maana ya kwamba, Menejimenti ya KADCO wanaendelea kuongea kwamba, Azimio la mwaka jana la Bunge limetolewa lakini bado wao hawatofanya kama vile ambavyo inapaswa, kwa maana KADCO itaendelea ku-run uwanja. Kwa hiyo, kilichopo sasa hivi wanapambana huko uvunguni, wanafanya lobbying kwamba Azimio la Bunge lisitekelezeke. Hicho ndicho kinachoendelea KADCO sasa hivi. (Makofi)

SPIKA: Mwanasheria Mkuu wa Serikali, naona ulisimama.

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, nilisimama kumpatia taarifa Mheshimiwa Mbunge, ninaemheshimu sana kwamba siyo taarifa yangu wala siyo taarifa ya Mheshimiwa Waziri iliyotolewa hapa kwamba Serikali ina mpango wa kuihamishia KADCO, TAA.

WABUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, mwongozo wa Spika.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tutulie kidogo. Mheshimiwa Waziri wa Nchi, naona umesimama.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hoja ambayo iko mezani kwetu ni hoja ya CAG na hoja hii ya CAG ni hoja ambayo inashirikisha pande zote mbili katika kufanya majadiliano. Serikali lakini ni hoja ya Bunge kwa maana ni hoja inayomilikiwa na Kamati za Bunge.

Mheshimiwa Spika, kama itakupendeza, kwa kuwa bado Kanuni zinaturuhusu ambazo hazizuii mjadala huu kuendelea na kuhitimishwa kwa mujibu wa utaratibu. Kama Bunge lako itakupendeza, Mheshimiwa Waziri ametoa maelezo na Mwanasheria Mkuu amatoa maelezo na kwa kuwa tayari Serikali inaonesha kwamba ina hatua ambazo zimekwishachukuliwa.

Mheshimiwa Spika, kama itakupendeza basi katika Bunge, Mkutano huu Serikali tupate nafasi ya kuja kutoa kauli yetu ya Serikali kuonesha hali halisi ya mahali tulikotoka, mahali tulipofikia na hasa katika katika kutekeleza agizo la Bunge na kutekeleza maagizo yote ambayo yalitolewa pia na Baraza la Mawaziri ili tuweze kupata uelewa mzuri wa pamoja, ikikupendeza. (Makofi)

MHE. HALIMA J. MDEE – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI ZA MITAA (LAAC): Mheshimiwa Spika, Mwongozo wa Spika.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, Mwongozo wa Spika.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, amesimama hapo Mheshimiwa Waziri, pia nafikiri tulimsikia Mwanasheria Mkuu wa Serikali akiomba pengine wiki ijayo wapewe muda waje watoe maelezo, lakini changamoto iliyopo ni kwamba, kauli za Serikali huwa hazijadiliwi, unasema halafu tunakuwa tumeelewa kwenye hoja hiyo.

Hoja ya msingi iliyopo mezani sasa, ni kwamba Bunge liliazimia, Serikali ikatoa majibu kuashiria kwamba hilo jambo limeshafika mahali, sehemu. Sasa leo tena imekuja na maelezo ya ziada. Kwa sababu hii Taarifa ya CAG ambayo inajadiliwa leo ni ya tangu Machi na hapo majibu yalishatokea, yalishatokea yalishatokea. (Makofi)

Februari mwakani siyo muda mrefu, lakini hoja iko pale pale. Hii KADCO ni ya Serikali na TAA ni ya Serikali, yaani KADCO inataka kulisimamisha Bunge? Yaani KADCO kama kampuni inataka kulisimamisha Bunge? Sawa, tuendelee na michango. Tutafanya uamuzi, sisi ndiyo Bunge tuko hapa na ndiyo kazi yetu kuisimamia Serikali. (Makofi)