Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Bajeti ya Wizara ya Fedha na Mipango. Awali ya yote naomba nichukue nafasi hii niishukuru Serikali kwa jinsi ilivyosimamia na kutekeleza bajeti nzima ya Serikali kwa kipindi kinachoishia tarehe 30 Juni, 2022. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitachangia katika maeneo machache, lakini mchango wangu sehemu kubwa nitatoa ushauri upande wa Serikali. Nikianza na upande wa TRA, nilikuwa napenda kutoa ushauri TRA waweze kufungua Ofisi za Forodha katika mipaka yetu mbalimbali ili kuhakikisha kwamba tunadhibiti na kusimamia mapato ya Serikali. Pamoja na hilo katika mipaka hiyo hiyo nilikuwa nashauri TRA kufunga scanner katika maeneo ya mipaka kwa ajili ya kuimarisha na kusimamia uhakiki wa mizigo inayoingia na kutoka nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upande wa pili nataka nichangie kwenye Ofisi ya Msajili wa Hazina; Msajili wa Hazina ni msimamizi mkuu wa mali nyingi za Serikali pamoja na mashirika mbalimbali ambayo yako chini ya Serikali. Kwa upande wa Ofisi ya Msajili wa Hazina nilikuwa nataka nishauri kwenye yale mashirika yaliyofilisiwa viwanda pamoja na taasisi mbalimbali, maeneo mengi utakuwa mashirika hayo na viwanda hivyo vimekuwa grounded yaani havifanyi kazi na mali ziko katika maeneo hayo lakini ziko katika hali mbaya.

Kwa hiyo, nilikuwa nashauri sasa ni wakati muafaka katika kuimarisha uchumi wetu tuhakikishe kwamba mashirika hayo yanasimamiwa na yanaanza kufanya kazi, nikitoa mfano wa mashamba ya maua Arusha na viwanda mbalimbali ambavyo viko chini ya Msajili wa Hazina, nilikuwa nashauri viwe activated na vifanye kazi ili viweze kutuingizia mapato mbalimbali katika kuchangia kwenye pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika upande huu wa Ofisi ya Msajili wa Hazina yeye ndiyo msimamizi mkuu wa madeni yote yale ambayo yalikuwa kwenye maeneo yaliyofilisiwa. Nataka nitoa mfano, mwaka 1997 kuna Vyama vingi vya Ushirika vilifilisiwa, lakini vyama hivyo vilikuwa vimekopa kwenye benki ya NBC na vyama hivi vilibaki vilikuwa na madeni makubwa na madeni hayo baadaye yalikwenda kwenye shirika moja la Consolidated Holding Cooperation. Sasa madeni hayo sasa hivi yanasimamiwa na Msajili wa Hazina.

Mheshimiwa Spika, natolea mfano kuna chama kimoja kule Mbinga kilikuwa kinaitwa Mbifaco Limited lakini baadaye kuna chama kingine kimeanzishwa ambacho kinaendeleza shughuli zile ambazo zilikuwa zinafanywa na Mbifaco Limited kinaitwa Mbinga Farmers’ Cooperative Union. Kwa hiyo madeni yale bado yanashikiliwa na Serikali kupitia Msajili wa Hazina, lakini wakati huo vyama hivi inabidi viendelee na mali zile ambazo hati zake ziko upande wa Serikali ni mali za wakulima. Kwa hiyo, nilikuwa nashauri kupitia Msajili wa Hazina na Serikali kwa ujumla kuhakikisha kwamba madeni hayo yanasamehewa ili hati zile miliki zirudishwe kwa wananchi na wakulima waweze kuendeleza hivyo Vyama vyao vya Ushirika na kuendelea kufanya masuala ya uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie tena kwenye upande wa hii Taasisi yetu ya Manunuzi hii PPRA. Ukiangalia katika bajeti za Serikali zaidi ya asilimia 70 fedha nyingi zinakwenda kwenye manunuzi, lakini sheria zilizopo katika hii taasisi ya PPRA zinachangia sana kutengeneza urasimu na matatizo mengi kwenye manunuzi ya mali na bidhaa mbalimbali kwa upande wa Serikali. Kwa hiyo, nilikuwa nashauri Wizara kwa kushirikiana na hiki chombo cha PPRA kuhakikisha kwamba tunafanya marekebisho ya sheria zetu ili kurahisisha kwenye suala la manunuzi na kuondoa urasimu ambao upo katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa Wizara nataka tena nichangie kwenye suala la mali chakavu. Maeneo mengi yana mali chakavu ambazo zilitakiwa ziwe disposed, ziwe zimeuzwa ili Serikali iweze kupata fedha kutokana na mali hizo nyingi. Lakini utaratibu unaotumika kwenye hizi procedure za disposal zinatuletea shida sana, unakuta kwa mfano mali za Serikali ziko kwenye Ubalozi nchi za nje. Lakini utaratibu ni kwamba huwezi kuuza hizo mali mpaka ufanye uthaminishaji. Sasa unaweza ukakuta afisa anatumwa kwenda nje kufanya uthaminishaji lakini gharama zile anazotumia kwenda nje ni kubwa zaidi kuliko mali ile ambayo itauzwa hapo baadaye.

Kwa hiyo, nilikuwa naomba Serikali iangalie uwezekano wa kufanya marekebisho kwenye sheria zetu ili kurahisisha uuzaji wa hizi mali mbalimbali ambazo ni chakavu.

Mheshimiwa Spika, mfano mwingine ukienda pale Dar es Salaam utakuta kuna mabehewa mengi ya TRC yako mengi na ni chakavu na ni ya muda mrefu, lakini ukiuliza kwa nini hayauzwi utaambiwa kwamba mchakato bado unaendelea kwenye upande wa Serikali. Kwa hiyo tulikuwa tunaomba Serikali iangalie uwezekano wa kuweka sawa na kuuza hizi mali ili zibaki ziendelee kuwa chakavu Serikali iweze kupata fedha na ziweze kutusaidia kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho naomba nichangie kwenye upande wa ulipaji wa madeni; kwanza nipongeze Serikali ya Awamu ya Sita inayoongezwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan - Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kusimamia na kuanza kulipa madeni mbalimbali ya Wakandarasi pamoja na wafanyabiashara. (Makofi)

Kwa hiyo, kwenye upande wa eneo hili nataka niishauri Serikali na niiombe iendelee kusimamia kufanya uhakiki wa madeni hayo na kulipa Wakandarasi pamoja na wafanyabiashara hususan wale wafanyabiashara wa pembejeo ambao walisaidia sana kwa wakulima wetu. Lakini ni kwa muda mrefu sasa madeni yao bado hayajalipwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hayo machache naunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)