Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Ester Amos Bulaya

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia na mimi niwapongeze watoto wetu Serengeti Girls kwa kutufanya tutembee kifua mbele, tunakwenda kushiriki michuano ya dunia. Lakini pia nimpongeze Waziri na Naibu wake mmeanza vizuri tuna matarajio na ninyi, tupeni raha watanzania wanapenda michezo wanapenda wasanii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muda mrefu sana tumekuwa tukitamani kwenye mpira wa miguu kusomeka kwenye ramani ya dunia, timu ya Serengeti Girls wametuonesha, kama Taifa Serikali inapaswa kuandaa bajeti stahiki ya kwenda kuwawezesha timu yetu kufanya vizuri, isiwe sasa utashi wa Rais peke yake, iwe commitment ya Serikali kwa ujumla. Hawa watoto wamejiwezesha sasa twende tuka-invest tuchukue Kombe la Dunia lije nyumbani. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulitamani kwa wanaume wamefanya yao kwa kiwango chao, hawa mabinti tuwekeze, tumeona commitment ya timu za wanawake, dada zao kwa Afrika tuliona walivyofanya vizuri COSAFA kama sikosei wamefanya vizuri, hawa na wenyewe wanafanya vizuri. Hii inatukumbusha twende tuka-invest soka la wanawake kuanzia level za wilaya, kuanzia mashuleni na Mheshimiwa Waziri tumerudisha michezo mashuleni kuna timu za wanawake za mpira wa miguu? Mpaka tulalamike wanawake ndio tuanze kusaidiwa, tuanze kupewa fursa kwenye maeneo mbalimbali. Sasa hawa wameonesha uwezo, wakati tunarudisha michezo mashuleni tusiangalie mpira wa miguu kwa wanaume peke yake, tuanze ku-invest kwenye mpira wa miguu kwa wanawake kwenye level za mashule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu tumeona commitment ya mtoto wa kike, sisemi kama wanaume hawafanyi vizuri, lakini hawa wamepewa nafasi na wameonesha. Leo tunatamba tutawaona timu yetu ya Serengeti Girls kwenye ulingo wa kidunia, sio jambo dogo, tumetamani hiyo nafasi. Sasa isiwe utashi wa Rais iwe commitment ya nchi. (Makofi)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo wanafanya nchi zingine.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Bulaya kuna taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante nami nampa taarifa Mheshimiwa Bulaya kwamba ni kweli anavyochangia kwamba Serikali lazima itenge bajeti sio utashi wa Rais. Mathalani tumeona wenzetu wenye ulemavu Tembo Warriors wanakwenda kushiriki World Cup, lakini wana bajeti constrained. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huko nyuma tuliona Rais aliwaita Ikulu wakati wameshiriki katika ile level ya Afrika, sasa wanakwenda World Cup lakini wana bajeti constrained, kwamba wangewatengea specifically kwa kuwa kuna bajeti kwa sababu ya kusaidia makundi haya inakuwa inasaidia sana. Kwa hiyo, nilikuwa nataka kumpa hiyo taarifa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Matiko nilikuwa nasikia mipasho, mipasho ulikuwa unamaanisha nini? Mipasho ya nani? Umesema mipasho ya Rais sijakuelewa maana yako ni nini?

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, utashi wa Rais, lakini tuwe na bajeti kabisa imetengwa kwa haya makundi ambayo unakuta wamefikia level ya kwenda kwenye World Cup na kadhalika. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Bulaya unaipokea taarifa?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naipokea maana leo wanaweza wakawa na Rais ambaye ameona kuna jambo jema kwenye timu zetu, kesho akaja Rais mwingine ambaye sio kipaumbele, lakini tukiwa tuna mpango mkakati kama nchi itatusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie netball (mpira wa pete); hivi kama Serikali mpira wa pete tunauchukuliaje? Na ninashukuru leo viongozi wa CHANETA wako hapa, wamechaguliwa na niwapongeze, wameanza kujitambulisha. Lakini bado hatujawa na mkakati wa kufufua netball kwenye nchi yetu, tuwawezeshe CHANETA, ni chama kidogo hiki hatuwezi kulinganisha na TFF. Hawana wadhamini, hawana fedha, watawezaje kwenda kuangalia vipaji mikoani na wilayani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaona je, na kwa sababu unahusu wanawake; tuanze kuuliza ni kwa sababu na wenyewe unahusu wanawake?

Mheshimiwa Waziri tuna wachezaji wazuri sana wa netball wako maeneo mbalimbali, hawapati fursa unakuta mpaka Wabunge waandae mashindano. Kuna muda mwingine mashindano yanakwama hawana fedha, tuiwezeshe CHANETA, tuanze sasa kuhamasisha na kuandaa mashindano mbalimbali level za wilaya ya netball. Tukarabati viwanja vya netball na kwenye mashindano yaliyopita hivi hivi kimkandamkanda tumepata wachezaji watatu kwenye timu ya Afrika. Je, tukiandaa, je, tukijipanga tutafika wapi? Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri nadhani mmenisikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona kwenye hotuba yako umezungumzia kiwanja cha mpira wa miguu hapa Dodoma. Nilikuwa nataka kujua hiki kiwanja kinahusiana na ule Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ambao zile fedha za huduma kwa jamii? Ndio nilitaka nijue na kama sio hiyo kwa nini? Kwa sababu na wenyewe upo na miongoni mwa fedha zilizotengwa ni shilingi bilioni 262 ukiwepo na ujenzi wa uwanja wa mpira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama sio hizo je, huyu mkandarasi kagoma kutoa hizi fedha na kama Serikali tunasemaje? Nataka kujua hilo yaani kama sio na wakati wameshaingia makubaliano na mradi unakamilika Juni 13 na hawajajenga uwanja, tunataka kujua je, huo uwanja utajengwa lini na makubaliano yanasema hivyo kuwa wajenge kiwanja cha michezo. Tumeamua kumuacha tu atuchezee tu kama nchi na tumeingia makubaliano, hilo pia nataka kujua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haraka haraka Baraza la Sanaa liko dhooful-hali, halina fedha. Ukiangalia mali tu za muda mfupi walizonazo milioni 116, madeni waliyonayo tofauti na mali milioni 350, mtaji wa kujiendesha milioni 234. Hawa ndio wanashughulikia tasnia nzima hii ya Sanaa, hawana Bodi hawa. Je, tumeweka hii sanaa yetu rehani na tunaona vipaji mbalimbali vya vijana wetu. Chombo chao kipo dhooful-hali kiasi hiki? Haya mlipanga kuwapa shilingi bilioni 1.1 mkawapa shilingi milioni 700 tu wajiendesheje? Sanaa imekua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama chombo chao tu hatukipi pesa, tuanze kulia kwenye timu za wanawake, tuanze kulia kwenye netball, tuanze kulia kwenye football, mpaka kwa wasanii ambao na wenyewe wanaliwakilisha vema Taifa letu? Hili suala la Bodi liko kwenye mikono yako, hawana Bodi huu mwezi wa nne, wako dhofuli hali, pesa hawana na ipo kwenye ripoti ya CAG ya mwaka huu, wapeni pesa Baraza la Sanaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunisikiliza. (Makofi)