Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Ndugu Mohamed Mchengerwa na Naibu wake Mheshimiwa Pauline Gekul pamoja na timu ya wataalamu Wizarani kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimwa Spika, nianze mchango wangu kwa kuipongeza timu yetu ya soka ya wasichana ya Serengeti Girls kwa hatua kubwa ya kuingia fainali ya kombe la dunia itakayofanyika huko India kuanzia tarehe 11.10.2022 hadi 30.10.2022.

Mheshimiwa Spika, soka la wanawake nchini Tanzania linakua kwa kasi ya ajabu na timu hizi zimeonesha mafanikio makubwa ukilinganisha na zile zinazotoka ukanda wa CECAFA, COSAFA na zile za Kanda za Afrika Magharibi.

Mheshimiwa Spika, timu hii imetupa heshima kubwa kwa hiki kilichotokea, soka hili la wanawake Tanzania limefanikiwa kuitangaza vyema nchi kupitia timu ya Taifa ya Twiga Stars na Serengeti Girls ambazo zimeweza kutwaa vikombe mbalimbali, kushinda katika mechi kubwa za kimataifa na kuipaisha nchi yetu katika viwango vya soka Barani Afrika na duniani.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio ya kubeba makombe mbalimbali na kuingia fainali ya kombe la dunia kwa wasichana wenye umri wa chini ya miaka 17, soka la wanawake nchini linakabiliwa na changamoto kubwa za aina mbalimbali, na ninazitaja kama ifuatavyo; kwanza kuna wakati maandalizi ya timu za taifa za wanawake kushiriki katika mashindano huwa duni sana; pili, kumekuwa kuna tatizo la kuibua vipaji vya wachezaji kutoka ngazi za vijiji, kata, wilaya na mikoa na tatu, kuna tatizo la uhaba wa makocha na waamuzi wa kike hapa nchini Tanzania.

Mheshimiwa Spika, nne, kuna tabia ya wasichana wanaocheza soka kuiga tabia za kiume na hivyo kupoteza uhalisia wao kama wasichana. Tabia hiyo imehusisha uvaaji wa suruali, pensi, fulana na kofia za kiume. Vilevile wachezaji wengi wameiga kutembea kitemi kama watoto wa kiume. Kwa mawazo yangu, kitendo hiki kimesababisha wasichana wetu wakadhalilishwa huko Cameroon kwa kuhisiwa kuwa walikuwa wavulana.

Mheshimiwa Spika, tano, changamoto nyingine kubwa ya kukua kwa soka la wanawake ni kukosekana kwa wadhamini wengi wa kueleweka

Mheshimiwa Spika, baada ya kuainisha changamoto hapo juu, ninaishauri Serikali ichukue hatua zifuatazo; kwanza Serikali itenge bajeti ya kutosha kuhudumia kambi ya Taifa ya timu za wanawake; pili, ili kuibua vipaji, soka la wasichana lianze kuchezwa katika ngazi za shule za msingi na sekondari. Hii ni pamoja na kuwa na mashindano ya aina mbalimbali kwa watoto hawa katika ngazi ya wilaya, mikoa, UMITASHUMTA na UMISETA.

Mheshimiwa Spika, Serikali iandae mafunzo ya muda mfupi na mrefu kwa walimu na waamuzi wa soka la wanawake na pia Serikali kupitia Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) liwekeze kikamilifu katika soka la wanawake. Hii ni kutokana na ukweli kwamba wamekuwa wakifanya vizuri katika mashindano ya kimataifa.

Mheshimiwa Spika, Serikali ihamasishe makampuni ya udhamini yawekeze kwenye soka na ligi za akina dada kwani wamefanya vizuri kimataifa ukilinganisha na zile soka na ligi za wanaume. Ushiriki wa wanawake katika soka utakuwa zaidi kama wadau zaidi watajitokeza na kuwainua na kutoa sapoti kwa wanamama ambao wanajitoa kwa ajili ya maendeleo ya soka la wanawake.

Mheshimiwa Spika, ninashauri mamlaka husika ziwahimize wachezaji wa kike kuvaa mavazi ya kike na matendo yao yawe kama ya watoto wa kike kwani huko Ulaya na kwingineko, wanasoka wanawake huwa na kila sifa anayostahili kuwa naye mtoto wa kike.

Mheshimiwa Spika, baada ya mchango wangu, naunga mkono hoja.