Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kushukuru kwa kunipatia nafasi hii na mimi niweze kutoa mchango wangu, lakini nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali niweze kusimama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwani siku ya jana sisi wananchi wa Jimbo la Meatu na wananchi wa Wilaya ya Meatu kwa ujumla, ilikuwa ni faraja kubwa kwetu sana kutokana na ule utiaji saini wa miradi 28 ya maji. Lakini Mheshimiwa Waziri aliendelea kusisitiza kwamba mradi ule wa kukabiliana na athari ya mabadiliko ya tabianchi ya kutoa maji Ziwa Victoria utatekelezwa mpaka Wilaya ya Meatu, Jimbo la Meatu. Kutekelezwa kwa mradi huu kutaokoa fedha nyingi inayotumika kufanya utafiti na maji yasipatikane. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nijielekeze katika hoja iliyopo mbele yetu na niishukuru Wizara ya Fedha na niunge mkono hoja. Nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa mwaka huu katika kutekeleza majukumu ya Wizara ya Fedha kazi kubwa sana mmeifanya. Kazi kubwa mmeifanya ya kupeleka fedha katika Halmashauri zetu, nadhani mwaka huu mmeweka historia katika upelekaji wa fedha za miradi ya maendeleo. Tumezoea kuona miradi ya maendeleo ikipelekewa fedha kwa asilimia 36 mpaka 40 kwa mwaka mzima, lakini kwa mwaka huu hadi mwezi Aprili, 2022 miradi mingi imepelekewa fedha kwa asilimia 80 na kuendelea. Mimi nishukuru sana na niipongeze sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, fedha hizi zilizopelekwa nyingi tunategemea Serikali ya Chama cha Mapinduzi itatekeleza miradi hii ili kuwe na manufaa yaliyokusudiwa kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu leo utajikita katika Idara ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali hususani katika katika level ya Halmashauri. Fedha nyingi zinapelekwa, lakini sasa ni wakati muafaka Mkaguzi wa Ndani akawezeshwa kwa ufasaha ili aweze kutekeleza majukumu yake kikamilifu. Kwa mfano, Halmashauri ya Meatu yenye Majimbo mawili mpaka sasa hivi imepelekewa shilingi bilioni tisa za kutekeleza miradi ya maendeleo upande wa Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiongelea katika Jimbo la Meatu nasema shilingi 10,500,000,000 kwa sababu fedha zingine tunazipata katika Wakala wa Barabara na Wakala wa Maji. Lakini ukiangalia sasa Mkaguzi wa Ndani kuna upungufu mkubwa wa wakaguzi wa ndani katika Halmashauri yetu ukilinganisha na fedha nyingi sana zinazopelekwa katika miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mimi nishauri kuanzia sasa ipo haja Wakaguzi wa Ndani wakaanza kutekeleza majukumu yao kuanzia fedha zinavyopelekwa, wasisubiri miradi ipelekwe ndio waone changamoto ziweze kuibuliwa. Changamoto nyingi zinajitokeza katika utekelezaji wa miradi ambazo zingeweza kuzuiliwa na Mkaguzi wa Ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunao uhaba mkubwa wa watumishi tunaomba waongezwe, kuna changamoto ya vitendea kazi ikiwemo mafuta hata magari. Magari yao yamepelekwa miaka mingi sana na yalikuwa yakitumiwa na utawala. Mimi niombe Serikali iangalie, ipeleke magari kutokana na utekelezaji ulivyo wa kasi wa miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, kuna changamoto ya fedha, fedha nyingi wanategemea wapewe na Mkurugenzi ambaye wanakwenda kumkagua. Hapo zamani walikuwa zilizokuwa zinapelekwa katika Fungu la General Purpose, lakini ile General Purpose Halmashauri zingine kwa sasa hivi hazipelekewi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mkaguzi wa Ndani kuendelea kuwaomba Wakuu wa Idara/Mkurugenzi ambaye anakwenda kumkagua kwa hiyo anaweza apate sio kwa wakati ambao unatakiwa.

Mheshimiwa Spika, lakini mimi niombe Wakaguzi wapelekewe miongozo ya matumizi ya fedha inayopelekwa ili waweze kunusuru miradi ambayo inakwenda kutekelezwa kinyume na ilivyopangiwa. Nitolee mfano, Jimbo la Meatu lilipelekewa fedha za kutekeleza/kukamilisha maboma, lakini user department ambaye ni Mkuu wa Idara ya Afya alibadili matumizi. Tunayo maboma kumi ya zahanati, lakini alikwenda kuanzisha boma jipya, akaacha kukamilisha yale yaliyokuwepo ambayo ndio ilikuwa base ya kuombea zile fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, shilingi milioni 35 zilikwenda kuanzisha na mpaka nilipokuwa mimi natembelea lilikuwa usawa wa kifua changu. Lakini mwaka huu wamepelekewa fedha nyingine za kukamilisha maboma mwezi Machi, Mkurugenzi alikuwa kwenye bajeti, yeye kwa kushirikiana na Afisa Mipango wamebadilisha fedha zile, badala ya kwenda kukamilisha maboma yale kumi wamekwenda kufanya miradi mingine wanayojua wenyewe. Lakini tukimuwezesha Internal Auditor ataweza kulizuia hili ndani ya CMT kabla halijapelekwa katika Kamati ya Fedha na Mipango. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niunge mkono hoja ya Kamati kwamba kuna haja ya kufanya mabadiliko ya Sheria ya Ukaguzi wa Umma ili kuleta tija kwenye Kkitengo cha Ukaguzi wa Ndani. Tunaona Kamati za Ukaguzi zinashindwa kufanya vikao vyao kutokana na ukosefu wa fedha, lakini muundo wake kama ulivyoelezwa bado hauleti tija katika kusimamia fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu wanaweza wakaa akidi ikawaruhusu kufanya wakiwa watumishi wa Halmashauri, lakini mimi niliwahi kuhudumu Halmashauri moja Mwenyekiti wa Kamati ya Ukaguzi alikuwa Afisa Maendeleo ya Jamii. Hili liangaliwe, Wenyeviti wawe na weledi, wawe na uelewa wa uhasibu ili kuweza kuleta tija katika usimamizi wa majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya majadiliano taarifa hii inawasilishwa kwa Afisa Masuuli wa Wilaya au wa Serikali ambaye ndiye mhusika aliyekaguliwa, kwa hiyo, yeye ni hiari yake aifanyie kazi ile taarifa au asiifanyie. Na hoja nyingi zimekuwa zikibaki mpaka zinakutwa na mkaguzi wa nje. Mimi niiombe Serikali ichukue maoni ya Kamati ya Bajeti ili sasa Mkaguzi wa Ndani awajibike moja kwa moja kwa Mkaguzi Mkuu wa Serikali. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa Komanya.

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, lakini niombe taarifa ya internal auditor iwe ajenda ya kudumu katika Kamati ya Ushauri ya Mkoa ili hoja ziwe zinafanyiwa kazi. Nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)