Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kuchangia katika hoja iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, ninaipongeza Serikali kwa kuja na bajeti nzuri, nimshukuru Mheshimiwa Rais wetu mama yetu Samia kwa kuweza kuruhusu kuanzisha dirisha maalum kupitia TASAF itakayosaidia watoto wanaotokea familia maskini. Watoto wengi wanaotoka katika familia maskini wamekuwa wakifaulu vizuri sana na kupangiwa mbali na kushindwa kumudu gharama. Kwa hiyo, kupitia mpango huu kutawasaidia hawa vijana wetu waweze kutimiza ndoto zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee na mchango wangu katika hoja yetu hii katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri katika eneo la mazingira ya biashara ndogo ndogo na sekta binafsi, ameelekeza kwamba wataitoa asilimia tano iende ikatengeneze miundombinu pamoja na masoko kwa ajili ya wamachinga. Naomba Serikali iahirishe kwanza hili jambo kwa sababu mazingira katika maeneo yetu yanatofautiana. Hivyo ikafanye tathmini pamoja na kuangalia fursa zilizopo katika maeneo yetu ili waone kama tunauhitaji wa kujengewa yale masoko na miundombinu ya Wamachinga vinginevyo miundombinu hii itakwenda kukaa bila kuleta tija yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema kwamba toka tupitishe sheria yetu mwaka 2018 Wakurugenzi wamekuwa wakichangia kwa kasi asilimia 10 katika makundi yaliyotajwa katika sheria hii na kuleta tija, katika kuinua wananchi wetu vijana wetu na wakina mama kiuchumi, tutakapowaondolea asilimia tano tutaendelea kuwadidimiza. Pamoja na Serikali ilitoa maelekezo kwamba mifuko yote ya uwezeshaji kiuchumi iweze kuunganishwa Pamoja, iweze kuhudumia vijana, lakini mpaka leo katika Wilaya ya Meatu hatujawahi kupata mfuko wowote kwenye hiyo mifuko ya uwezeshaji kiuchumi. Kwa hiyo, tutakapopunguza hii asilimia tano tutaendelea kuwapunguzia uwezo wa kujijenga kiuchumi vijana wetu na wakina mama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, mazingira ya Meatu hayaruhusu kuwa na miundombinu ya kimachinga kwa sababu ya vikundi vinavyojishughulisha na shughuli tofauti ambazo hazihitaji miundombinu hii. Shughuli hizi ni kilimo cha vitunguu, kilimo cha ufugaji ng’ombe, ambao soko lao ni kupeleka minadani tayari soko lipo, kwa ajili ya ile mifugo na mingine inasafirishwa kwenda Dar es Salaam tena inaleta matokeo kwa haraka. Kama asilimia tano itatumika kujenga miundombinu wa wamachinga pale, sioni mwananchi anayetoka Mwasengera kilomita 120 kuja pale makao Makuu ya Wilaya atanufaikaje na hiyo miundombinu. Kwa hiyo, miundombinu hii itakaa idle bila kuleta tija yoyote kwa vijana wetu, labda nimuombe tu Mheshimiwa Waziri aongeze ifikie hata asilimia tano ziwe 15 ili ziweze kunufaisha na kuziba zile pengo la mifuko ya kiuwezeshaji kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika maoni ya Kamati ya Bajeti iliongelea kwamba kilimo ni moja ya sekta ambazo ni nguzo kuu ya maendeleo ya viwanda kwa sababu ndio malighafi zinazopatikana. Mimi naunga mkono maoni ya Kamati kwa sababu zifuatazo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza Serikali iwekeze zaidi katika mazao ambayo inayaona ni malighafi kwa ajili ya viwanda vyetu. Kwa mfano, Kamati ilitembelea Kiwanda cha Nguo cha NIDA kiwanda kile kilionekana kinaupungufu mkubwa wa malighafi ambayo ni pamba, pia Serikali inataka kufufua viwanda vingi vya ginnery kikiwemo kiwanda cha solar, hata viwanda vilivyopo havina malighafi ya kutosha kwa sababu msimu wao unakwenda miezi mitatu tu ile pamba inakuwa imekwisha. Zao hili pamoja na mazuri yaliyofanywa na Serikali mimi nimshukuru Rais kwa miaka miwili mfululizo, bei ya pamba imepanda juu maradufu kuliko miaka ya nyuma ilivyokuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ninamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kusamehe madeni ya pembejeo kwa ajili ya wakulima wa pamba. Nimshukuru kwa sababu, zao hili limekuwa na changamoto nyingi sana kuanzia pembejeo ya kuua wadudu pamoja na mbegu. Pamoja na ukame ulioikumba nchi yetu ikiwemo Wilaya ya Meatu wakulima walipanda mbegu ya pamba lakini hazikuweza kuota kutokana na ukosefu wa mvua, walipotaka kurudishia mbegu zingine walikosa kwa sababu hakukuwa na mbegu zilizokaribu kwa ajili ya kupanda mbegu nyingine. Hii ni kutokana na kiwanda cha kuzalisha mbegu kiko Mkoa wa Katavi, lakini pamoja na kuwa Serikali imeweka ruzuku kwa ajili ya pembejeo bado kuna gharama kubwa ya kusafirisha mbegu hizo kuzitoa Katavi mpaka kuzileta Simiyu. Ninaiomba Serikali ifanye inavyoweza ili wananchi wasiwe na changamoto ya ukosefu wa pembejeo ya mbegu kwa ajili ya viwanda tunavyovifufua pamoja na viwanda vya nyuzi na viwanda vya ushonaji nguo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa nyingine iko kwenye dawa za kuua vidudu. Mheshimiwa Rais akiwa Makamu wa Rais alipokuja Mkoa wa Simiyu alitoa maelekezo wataalam wetu wajikite kutengeneza dawa ambayo itauwa vidudu, lakini mpaka leo Mheshimiwa Samia akiwa Rais bado wakulima wa pamba wanaletewa dawa za kuua wadudu ambazo haziui wadudu, zinafifisha tu. Ukimwagia wadudu ndio wanashamiri, ukimwagia ndio matunda yanaanguka chini, lakini sasa ni afadhali ambao hawakumwagilia angalau wameweza kuvuna. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali yetu inapoongea kwamba, uzalishaji wa pamba unaenda kuongezeka mara dufu msimu huu, sikubaliani nao, kuweza kulichukua lile kijumlajumla, waangalie maeneo ambayo zao litaongezeka mara dufu, lakini waangalie maeneo ambayo yana changamoto ili waweze ku-deal na changamoto zilizojitokeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kushukuru pia pamoja na upungufu uliopo katika AMCOS zetu na kwamba, utaratibu wa ununuzi maeneo mengine unataka kubadilishwa, lakini AMCOS imefanya kazi kubwa. Mkulima miaka yote amekuwa akipunjwa kilo yake ya pamba, lakini toka AMCOS zianze wakulima hawalii kuhusu kupunjwa mizani kwenye zao la pamba. Hata kama watabadili utaratibu, lakini waendelee kulinda mkulima asiendelee kupunjwa katika mizani ya pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)