Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na Naibu wake Mheshimiwa Hamad Hassan Chande na wataalamu wa Wizara pamoja na wadau kwa kazi nzuri wanayofanya katika sekta ya fedha na uchumi.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inalo jukumu kubwa la kuwapatia wananchi huduma bora za umma. Ili Serikali iweze kutimiza wajibu wake kwa umma, inahitaji kuwa na rasilimali fedha ya kutosha inayotokana kwa kiasi kikubwa na makusanyo ya kodi kutoka vyanzo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, jukumu hili limeainishwa vizuri sana katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020/2025. Kama Serikali itashindwa kukusanya mapato ya kutosha kupitia mamlaka husika, uwezo wake wa kutoa huduma bora kwa Watanzania utakuwa kidogo.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu inakabiliwa na tatizo la kupoteza sehemu ya mapato yanayotokana na kodi kutokana na sababu mbalimbali. Upotevu wa mapato ya Serikali husababishwa na yafuatayo: -

Moja, asilimia kubwa ya wafanyabiashara wadogo (SME's na Wamachinga) hawajadhibitiwa na kuwekwa rasmi kwenye mifumo wa kulipa kodi. Idadi yao ni kubwa lakini mchango wao kwenye kulipa kodi ni mdogo sana.

Pili, ukwepaji wa kodi; katika hili imejidhihirisha kwamba watu wachache sana, hasa hasa walio kwenye ajira na sekta rasmi ndio wanaolipa kodi, hivyo kubeba mzigo wa wale wasiolipa kodi, ambao bado wanafaidi bidhaa na huduma za umma sawasawa na wale wanaolipa kodi. Walipakodi waliosajiliwa kukusanya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ni walipakodi wachache na hawa ndio wanaotumia mashine za EFD.

Tatu, kwa kiasi kikubwa, wafanyakazi wa Halmashauri nyingi nchini wenye majukumu ya kukusanya kodi pamoja na sehemu kubwa ya wafanyabiashara walio rasmi na wasio rasmi hawana mashine za kukusanyia kodi. Hii imesababisha Serikali kupoteza kiasi kikubwa cha mapato.

Nne, upotevu kwenye misamaha ya kodi; baadhi ya misamaha ya kodi iliyotolewa na Serikali kwa nia nzuri imekuwa ikitumika visivyo kuwanufaisha watu au makampuni yasiyostahili. Hali hii imekuwa ikisababisha upotevu wa fedha za Serikali.

Tano, utoroshwaji wa mali na fedha nje ya nchi; viwango vipya vya upotevu wa mapato yatokanayo na utoroshwaji wa fedha nchini kwenda nje ya nchi ni dola za Kimarekani milioni 464 kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu, natoa mapendekezo yafuatayo kwa Serikali; kwanza naishauri Serikali iwe na mkakati wa kuwaendeleza wafanyabiashara wadogo na wale wasio rasmi, iwasajili kwenye maeneo yao na kuweka mifumo rasmi ya kuwalipisha kodi kutokana na shughuli wanazofanya. Kufanikisha hili, Serikali inashauriwa kuajiri watumishi wa kutosha ili wasaidie kufanikisha azma hii.

Pili, naishauri Serikali ipunguze misamaha ya kodi na hii itolewe kwa wanaostahili baada ya kufanya tathmini ya kutosha kubainisha wahitaji sahihi; tatu, naishauri Serikali iboreshe uwazi katika utoaji wa misamaha ya kodi; nne, naishauri Serikali iendelee kuelimisha wananchi na kuwajibisha wale wote wanaohusika na ubadhirifu au wanaokiuka sheria zinazosimamia fedha za umma.

Tano, naishauri Serikali isambaze kwa wafanyabiashara wote mashine za kukusanya kodi (EFD), na izidi kuwekeza katika mifumo ya kielektronki ya ukusanyaji kodi, hata katika ngazi ya Halmashauri na wafanyabiashara wadogo wadogo; sita, naishauri Serikali itekeleze kwa makini suala la mapitio ya sheria mbalimbali ili makampuni yote yalipe kodi stahiki; na saba, naishauri Serikali itoe elimu kwa wananchi wote ili watambue kuwa ni wajibu wao kulipa kodi kwa ajili ya kuchangia maendeleo ya nchi yao.

Mheshimiwa Spika, kwa kufanya haya, mapato mengi yataweza kukusanywa na hivyo kuwa katika nafasi nzuri ya kupata huduma muhimu na kwa ubora zaidi.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.