Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi siku ya leo kuwa mchangiaji wa pili jioni ya leo katika Bajeti ya Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kumpongeza nakumtakia kila la heri Mheshimiwa wetu Waziri, jirani yangu Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa pamoja na Naibu Waziri wetu Mheshimiwa Pauline Gekul, Katibu Mkuu Hassan Abbas pamoja na Naibu Katibu Mkuu Ndugu Saidi Yakubu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema haya kwa sababu kuna mambo mengi tangu wameingia katika Wizara hii kwa pamoja wameweza kuyafanikisha wakishirikiana na watumishi waliopo katika Wizara hii. Tumeshuhudia sinema ya Royal Tour waliisimamia vizuri na leo inaitangaza nchi yetu ya Tanzania katika medani ya utalii pia wamesimamia timu yetu ya michezo ya Tembo Warriors, Timu ya Taifa ya walemavu ambayo iliweza kufuzu katika mashindano ya Kombe la Dunia ya Timu za Walemavu.

Mheshimiwa Spika, juzi tu hapa tumeshuhudia Timu yetu ya Taifa ya Wasichana chini ya miaka 17 ikifuzu kwa kucheza Kombe la Dunia kule nchini India jambo ambalo halijawahi tokea. Timu zetu za mpira wa miguu hazijawahi tokea wakati wowote ule ukiondoa ile ya walemavu kufuzu kwa ajili ya mashindano haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nitakuwa mtovu wa fadhila kama sitaipongeza Klabu ya Young Africans kwa kuwa na mafanikio makubwa sana katika msimu huu. Mafanikio ambayo yalikuwa adimu katika klabu yao kwa miaka mfululizo minne iliyopita. Nawapongeza lakini nawapongeza pia katika hata zile point ambazo tulipata za kutuwezesha kuendelea kuwa na washiriki wanne katika mashindano ya vilabu barani Afrika wao wamechangia alama 0.5 kati ya alama 30.5. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nawapongeza klabu ya Namungo kwa kuendelea kuchangia katika timu ambazo zinakwenda kucheza msimu ujao wa mashindano ya vilabu Barani Afrika kwa kuwekeza point mbili pale. Hongera sana naona Mwenyekiti yupo hapa wa Namungo, hongera sana Mheshimiwa Hassan. Sana sana niipongeze Klabu ya Simba, Klabu ya Simba imetutangaza vilivyo katika medani ya Kimataifa hasa katika mashindano ya vilabu Barani Afrika, kuweza kushiriki mashindano ya Kimataifa ya vilabu Barani Afrika mara nne, ukaweza kupata nafasi ya kucheza robo fainali mara tatu, si jambo la mchezo ni jambo ambalo linatakiwa kuigwa, ni jambo la mfano ambalo limeiweka nchi yetu katika level ya juu kabisa ya mashindano ya vilabu Barani Afrika. Simba kutokana na mafanikio ya miaka minne wamechangia alama 28 kati ya 30.5 ambazo zimetufanya tuendelee kuwa na vilabu vinne. Alama za klabu ya Simba peke yake zimezizidi alama za nchi maarufu hapa Barani Afrika kama Libya na Nigeria overall kwa timu zao zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningeomba tujifunze kutokana na Simba, haikuwa rahisi sana kwa klabu ya Simba kuweza kupata mafanikio katika medani za Kimataifa haya ambayo wameyapata. Mimi ni mdau wa mpira wa miguu katika mpira wa miguu kuna mambo matatu huwa tunayazungumza ambayo ndiyo msingi wa kuboresha mpira mahala popote unapochezwa. Jambo la kwanza ni utawala bora katika klabu, jambo la pili ni kuwekeza katika wachezaji bora, jambo la tatu ni kuwekeza katika benchi la ufundi. Kwa hiyo, hayo ni mambo matatu ambayo ni ya msingi sana ambayo Simba yote walifanikiwa kuwa nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia Simba walijiongeza kwa kuongeza factors zingine, factor iliyoongezeka ya nne ilikuwa ni kuwekeza rasilimali fedha ya kutosha kwenye klabu. Kama huna fedha huwezi kucheza mpira lakini pia walikuwa na washabiki bora wa mfano Barani Afrika, pia walitumia vyombo vya habari vizuri … (Makofi)

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Ndulane kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mwita Boniphace Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba pamoja na umaarufu wa Simba lakini anadaiwa na TRA bilioni sita, Yanga anadaiwa bilioni tatu. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, futa usemi.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante.

SPIKA: Unajua mimi humu ndani napima tu mashabiki gani ni wavumilivu, wapi uvumilivu hamna. Mheshimiwa Ndulane unaipokea taarifa hiyo.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante nimeipokea taarifa yake lakini ni imani yangu kwamba klabu ya Simba haina shida ya kulipa deni kama hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la sita; ni kwamba Simba waliboresha miundombinu ya uendeshaji wa klabu yao ikiwemo kiwanja cha mazoezi pamoja na program nzima za mazoezi na ushiriki wa timu kwenye mashindano mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nini nichotaka kusema, sifikiri kwamba Simba wamefika mahali ambapo wanatakiwa kufika, lakini wamejitengenezea brand ambayo inapaswa kuigwa na vilabu vingine. Vilabu vingine vinapaswa kujifunza kutokana na Simba ili tuweze kwenda mbele. Nina imani kama vilabu vingine vitajifunza kutokana na Simba sitashangaa kwa speed hii ambayo wanakuja nayo Yanga na vilabu vingine, mwakani sitashangaa kuona vilabu vyetu vinne vyote vikishiriki angalau hatua ya robo fainali Barani Afrika pia sitashangaa pia kuona vilabu vyetu nchini Tanzania vikifikia angalau viwili vikifikia hatua ya nusu fainali kwenye mashindano ya vilabu Barani Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niviombe vilabu vingine viendeshe mpira kisayansi kama ambavyo wanafanya Simba, ingawa niseme tu hapa katikati Mheshimiwa Rais wetu Mstaafu aliwahi kusema wakati fulani tatizo la nchi yetu kuna baadhi ya vilabu vinaendesha mpira, wanawekeza kwenye Kamati za ufundi badala ya benchi ya ufundi, hilo ningeomba lizingatiwe lakini pia tuweze kuona namna ambavyo timu zitasonga mbele.

Mheshimiwa Spika, Simba nao nafikiri hawajafika pale ambapo tunatarajia, haiwezekani miaka minne tunaishia robo fainali, nilifikiri wanapaswa sasa kupiga hatua kwenda mbele zaidi. Ninafikiri hilo linawezekana kwa sababu wametoka mbali, wamefika mbali. Kwa hiyo, niwaombe Viongozi wa Klabu ya Simba wakishirikiana na Serikali yetu kupitia Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo waweze kuboresha mazingira ya klabu zetu ili hatimae ziweze kufanya vizuri zaidi. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Ndulane kengele ya pili imeshagonga.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)