Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. NICODEMUS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante nashukuru kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia Wizara hii ya Fedha.

Mheshsimiwa Spika, jambo la kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii adimu kuweza kuchangia Wizara ya Fedha ambayo inadai shilingi trilioni 14.94. Nimejaribu kuangalia mchanganuo pamoja na Mheshimiwa Waziri kweli mimi sina mashaka kulingana na mchanganuo jinsi nilivyouona hapa kwenye hotuba ya Waziri.

Mheshimiwa Spika, lakini napenda muda wangu huu kuishauri Serikali kama zilivyo kanuni, taratibu na sheria zetu kwamba Mbunge ni mtunga sheria, halafu ni mshauri wa Serikali. Walipakodi nchi hii wanaolipa ni wachache sana, nakuomba Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri kwanza kwenye Wilaya yangu mnisaidie nipate Ofisi ya Mamlaka ya TRA ili wafanyabishara waweze kupata huduma karibu. (Makofi)

Mhehsimiwa Spika, ukiangalia Mkoa wa Geita sehemu nyingi hazina Ofisi za TRA, pale Mbogwe Ofisi ilishakamilika lakini bado haijafunguliwa. Kwa hiyo nikuombe Waziri ulichukue hili na uweze kunijibu kule mwishoni utakapotoa ufafanuzi wako kwamba sasa Mbogwe inaenda kufunguliwa Ofisi ya TRA ili kusudi wanaeonda zaidi ya kilometa 40 kwenda Bukombe kwenda kulipa kodi waweze kulipia karibu.

Mheshimiwa Spika, ninamshukuru Mheshimiwa Rais, mwaka jana nilisimama hapa, Naibu Waziri wa Fedha alikuwa Mheshimiwa Masauni nilikuwa nawalilia sana wafanyabiashara jinsi walivyokuwa wanapambana na TRA, lakini kwa sasa hivi bila unafiki kwa kweli kumekuwa na mazungumzo na makubaliano mazuri kwenye upande wa TRA.

Kwa hiyo nimpongeze Mkurugenzi wa TRA pamoja na Makatibu Wakuu wa TRA, najua mmeajiri vijana wengi katika sekta hii, niiombe Wizara hii sasa ijitahidi kuwapa mafunzo ili kusudi watakapoenda kwa wateja wetu, wananchi wetu, wafanyabiashara wetu wawe na kauli nzuri ili kuweza kuwafanya watu walipe kwa hiyari kama Rais anavyotaka maana nia ya Rais ni kumuona kila Mtanzania anafurahi, analipa kodi bila kusumbuliwa, watu wasivamiwe kama zamani walivyokuwa wakinyang’anywa na kufungiwa akaunti zao na kwa kweli mimi nikiri wazi tu nimetembea Taifa jirani hapa, kodi wakati ikifika mtu anaenda kabisa kulipa mwenyewe bila hata kufuatwa. Na neno la kodi hili ukiangalia hata kwenye maandiko matakatifu ni itu ambacho kipo halali. Kwa maana hiyo hapo hakuna maswali sana.

Kwa hiyo, tuombe tu hawa mliowaajiri muwape mafunzo ili wasije na munkari na morali za kutoka huko chuoni wakaanza tena kusumbua wananchi wetu na kutochonganisha tena nikawa mchango wangu huu leo nimeomba Ofisi ya TRA halafu wananchi wakaanza kukamatwa na kusumbuliwa, hapo nitakurudia Mheshimiwa Waziri kwa vile wapo chini yako. (Makofi)

Lakini ajenda ya pili nilete malalamiko ya wafanyabiashara hapa nchini, haya mabenki ya ndani yanawakanyaga sana wafanyabiashara wa ndani hapa. Tukiangalia tumetoka kwenye hili suala la corona, mfano kuna watu waliagiza mizigo yao China, kuna watu waliagiza mizigo yao mataifa mbalimbali, lakini wafanyabiashara hao wamekopa katika haya mabenki. Mabenki yameshinda kuwasikiliza, kuwapunguzia riba na kipindi naingia hapa Bungeni hotuba ya Rais wa Awamu ya Tano alitoa maelekezo kabisa kwamba riba zipungue kwenye mabenki. Lakini pia hata Mama Samia Suluhu Hassan wakati analihutubia Bunge hapa suala la riba aliliongelea hapa Bungeni kwamba riba zipungue. Waziri hizi taasisi zipo chini yako, unafeli wapi? (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, Waziri ana mamlaka ya kuweza hata kufuta leseni ya hizi benki, maana kweli wanasiasa wengi sasa hivi wanasimama wanasema nchi imefunguliwa, lakini kufunguliwa kwa nchi inaweza ikawa maumivu kwetu sasa. Kama sisi tunapigwa riba za juu wa ndani, halafu mgeni akija anapoozewa riba, inafunguliwaje hapo nchi? Si sisi sasa tumefungwa, wamefunguliwa wa nje! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimuombe Waziri hili lichukulie serious sana, wafanyabiashara wa ndani wanaumia sana, halafu mbaya zaidi hizi taasisi za kifedha hazina kauli kwa wafanyabiashara wa ndani vizuri. Haziwavumilii kwa mfano mtu amerejesha marejesho tisa, bado marejesho matatu tu unaenda kukamata nyumba yake, unaenda kumfilisi, ina maana ulimpa mkopo huo umsaidie au kumfilisi hiyo nyumba aliyonayo?

Mheshimiwa Waziri kwa vile leo nimepata nafasi hii, nakushauri sana Rafiki yangu na nanakupenda sana na mtu anayekupenda ni lazima akueleze ukweli bila kukupongeza pongeza maana yake mtu anaweza akawa anakupa pongezi kumbe anategemea umpe chochote. Mimi ninakushauri kwa vile ni jamaa yangu najua ndoto zako bado Taifa tunakutegea sana. Kwa hiyo, livalie njuga hili na haya ya mabenki ya ndani yaweze kupunguza riba. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, namshukuru Waziri wa Kilimo alielekeza mabenki yatoe asilimia tisa tu kwenye kilimo, naona kama kwenyewe kunawezekana. Sasa huku kwingine kunashindikana vipi? Rais wa Kwanza alishasema na wa Awamu ya Sita alishasema riba zipungue, hazipungui. Futa leseni, zitasajiliwa benki nyingine tutakuja kufanya nazo hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nataka nizungumzie hapa hali halisi ya maisha ya Watanzania wale wa kawaida. Kweli tunasema kwamba hali sasa hivi ina unafuu lakini bado hali ni ngumu. Sasa wewe kwa vile ni Waziri wa Fedha, angalia kama kuna sehemu yoyote fungulia fedha ili kusudi zifunguke hata kwa wanyonge zijae mifukoni, maana kwenye kampeni huwa tunasema tunawapigania wanyonge, sasa wanyonge hawajapata fedha bado, ninaangalia tunaenda mwishoni mwishoni bado kuna Bajeti Kuu, na kwenyewe niombe viongozi mnipe nafasi niweze kuruka vizuri na kuweka mchango wangu vizuri maana ninayo mambo mengi, maana sikupata nafasi ya kuchangia Wizara nyingi sana, lakini zipo Wizara ninahitaji nipate nafasi ya kuweza kuwasemea wananchi wangu wa Jimbo la Mbogwe.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo sasa nikuombe Waziri wa Fedha kwa kuwa leo tupo Wizara hii ya Fedha kama kuna uwezekano wowote ule kufungulia mahali popote pale, fedha zifunguke ili kusudi hata na wananchi wangionge nao waende wakanufaike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunashukuru kwa jitihada mnazozifanya, tumeona kwa watumishi mmeongeza mishahara, watumishi kwa kweli wanafurahi, walimu sasa hivi kila mwalimu anachekelea, watumishi mbalimbali wanafurahia kwa ongezeko hilo la asilimia 23.3 lakini wapo wengine ambao hawana nafasi ya kuweza kuingia kwenye manufaa haya. Kwa hiyo, ni vyema Waziri kwa vile ni msomi mzuri ujaribu kufikiria jinsi gani unaenda kulisaidia Taifa ili kila mtu apate haki yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho niseme...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga.

MHE. NICODEMUS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, yes naomba kumalizia, mimi nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii, maana nafasi ni ngumu sana kuzipata humu ndani, ahsante sana. (Makofi/Kicheko)