Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika Wizara hii ya Sanaa, Utamaduni na Michezo. Kwanza nianze kwa kutoa pongezi za dhani kwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na timu nzima ya Wizara kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya. Moja ya kazi kubwa ni pamoja na kutangaza lugha yetu ya Kiswahili katika Tamasha la Dubai Expo kule nchini Dubai. Tunawapongeza sana, lakini hata katika bajeti yenu mmeonyesha namna gani mtaendelea kununua vifaa vya kutafsiri lugha ili kuendelea kukuza lugha yetu ya Kiswahili.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza kwa dhati kabisa Rais wa Jamhuri wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kutenga Shilingi bilioni moja ya kuongeza katika Mfuko wa Maendeleo ya Sanaa. Hii iwe rai kwa Watanzania na wadau wengine mbalimbali kuweza kuchangia mfuko huu ili uweze kuwasaidia vijana wengi wa Kitanzania.

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee katika Wizara hii Shirikisho la Maonesho ya Sanaa na Ufundi Tanzania. Kwenye bajeti ya Wizara hatuoni sehemu ambapo shirikisho hili limepangiwa bajeti, lakini tukiangalia shirikisho hili limebeba ajira kubwa za Watanzania, kwa marika tofauti tofauti; vijana akina mama, wazee na makundi mengine mbalimbali. Shirika hili la Maonesho ya Sanaa wapo wachongaji, wachoraji, wabunifu wa mavazi, wabunifu wa mapishi, watu wa sarakasi na ma-MC.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia, pale ambapo wageni mbalimbali wanakuja kwenye nchi yetu, kitu cha kwanza cha utamaduni tunachokwenda kutambulika nacho ni hivi vikundi vya ngoma, vinakwenda kupokea misafara mbalimbali lakini vinashiriki katika matukio mbalimbali, ndani ya nchi yetu. Itapendeza tukiona watu hawa wanawekwa kwenye bajeti wanatambulika kwa sababu wana mchango mkubwa katika nchi yetu ya Tanzania lakini wamebeba ajira nyingi za kuleta maendeleo katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika,…

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Asia Halamga kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Saashisha Mafuwe.

T A A R I F A

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika ahsante. Nilitaka kumpa taarifa kwamba BASATA nchini Tanzania imesajili mashirikisho manne, lakini haya mengine yanasemwa sana isipokuwa Shirikisho la Sanaa za Maonesho Tanzania, humo ndani kuma ma-MC, ma-DJ, halafu kuna shirikisho sasa la ufundi. Kwa hiyo, nilikuwa nampa taarifa pia kwamba hivi ni vyombo muhimu sana na visaidiwe na bahati nzuri wana uongozi wao unaongozwa na Mama Henjewele.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

SPIKA: Sasa wewe ulikuwa umeshaota kuwa hayo hana kwenye mchango wake? Maana alikuwa hajamaliza bado. Mheshimiwa Asia Halamga.

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Namshukuru ndugu yangu Mbunge wa Jimbo la Hai kwa kuliona hili na yeye, hakika lina mchango mkubwa sana kwa Taifa letu. Hili nisiendelee kuchukua muda kwa sababu ameliongelea pia kwa mapana yake, niombe tu sasa Wizara, lile jengo la Maonesho la BASATA lililopo pale Ilala, basi vikundi hivi vikikusanywa na wakawa wamepewa eneo lile, itasaidia sana hata wageni wanapotoka maeneo mbalimbali ikatambulika kwamba jengo fulani ukifika utakutana na vinyago vinavyochongwa na vijana wa Kitanzania na akina mama wa Kitanzania; vitu kama shanga, bangili, nguo za kiasili, iko center moja ambapo tunaweza tukavipata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuchangia mchango wangu katika eneo hilo, naomba niende kwenye suala la riadha. Nianze kwa kutambua kwanza mchango mkubwa wa watangulizi wetu ambao wamefanya vizuri sana katika mchezo wa riadha. Napenda kumtambua Mzee Filbert Bayi, Gidamis Shahanga, Selemani Nyambui, Juma Ikangaa, Mwinga Mwanjala na Simon Robert. Tunatambua mchango mkubwa sana wa wazee na waasisi hawa katika mchezo wa riadha. Naomba Wizara isiache, iendelee kuwatumia kwa sababu waliwahi kuwa na mchango mkubwa katika Taifa, lakini hata sasa bado wana ushauri mkubwa katika Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza kijana Emanuel Giniki anayetokea Wilaya ya Hanan’g katika Mkoa wa Manyara kwa kufanya kazi kubwa na nzuri na kuweza kushinda mashindano ya riadha kule nchini Geneva tarehe 15 /5/2022. Hivi karibuni vijana wawili wa Kitanzania akiwemo Emanuel Giniki wanatarajia kwenda nchini USA kwa ajili ya mashindano ya kidunia.

Mheshimiwa Spika, naomba Wizara iweze kuwaweka vijana hawa kambini. Changamoto inayowakuta wanariadha wengi ni mazingira na maandalizi ya kwenda kushinda kwao kwa sababu hawana makambi rasmi ya kuweza kujiandaa kwa ajili ya kwenda kupambana huko duniani. Wote tumeshuhudia na tumefurahia alivyokuja hapa amepeperusha bendera ya Kitanzania vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tuweze kuwatumia vijana hawa kwa kuhakikisha kwamba viwanja wanavyotumia vinakuwa na mazingira bora na pia vifaa vya michezo mbalimbali ya riadha wanaweza kupatiwa na wanaendelea kupeperusha bendera ya nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuwapongeza CHANETA kwa kufanya kazi kubwa na nzuri sana. Tunaamini sasa watarudisha heshima ya mpira wa pete na kama ambavyo Serengeti Girls kwenye mipira mbalimbali hii ya kiume sasa wameanza kufanya vizuri, na tunaona kwa namna ambavyo wanawake wote ambao wamefanya mashindano, wameweza kuiletea heshima nchi yetu. Tunaamini CHANETA ikipewa nguvu itafanya vizuri zaidi na kuendelea kuongeza nguvu ya kupeperusha bendera vyema na kuleta vikombe vingi katika nchi yetu ya Tanzania kupitia CHANETA na mipira mbalimbali ya miguu inayofanywa na wanawake wa Kitanzania.

Mheshimiwa Spika, niendelee kuiomba Wizara, kuendelea kutoa semina mbalimbali kwa wasanii. Wasanii wengi saa nyingine wanaadhibiwa siyo kwa kupenda kwao. Wasanii wa Kitanzania ni vijana ambao wanahitaji semina za mara kwa mara, na ikimpendeza Mheshimiwa Waziri waweze kutoa elimu za ujasiriamali kwenye makundi haya, kwa sababu kile kidogo wanachokipata waweze kukihifadhi ili kiweze kuwa na maslahi bora na tija kwao kwa sababu bado ni vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, mchango wangu wa siku ya leo unatosha, niwe nimeishia hapo.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)