Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Awali ya yote namshukuru sana Mwenyezi Mungu kutujaalia uzima. Pia naomba niwashukuru wananchi wa Mkoa wa Rukwa kwa kuniamini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa umahiri wake wa kazi, uwajibikaji na kuiletea heshima Serikali. Nimpongeze pia Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa kuchaguliwa kwake na uchapakazi wake. Niwapongeze Mawaziri wote na Manaibu wote kwa uchapakazi wao mzuri, hakika tunayo majembe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niunge mkono hoja wakati nikitaka ufafanuzi wa hoja zifuatazo; Mkoa wa Rukwa uliiunga mkono Serikali hii kwa kukipatia Chama cha Mapinduzi kura nyingi sana za kishindo, sasa nipe nikupe. Je, uwanja wa ndege wa Sumbawanga utaanza kujengwa lini? Wananchi wanapata shida sana kutokana na umbali, hasa wanaposafiri kwenda Dar es Salaam ambako huduma nyingi za Serikali hutolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wananchi wa Sumbawanga, wenyeji wa Bagwe, wanaoishi pembezoni mwa uwanja walifanyiwa tathimini ya nyumba zao muda mrefu kwamba watalipwa na nyumba zao zikawekwa alama ya “X” kwa muda mrefu. Mpaka sasa hawajalipwa na wanakosa huduma muhimu za kibenki na huduma nyingine mbalimbali, je, watalipwa lini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ningependa kuishukuru Serikali kwa kutambua umuhimu wa Barabara ya Sumbawanga - Mpanda - Nyakanazi yenye urefu wa kilometa 346.6 kwani barabara hii ni kiungo muhimu cha mawasiliano. Lakini kuna barabara ya Kibaoni - Muze - Mtowisa - Ilemba - Kilyamatundu kilometa 200 ijengwe kwa kiwango cha lami kwani ukanda huu wa Bonde la Ufa ndiko mazao mengi yanatoka huko kama ngano, asali, mpunga, samaki, ufuta na mazao mengine. Kwa hiyo, ni vema ikajengwa kwa kiwango cha lami na madaraja yajengwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo barabara ambazo zinasimamiwa na Halmashauri ambazo hawawezi kuzihudumia kutokana na fedha wanazozipata, ikiwemo Kalambazite - Ilemba ambapo hii barabara iliomba ibadilishwe iwe ya TANROADS kwa sababu inakidhi viwango na nyingine ni barabara ya Miangaluna - Chombe, Mtowisa - Kristo Mfalme, Mawenzusi - Msia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sijajua Serikali inafikiria nini juu ya mgogoro wa shamba la Efatha ambao ni wa muda mrefu. Wananchi wanapata shida hata kupitisha barabara, matokeo yake wananchi wameendelea kuwa maskini kwa kushindwa kuwasomesha watoto. Naomba Serikali yako sikivu iwarudishie shamba hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nichukue fursa pekee kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano ambayo ni ya Hapa Kazi Tu, chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kwa uamuzi wa kununua ndege zetu. Hii itatujengea heshima kubwa na tutaendelea kumuunga mkono Rais wetu kwa jitihada zake za kutumbua majipu na kukusanya kodi kwa wingi na hususani Mkoa wa Rukwa. Naunga mkono hoja.