Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi ya kuchangia Wizara ya Michezo; mimi leo yangu ni ya ushauri tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuwateua watendaji wazuri katika Wizara hii Mheshimiwa Mchengerwa na mwenzake Naibu, Katibu Mkuu na watendaji wote wanafanya kazi nzuri kwa kweli, kwa mara ya kwanza na mara nyingi tumeona sasa michezo hii inaenda na watu wanahangaika kwenye maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nimshukuru kwakweli Mheshimiwa Rais kwa sababu Wizara nyingi amechagua watu sasa wenye mtazamo mpana, vijana walikuwa wanalia mara nyingi kwamba tunaambiwa sisi ni vijana Taifa la kesho, kumbe wanasema Taifa la leo, wamepata nafasi tunataka waitendee haki Wizara zote walizochaguliwa vijana, Mheshimiwa Mchengerwa nakushukuru sana kwa uchapakazi wako.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka kushauri mambo machache tu; ushauri wa kwanza alikuja hapa Mfalme wa Morocco tukaoneshwa uwanja hapa Dodoma na magreda yakaenda pale yakatengeneza uwanja ule na tukaahidiwa kwamba uwanja huu utakuwa upo tayari sijajua ni mwaka gani lakini maana yake ulikuwa upo busy kwenye huo uwanja.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nilitaka kujua tu kwamba je, hilo wazo la kujenga uwanja wa Dodoma pale limekufa au linaendelea? Maana sasa sioni kwa mfano kwa Tanzania kama kweli tunapata msaada hivi hata kuweka uzio ni kiasi gani hicho, kuonesha kwamba sisi tuna uwanja na tumeuwekea uzio. Uwanja huu wa Dodoma ambao ndio uwanja wa kitaifa tungeweza kuwa nao kwa sababu tulipata msaada na tungeendelea kuona uwanja kwamba uwanja huu unapendeza kwa Jiji la Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri mwingine ninaotaka kutoa, sasa tukubaliane Wizara hii ya Michezo na Serikali kwa ujumla watupe shortlist hivi tuna mikoa 26, mikoa mingine ina viwanja hivi kuweka nyasi za bandia kwenye hivyo viwanja kuna shida gani? Ni fedha kiasi gani zinahitajika kwenye hivyo viwanja?

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sasa Wizara kwenye bajeti ijayo mtuambie kwamba katika viwanja tulivyonavyo 26 vya mikoa ni vingapi vimewekwa nyasi bandia. Lakini hili niseme mimi niombe TFF kama sio TFF Wizara ya Michezo nendeni mkatoe tuzo maalum kwa Bakhresa (Azam Tv) muwape tuzo maalum wapeni tuzo maalum Bakhresa (Azam Tv) wametufanyia kazi nzuri sana kwenye nchi hii vijana wetu wengi walikuwa sasa wamelewa Ulaya wanatazama ligi za Ulaya, leo kila mtu yupo kwenye tv ya Azam wapeni tuzo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Mheshimiwa Waziri wewe ni kijana, angalia na Serikali yako mkae vizuri na Mawaziri na wetu wengine na Waziri Mkuu nendeni mkamwite Bakhresa na timu yake na makampuni yake yote, kampuni ya Bakhresa inafanya kazi nchi karibu 55 karibu 60 mwambieni tutengenezee nyasi za bandia, mpunguzieni bei zote za vifaa vya michezo, viwanja vyetu vyote vitakuwa na nyasi za bandia kwa kupitia Bakhresa kwa sababu biashara hii anaiweza. Kwa hiyo niwaombe kwamba sisi tusihangike mambo mengi, tuna mtu ambaye ni msamaria na mzalendo wa kweli kweli katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpeni viwanja vyote 26 vya mikoa na vile vya Zanzibar vilivyopo Zanzibar atengeneze mpunguzieni bei ya baadhi ya vifaa vinavyohusika mimi nadhani hilo linaweza kuwa wazo zuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine michezo ni ajira, nilikuwa naomba sasa kwanza demokrasia TFF, kila tukifanya uchaguzi wa TFF wa Rais kila mara kunakuwepo na watu mara wanakamatwa, mara karatasi zimepungua, mara watu wamefungiwa, mara sijui kuna nini, kuna nini TTF, kuna nini humo ndani kila uchaguzi ukija wa TFF hadi watu wafungwe, wengine waende lock up wengine wafanywe nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nikuombe Mheshimiwa Waziri uchungulie humo ndani hii ni kazi ya utendaji; wekeni demokrasia ndani ya TFF, anayegombea kama anastahili apewe fomu, ajaze fomu vizuri na ashinde, kwa hiyo nafikiri kwamba hili nalo tulitazame na tuone linavyokwenda kwenye jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini academy, tujitahidi sasa tuna kanda sijui ngapi ikiwemo Kanda ya Ziwa, lakini kanda zipo nyingi kuna Kaskazini, kuna Kusini, kuna Kanda ya Ziwa tukajenga academy kwa hizo kanda tukubaliane kwamba sasa academy ziwepo kwenye hizo kanda, lakini tuhakikishe kwamba kwa kila timu ya ligi kuu inakuwa na timu ndogo inakuwepo academy zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuhakikishe kwamba hilo linakuwepo, tupate wachezaji bora kwenye maeneo yote, lakini pamoja na hayo niwapongeze sana Tembo Warriors ambao walikuwepo, ile timu ambayo inakwenda kuchezo Kombe la Dunia, mimi naomba hata Wabunge tuwachangie, kwani kuna shida gani mbona watu wengine tunawachangia. Hebu kaeni vizuri tuangalie hayo mambo, tuangalie hawa watu ndio neema tunaipata hivi mtu anahangaika kwenyewe na fimbo yake na nini hadi anashinda anakwenda Ulaya tunashindwa nini kuwachangia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Serikali ikae vizuri wachange na sisi Wabunge tuwachangie, mimi nafikiri kwamba hili ni jambo zuri na timu zote zinazoshiriki tuone nafasi gani tunawachangia ili na wenyewe waweze kucheza vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimefurahi waliokuwa wanazungumzia wanamuziki, jamani wanamuziki wetu wa Tanzania wanahangaika sana, nilikuwa nasoma historia ya Diamond alivyoshinda kwenda kuwa mtu maarufu, wanahangaika wanakwenda kwenye ukumbi wanafukuzwa, wanahangaika sana hakuna chombo cha kuwashika, wakipata wenyewe wakishakuwa maarufu ndio tunaanza kuimba, wamezunguza watu wengi hapa tutafute namna ya kuwashika mkono, vijana wapo wengi hata Jimbo la Bunda tunao vijana wengi sana wanaimba vizuri, lakini namna ya kufika huku inakuwa shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutafute mfuko maalum ambao utakuwepo wa kuwasaidia wasanii, tuweke mfuko maalum uwe chini ya Waziri Mkuu ambao utawasaidia wasanii wetu waweze kufanya vizuri kwa sababu ni ajira. Lakini mfuko huo pia uwepo wa kusaidia timu za Taifa. Sasa timu kama ya Biashara ya Mara leo wamenyong’onyea inafanya vibaya watu wanaiona kama timu imefanya vibaya, lakini ile timu imeshindwa kwenda kucheza michezo ya nje, imekosa nauli ya kwenda huko, sasa leo wanacheza kwenda wapi, wanasikitika Mungu wangu, sasa wanajiuliza tukicheza tukishinda tunakwenda wapi, hakuna fedha ya kutupeleka kucheza michezo ya nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuundeni mfuko wa kusaidia vilabu ili viweze kufanya vizuri tunakokwenda nakushukuru kwa yote hayo. (Makofi)