Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Christopher Olonyokie Ole-Sendeka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Simanjiro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kukushukuru wewe mwenyewe binafsi kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyoko mbele ya Bunge lako Tukufu. Pia nichukue nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuliongoza Taifa hili na hatua aliyokwisha lifikisha Taifa hili kwa mwaka mmoja ni hatua kubwa sana ambayo kila mtu ni lazima aiunge mkono.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee pia nataka nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha Daktari Mwigulu, kuanzia hotuba yake ya Mpango na hotuba yake pia ya Bajeti, Mheshimiwa Waziri ninakutakia kila lililo jema kwa sababu mipango bora ya sasa ndiyo itakayoamua kesho iliyo njema ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, naomba niende kwenye hoja ambayo ningetaka nigusie na maeneo ambayo nimeyachagua kuyazungumza. Nianze kwa kuyanukuu maneno ya Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika Kitabu chake cha Uhuru na Maendeleo, ukurasa wa Tisa naomba kunukuu kwa ruhusa yako. ‘‘…..kama tunataka maisha yetu yawe na amani na raha na kama tunataka kufanikiwa katika shabaha zetu na kuinua maisha yetu, basi lazima tuwe na uhuru pamoja na utii. Maana uhuru bila utii ni wazimu na utii bila uhuru ni utumwa’’. Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Spika, ninaomba tena nifanye nukuu ya pili ili niendelee na ninaifanya katika imani za mwanachama wa CCM, nataja imani ya kwanza na imani ya pili, inasema… ‘‘binadamu wote ni sawa na ya pili ninasema kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake’’. Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Spika, jamii ninayotokana nayo, jamii ya Wafugaji au jamii ya Wamasai katika kipindi hiki wanapita katika taharuki na huzuni kubwa kutokana na maamuzi ya Serikali yanayoendelea katika eneo la Ngorongoro, eneo la Loliondo na sasa tamko la Waziri wa Maliasili na Utalii juu ya nia yake ya kutangaza kupandisha hadhi baadhi ya mapori tengefu kuwa mapori ya akiba.

Mheshimiwa Spika, naomba ninukuuu maneno ya Waziri wa Maliasili na Utalii katika hotuba yake aliyoitoa Tarehe Tatu yanasema hivi …. ‘‘eneo la Idara ya Wanyamapori; Mheshimiwa Spika, Wizara inatarajia kupandisha hadhi mapori tengefu ya Lake Natron, Kilombero, Loliondo, Lolkisale, Longido, Muhuwesi, Umba River, Mto wa Mbu, Simanjiro, Ruvu Masai, Ruvu Same na Kalimawe, misitu ya Litumbandyosi na Gesimazoa kuwa mapori ya akiba. mwisho wa kunukuuu.

Mheshimiwa Spika, suala la mapori tengefu kupandishwa hadhi, kwa maana maeneo ambayo Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii ameyatamka katika Wilaya ya Simanjiro maana yake Simanjiro kwa ujumla wake sasa inatarajiwa kupandishwa hadhi kwenda kuwa pori la akiba, maana Simanjiro kwa asilimia 100 ni pori la akiba kwa mujibu wa Sheria ya Mwaka 1951 ya Fauna Conservation Ordinance Sura ya 302. Mapori yale yalipotangazwa Simanjiro yote na niseme the whole of Masai land wakati wa Masai District Council karibu yote ukiacha maeneo ya National Parks ni game controlled areas.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Fauna Conservation ilikuja kubadilishwa na Sheria ya Uhifadhi ya mwaka 1974, na Sheria ya 1974 ya uhifadhi ilifutwa na Sheria Na. 5 ya Mwaka 2009. Sheria zote Mbili nilizozitaja za mwanzo Fauna Conservation Ordinance na Sheria ya Uhifadhi ya mwaka 1974 hayakufanya maeneo ya Game Controlled Areas au maeneo ya mapori tengefu kuwa maeneo yanayokataza malisho makazi na vijiji kuanzishwa ndani ya maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, sheria mpya ya Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009 iliyafanya mapori tengefu kuwa na hadhi ambayo shughuli za binadamu haziruhusiwi isipokuwa kwa kibali cha Mkurugenzi wa Wanyamapori. Kwa maana hiyo Waziri alitakiwa kwa mujibu wa sheria hiyo na hasa Kifungu cha 16(1) ilimtaka Waziri kutamka na kutangaza katika gazeti la Serikali eneo lolote la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa pori tengefu, lakini sheria hiyohiyo Na. 16 Kifungu Kidogo cha (4) ilimpa Waziri huyo muda wa kuchukua zoezi hili la kuyapitia mapori hayo tengefu yote ambayo yako 49.

Mheshimiwa Spika, Kifungu hicho cha 16 cha Sheria ya Warrant Conservation Act, ikamkataza Waziri mwenye dhamana ya Maliasili na Utalii kuingiza eneo lolote la ardhi ya Kijiji katika eneo hilo la pori tengefu. Kwa maana hiyo ni kwamba hakuna ardhi ya kijiji ambayo kwa mujibu wa sheria itageuzwa kuingizwa katika ardhi ya pori tengefu, na kwa maana hiyo shughuli zinazoendelea katika Tarafa ya Loliondo na Sale ya kuchukuwa ardhi vijiji vya Kata Saba, Nane za Tarafa ya Loliondo na Sale na kuunda pori tengefu la Loliondo katika sura ya sheria niliyoitaja, ni zoezi batili na linastahili kukemewa na mtu yoyote anayeyatakia mema Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, ninasema hayo kwa kutaja vifungu hivyo vya sheria vinavyokataza kuchukua ardhi ya Kijiji na kuifanya kuingia katika pori tengefu, lakini wakati Loliondo yakiendelea na ya Ngorongoro yakiendelea Waziri mwenye dhamana kana kwamba haoni jeraha hilo kwa jamii ya wafugaji, anatangaza sasa kuifanya Simanjiro kwa ujumla wake kuwa pori la akiba ndiyo kusudio lake, kwa maana ya mapori tengefu aliyoyataja. Kwa lugha nyingine anatangaza Wilaya nzima ya Longido kwa kuchukuwa Natron game controlled area na Longido game controlled area, sasa Longido yote kwa asilimia 100 kwa nia ya Mheshimiwa Waziri Pindi Chana sasa itatarajiwa kuwa pori la akiba na sijui wananchi wale wanaenda wapi. Kana kwamba hiyo haitoshi eneo la Ngorongoro lililokuwa limebaki katika Tarafa ya Sale na Loliondo nalo linamegwa katika sura hii.

Mheshimiwa Spika, ukiondoa eneo la Km 8,300 za Tarafa ya Ngorongoro eneo linalobaki kwa wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro ni Km. za mraba sizizozidi 2007 kwa watu wapatao zaidi ya 180,000. Jambo hili kwa vigezo vyovyote vile haiwezi kukubalika, ushauri wangu kwa Serikali yangu Chama cha Mapinduzi, ni kukaa na wananchi katika eneo la Loliondo, na kuwashirikisha kama ambavyo barua ya Mheshimiwa Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Kayanza Peter Pinda ilivyoelekeza alivyokuwa amemuandikia Mkuu wa Mkoa wakati huo wa Mkoa wa Arusha kwamba wananchi washirikishwe kwa sababu sheria haziruhusu kulichukuwa eneo hili na kulifanya kuwa Pori Tengefu.

Mheshimiwa Spika, kugeuza ardhi za Wilaya hizo zote za Masai maana wamasai wana Wilaya hizo nne ndiyo ambalo ndiyo wako majority leo kuyageuza yote kuwa mapori ya akiba yanatwisha mzigo wa kujiuliza dhamira yake ni nini?

NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mary Masanja.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa ambae ametoka kuzungumza sasa kwamba hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii iligusia maeneo ambayo hayatahusisha maeneo ya vijiji vya wananchi, kwa hiyo maeneo yanayoenda kupandishwa hadhi, kutoka mapori tengefu kwenda mapori ya akiba ni maeneo potential tu kwa ajili ya uhifadhi na hayana wananchi ndani yake. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka unapokea taarifa hiyo?

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, naomba nikuhakikishie wala siIpokea maana wala haina hadhi ya taarifa, kwa sababu akisoma section 16 sub-section (5).

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, naam!

SPIKA: Kanuni unazifahamu vizuri, unapokea taarifa au unaikataa unaendelea na mchango wako.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, ninakataa siIpokei, kwa sababu ukweli unabaki hivi kwamba alichokitangaza Waziri ni kupandisha mapori ya akiba yaliyoanzishwa na Fauna Conservation Ordinance kuwa game reserve, wakati yeye mwenyewe anajua kabisa kwamba pori, game reserve inaanzishwa na Rais kwa mujibu wa Kifungu cha 14, anamuuzia Rais Mbuzi kwenye gunia kwa sababu yeye mwenyewe hana mapori tengefu hajayaanzisha, kwa mujibu wa Sheria hiyo Na. 16 (1). hujaanzisha kitu halafu unamwambia Rais aanzishe pori la akiba na unafanya hivyo katika Wilaya Nne kamili. Kwa kweli nia hiyo siyo ni njema na Wizara hiyo mnapaswa mjitafakari, muangalie na mpitie maamuzi yenu, lazima yajenge haiba nzuri kwa nchi yetu, yajenge haiba nzuri kwa raia waliotuchagua yajenge haiba nzuri ya nchi yetu katika uso wa dunia.

Mheshimiwa Spika, nataka nirudie kusema….

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka nakulindia muda wako Makatibu mtazame hapo.

Mheshimiwa Naibu Waziri, hii taarifa uliyoitoa kwamba maeneo yale yanayopandishwa hadhi hayana wananchi, Mbunge anasema hayo maeneo yana wananchi, sasa hebu fafanua vizuri hapo, kwa sababu upotoshaji upo kona gani kwenye hoja hii. Hayo maeneo yanayo wananchi au hayana wananchi ili kama hayana wananchi mchango wa Mheshimiwa Ole-Sendeka nitakuwa na mazungumzo nao huo mchango wake kama maeneo hayana wananchi.

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba nirudie tena ili muongeaji asikie vizuri. Haya maeneo ni maeneo ambayo yalikuwa ni mapori tengefu Game Controlled Areas. Maeneo haya yanapokuwa na hadhi nzuri na haya maeneo kwa asilimia kubwa yanawawekezaji tayari, hivi ninavyoongea kuna wawekezaji ndani yake, kuna wawindaji wa kitalii nakadhalika. Tunapoona yana sifa ya kuhifadhiwa ili wananchi wasiendelee kuwasongelea tumeyapandisha hadhi. Game controlled area inapanda kuwa game reserve, game reserve inapoongezeka kuwa sifa tunapeleka kwenye National Park. Sasa tumeona haya maeneo yana hadhi ya kupanda kutoka kwenye Game Controlled Areas kwenda kwenye game reserve na hayana wananchi.

Mheshimiwa Spika, naomba nirudie hili aelewe vizuri, amesema kwamba asilimia 100 ni maeneo ya wananchi, na hii kauli niwaombe Waheshimiwa Wabunge wanapotumia maeneo eti ardhi yetu, Tanzania ardhi ya Umma, siyo ya mtu mmoja. Tunawagawa wananchi tunaposema kwamba haya ni maeneo ya kwangu, haya ni maeneo ya nani!

Mheshimiwa Spika, tunapoona haya maeneo hayana watu tumeyahifadhi vizuri na yamekuwa na sifa nzuri, tunayapandisha hadhi. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni asilimia 100 haya maeneo hawamo wananchi ndani yake. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka nimekusikiliza kwa makini sana, ukizungumzia hizo sheria, ukivitaja na vifungu. Maelezo niliyomtaka atoe ya ziada Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, ambayo wananchi ndiyo maneno kama haya yanayozungumzwa, kwamba wananchi watahamishwa hayo maeneo yote wanayoishi huko ndiyo yanayoleta taharuki! Kwa mchango wako Mheshimiwa Ole-Sendeka unaashiria kwamba wananchi wote wa Simanjiro asilimia 100 watatakiwa kutoka huko kwa agizo la Mheshimiwa Waziri. Hebu fafanua hapo ili mimi nijue upotoshaji upo sehemu gani.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, mapori tengefu hayo ambayo Waziri anayazungumza kwanza ili uyajue ni mapori tengefu ambayo yalishafutwa na Sheria Na. 5 ya mwaka 2009 na yakamwelekeza Waziri hivi….

SPIKA: Kwa kuwa sheria unayo hapo nisomee Mheshimiwa.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, naomba nikusomee.

SPIKA: Nisomee.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, for the purposes, nakusomea section 16 subsection (5). …. ‘‘for purposes of subsection (4), the Minister shall ensure that no land falling under the village land is included in the game controlled areas. Lakini….

SPIKA: Nisomee subsection four.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, ngoja nirudi sasa exactly, ngoja nikuanzishie na hiyo subsection (4), safi sana nakushukuru sana. Ninaanza na one ili tuenda four.

SPIKA: Soma four, tutaenda kwa mtiririko huo mpaka tutafika sehemu nzuri wala usiwe na wasiwasi soma subsection four.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, subsection four, The Minister shall, within twelve months after coming into operation of this Act and after consultation with the relevant authorities, review the list of game-controlled areas for the purposes of ascertaining potentiality justifying continuation of control of any of such area.

Mheshimiwa Spika, sasa subsection (1)...

SPIKA: Sawa ngoja umeshanisomea hiyo 16 ngapi ngapi na nimekusikiliza, sasa hebu nisomee kwenye hiyo hiyo sheria kifungu kilichofuta, kwa sababu umesema hiyo sheria imefuta hayo maeneo, hebu nisomee hicho kifungu kilichofuta, nakupa muda nisomee kifungu kilichofuta.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, kifungu cha 16 nilichokusomea kwamba Waziri atayapitia mapori hayo tengefu na ku…

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka kupitia ni sawasawa na kufuta?

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, ndio nilikuwa nataka nikusomee, twende moja turudi nne, twende tano ili wewe Mwanasheria utusaidie.

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka sheria huwa inasomwa namna ulivyoanza, wakakuambia subject to subsection (4). Kwa hiyo, kabla hujamaliza kile unakwenda kwenye kifungu kidogo cha (4) ambayo umeshanisomea. Sasa katika kifungu kidogo cha (1) mpaka (4) kuna mahali wanasema wamefuta, kwa sababu ile kifungu kidogo cha (1) uliyonisomea na (4) uliyonisomea, hakuna mahali niliposikia yamefutwa. (Makofi)

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, sitaki kubishana na wewe katika angle ya sheria.

SPIKA: Kwenye hoja hii mimi ndiyo niliyekupa ruhusa kwa sababu nazungumza nawe..

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, ndiyo.

SPIKA: Ili nielewe upotoshaji upo wapi?

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, kweli ni hivi kabla sheria hii ili utusaidie wote, maeneo ya Game Controlled Area ilikuwa ni ardhi ambayo ni ardhi za vijiji kwa wakati huo. Kwa hiyo...

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka sheria unayo wewe mwenyewe, nimekwambia usome wewe mwenyewe na mimi nakusikiliza, sasa nakupa nafasi hebu soma hicho kifungu kidogo cha (1) mpaka (4) labda nitasikia mahali uliposema pamefutwa hebu soma.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE–SENDEKA: Mheshimiwa Spika, naomba kwenye section 16 (1); subject to section 4(2) of the Land Act, the Minister may, after consultation of the relevant local authorities, and by order in the Gazette, declare any area of land in Tanzania to be a Game Controlled Area.

Baada ya mamlaka hayo ya kutamka na kutangaza…

SPIKA: Nisomee umalize ili tuwe tunasikilizana, soma moja mpaka nne kama ulivyosema na mimi nakusikiliza kwa makini sana. Soma sheria yako uliyonayo, usiongezee maneno kwa sababu nitahisi pengine umeanza kutafsiri. Wewe nisomee ili mimi na wewe twende ngazi kwa ngazi.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE – SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nilishakusomea kifungu kinachoanzisha Game Controlled Area na ambacho ni kifungu cha 16(1), nimeshakusomea kifungu hicho cha …

SPIKA: Umesema nikupe nafasi unisomee kifungu cha 16(1) mpaka (4) ndio nitaelewa, si ndio umesema hivyo?

MHE. CHRISTOPHER O. OLE–SENDEKA: Mheshimiwa Spika, sawa kwa hiyo nirudie.

SPIKA: Nisomee pengine nitasikia neno la kufuta ili nimshike sasa Naibu Waziri kwamba yeye ndio anayezusha.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE–SENDEKA: Mheshimiwa Spika, naomba nirejee kwenye wapi ambapo nimenukuu kwamba sheria moja inapoanzishwa inafuta nyingine, naomba nimnukuu barua iliyoandikwa na Waziri Mkuu Mizengo Kayanza Peter Pinda.

SPIKA: Naomba unisomee Sheria kifungu cha 16(1) mpaka (4).

MHE. CHRISTOPHER O. OLE–SENDEKA: Mheshimiwa Spika, sawa niende kwenye (4), niende kifungu 16(4).

SPIKA: Kifungu kidogo cha (2) umeshasoma tayari?

MHE. CHRISTOPHER O. OLE–SENDEKA: Mheshimiwa Spika, no hapa...

SPIKA: Nisome (1) mpaka (4), mimi ninakurahisishia ili nikuelewe, nakulinda na Naibu Waziri naye namlinda.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE–SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nilinukuu kwenye sheria na nikawa nakusomea kwa hiyo (2) haikuwa na uhusiano na hoja yangu, kwa hiyo ambazo nimezitaja ndizo zilikuwa na uhusiano na hoja yangu.

SPIKA: Kama hivyo ndivyo, maelekezo yako marefu niliyoyasikiliza, kifungu cha 16(1) na 16(4) ulivyonisomea, hakuna mahali panaeleza kwamba hayo mapori tengefu yaliwahi kufutwa. Hakuna na kwa maelezo aliyoyatoa ya ziada Mheshimiwa Naibu Waziri hakuna mahali ambapo maelekezo ya Waziri mwenye sekta yanasema watu wa Simanjiro na pori tengefu wanaondoka, hakuna. (Makofi)

Sasa haya maneneo ya kwamba maeneo yote ambayo wanakaa Wamasai katika Wilaya nne zote wanaondoka, yametoka wapi?

MHE. CHRISTOPHER O. OLE–SENDEKA: Mheshimiwa Spika, hapo ndiyo mahali ningeomba wote wanisikilize. Kabla ya sheria hii tunayozungumza namba tano, maeneo yaliyokuwa yanaitwa mapori tengefu ni maeneo ambayo shughuli za binadamu zilikuwa zinaruhusiwa na zilikuwa zinahifadhiwa kwa mujibu wa sheria hizo mbili nilizozitaja ya mwaka 1974 na ile ya mwaka 1951. Ilipokuja sheria hii ndiyo ikapandisha pori tengefu kupewa hadhi sasa ya kuwa ya miongoni mwa reserved lands ambazo shughuli za binadamu haziruhusiwi. Ili hilo liwezekane ilikuwa lazima mapori hayo yapitiwe kama ilivyosema section (4) halafu mwishoni yatangazwe na Waziri mwenye dhamana baada ya kufanya consultation na local authorities.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo...

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka unanipa wakati mgumu sana, kwa nini unajua? Sheria uliyosoma hapo imetumia neno may, mimi nikakusikiliza kwa sababu wewe unajua sheria, mimi pia ni Mwanasheria. Umesoma mwenyewe hapo, hakuna mahali palipofuta, hilo ni la kwanza, maana ulianza kwa kusema kwamba sheria ilifuta hujasema ni wapi sheria ilifuata, moja.

La pili, umesema maeneo yote wanayokaa Wamasai maeneo ambayo ni mapori tengefu, Wamasai wanaondoka kwa sababu maeneo hayo yamepandishwa hadhi. Mheshimiwa Naibu Waziri pale ametoa ufafanuzi kwamba si kweli maeneo yanayopandishwa hadhi wananchi huko hawapo. Kwa hiyo hapo wewe ukiambiwa kwamba unazikosea kanuni zetu, ukiambiwa wewe Mheshimiwa Ole-Sendeka unazikosea kanuni zetu, kwa nini? Kwa sababu umesema jambo ambalo halipo, kwa sababu la sivyo wote ninyi, jamani mimi ndiyo shughuli yangu hapa ya kusimamia kanuni.

Mheshimiwa Ole-Sendeka tukiendelea kwa mtindo huo, nitataka uniletee ushahidi na Mheshimiwa Waziri ataleta na yeye wa kwake, halafu mimi nitafanya maamuzi kama unashikilia huo msimamo wako. Nilitaka nikurahisishie ili kama huna uhakika na hicho unachokisema tuliachie hapo, kama unao uhakika nitataka wewe uniletee ushahidi na Waziri aniletee ushahidi na si ushahidi ule ambao umeusema hapa Mheshimiwa, kwa nini? Kwa sababu hapa nimekuongoza vizuri, hiyo sheria inachosema, nitakapokutaka ulete ushahidi siyo ushahidi wa hivyo vifungu vya sheria kwa sababu hivyo vinakukaba wewe mwenyewe.

Mheshimiwa Ole-Sendeka nakupa hiyo nafasi.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE–SENDEKA: Mheshimiwa Spika, kwa sababu hapa nazungumza habari ya tafsiri ya sheria na mimi siyo bingwa kwenye eneo hilo, naomba niondoe hoja hiyo katika sura hii. (Makofi)

SPIKA: Sasa Katibu alikuwa amekutunzia muda wako kama nilivyoahidi, kwa hiyo sasa endelea na mchango wako. (Makofi)

MHE. CHRISTOPHER O. OLE–SENDEKA: Mheshimiwa Spika, katika barua ya Waziri Mkuu naomba nifanye nukuu, Mheshimiwa Mizengo Kayanza Pinda alisema hivi, nanukuu: “Mwaka 1974, Sheria ya Hifadhi ya Wanyamapori ilianzishwa na kufutwa Sheria ya awali ya Fauna Conservation, Sura ya 302. Chini ya sheria hizo mbili masuala ya malisho na makazi hayakukatazwa katika maeneo ya pori tengefu ikiwa ni pamoja na Pori Tengefu la Loliondo. Sheria hiyo ya Hifadhi ya Wanyamapori iliendelea kutumika hadi mwaka 2009 ambapo sheria mpya ya Uhifadhi wa Wanyamapori ya The Wildlife Conservation ya mwaka 2009 ilianzishwa na kufuta ile ya awali ya mwaka 1974.” Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Spika, hiyo ni barua ya Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda alipomuandikia Mkuu wa Mkoa baada ya kuchambua hali ya mgogoro wa Loliondo na haya ndiyo maneno ambayo nimeyanukuu.

Mheshimiwa Spika, lakini mwisho, baada ya Waziri Mkuu kupokea maoni ya wananchi wa Loliondo alikuja na uamuzi huu. Kwanza amebainisha kwamba maoni ya wananchi kwa ujumla yanataka eneo hilo kumilikiwa na wananchi ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakitumia kuhifadhi kwa taratibu zao za kimila na desturi za jadi, lakini mwisho kabisa Waziri Mkuu alitambua hali iliyokuwepo ya wananchi kutokushirikishwa awali katika uamuzi huo.

Mheshimiwa Spika, ninalotaka kuishauri Serikali kwa sasa ni kwamba ikitaka kwenda kuanzisha mapori tengefu kwa sababu ni matakwa ya sheria kushirikisha wananchi, hakuna mwananchi wa Simanjiro aliyeshirikishwa kuanzishwa kwa pori tengefu, kinachotakiwa sasa ni waje watushirikishe ili wapate pori tengefu ambalo watamshawishi Mheshimiwa Rais kwa mujibu wa kifungu cha 14 alipandishe hadhi kuwa pori la akiba. Hiyo ndiyo hoja yetu ya msingi ambayo tunazungumza na hicho ndiyo kilio cha wafugaji katika maeneo hayo niliyoyataja ambayo yameathiriwa na mapori tengefu hayo niliyoyataja.

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee na hoja nyingine moja ya uagizaji wa mafuta kwa njia ya bulk procurement. Ni jambo la busara sana kama tunataka kupunguza gharama za mafuta na kuondoa mzigo kwa wananchi, tuyaachie makampuni yote yenye nia ya kuleta mafuta nchini, kazi yetu iwe kuangalia usafi na ubora wa mafuta pale yanapoingizwa badala ya kuwa na makampuni sita au nane. Hii itasaidia kuhakikisha kwamba tunapunguza ugumu wa maisha na jambo hili halina sababu kuendelea kufichwa, tuendee tuweke uwazi kwa kuwakaribisha watu wote wenye uwezo wa kuleta mafuta.

Mheshimiwa Spika, nimwombe pia Waziri mwenye dhamana ya Nishati ya kupitia suala la vinasaba katika mafuta ambapo Wizara ilikuwa imeipatia kampuni moja uwezo wa kutosha shilingi saba kwa kila lita ya mafuta na iliingizwa kwenye pricing template ya mafuta na kampuni hiyo siyo kampuni nyingine ni kampuni ambayo imefanya kazi kwa zaidi ya miaka 10 ya GFI ikishirikiana SICPA SA ambayo ilikuwa ime-tender bei mara mbili zaidi ya washindani wenzake ambao walikuwa wameomba katika zabuni hiyo. Nakusudia baadaye kuleta hoja katika Bunge lijalo ili mambo haya yaweze kuwa wazi na kuweza kunusuru katika nchi yetu katika mzigo huu mkubwa.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, maana naona umeshika microphone.