Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Maliasili na Utalii Mheshimiwa Dkt. Pindi Chana, Naibu Waziri Mheshimiwa Mary F. Masanja na wataalamu wa Wizara na wadau wa maendeleo kwa mchango mkubwa sana kwenye sekta ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, Mlima Kilimanjaro na viunga vyake ni moja ya vivutio muhimu vya utalii ambavyo vimeipatia Tanzania heshima kubwa kimataifa. Ndani ya Mlima Kilimanjaro na maeneo yanayouzunguka mlima kuna vivutio vya aina mbalimbali vya kitalii.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni, Rais wetu alishiriki kikamilifu kwenye filamu ya Royal Tour iliyokuwa na kipengele cha kutangaza utalii ukiwepo Mlima Kilimanjaro. Kutokana na hili, ni vyema tukachukua tahadhari mapema ili watalii watakapoanza kumiminika kuja kutalii Kilimanjaro wakutane na mazingira mazuri. Tusipofanya hivyo, watalii wakija wakikumbana na changamoto watapeleka sifa mbaya kuhusiana na eneo letu na kuathiri idadi ya wageni watakaotembelea Kilimanjaro.

Mheshimiwa Spika, mimi nitachangia kwenye suala la vivutio vya Mlima Kilimanjaro na umuhimu wa kutatua changamoto za vivutio hivyo ili kuwezesha watalii kufika maeneo hayo kirahisi na kuliingizia Taifa fedha za kigeni.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni imegundulika kwamba mti mrefu kuliko yote Barani Afrika umepatikana katika Kijiji cha Tema, Kata ya Mbokomu, Jimbo la Moshi Vijijini, Mkoani Kilimanjaro. Mti huo ambao una urefu wa mita 81.5 upo ndani ya eneo la Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (KINAPA). Ugunduzi huo umeonesha pia huu ni mti wenye miaka mingi zaidi duniani kwani una miaka 600. Mti huu umeupa heshima Mkoa wa Kilimanjaro na Tanzania kwa jumla. Kugundulika kwa mti huo kumeongeza chachu ya watalii kupanda Mlima Kilimanjaro na wengine kwenda kushuhudia mti huo.

Mheshimiwa Spika, licha ya mti huu kuwa kivutio ambacho kinaweza kuiingizia Serikali fedha za kigeni, lakini changamoto iliopo ni ugumu wa kuufikia mti huo. Ili kufika katika eneo la Mrusungu ambapo ndipo ulipo mti huo mrefu zaidi, ni safari ya kutembea kwa mguu kwa takribani muda wa saa nne kwenda na kurudi kwa kupita katika milima, mabonde, mito na makorongo.

Mheshimiwa Spika, ili kutatua changamoto hii, ninaishauri Serikali iboreshe miundombinu ya barabara ili kuweza kuufikia mti huo iwapo watalii watataka kwenda kuuona. Barabara ya kufika kwenye mti huu ni mbaya sana na hii ni changamoto inayowafanya watalii wasitembelee eneo hili.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali ihakikishe kuwa eneo hili linaendelezwa ili liwe na hadhi ya kuwa sehemu ya utalii katika Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro. Vilivile ninaishauri Serikali itengeneze utaratibu wa kuhakikisha wanaokwenda kuuona mti wanalipa ada.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa pili utahusu maporomoko ya maji Materuni. Maporomoko haya ni moja ya maporomoko ya maji katika Mto Mware, Kata ya Uru Mashariki, Jimbo la Moshi Vijijini, Mkoa wa Kilimanjaro. Maporomoko haya yanapatikana katika Kijiji cha Materuni pembezoni mwa Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro. Maporomoko haya yana urefu wa zaidi ya mita 100. Pamoja na kivutio cha maporomoko ya maji, eneo hili la utalii limekuwa maarufu kwani watalii wanaokwenda kuona maporomoko hupata fursa ya kutembelea shamba la kahawa na kujifunza jinsi kahawa inakuzwa, kuvunwa na kusindikwa. Watalii hupata fursa ya kujaribu kwa mkono yao kuchoma na kuandaa kikombe cha kahawa kwa kutumia njia asili ya Wachagga.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa inayokabili eneo hili ni ubovu wa miundombinu ya barabara yenye urefu wa kilometa 15 kutoka mjini Moshi. Kutokana na ubovu wa barabara, watalii hupata shida kufika katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, changamoto za barabara katika maeneo yanayopeleka watalii kwenye vivutio vya Mlima Kilimanjaro zinatakiwa zipewe kipaumbele cha pekee na Wizara ya Maliasili na Utalii kwani wao ni wanufaika wakuu. Ninaishauri Serikali iachane na kuzitegemea TARURA na TANROADS kwani mitandao yao ya barabara ni mingi, na hawajatoa kipaumbele kikubwa kwa barabara za jimbo langu kama zile za kupeleka watalii kupitia Umbwe Gate, Kidia VIP Route, Materuni Waterfalls, Mti Mrefu Kijiii cha Tema huko Mbokomu, Kanisa la Kibosho Singa na maeneo mengine muhimu.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali, huu ni wakati wa kutumia michango ya Corporate Social Responsibility (CSR) unaotokana na mapato ya Mlima Kilimanjaro kutengeneza miundombinu ya barabara katika jimbo langu la Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Spika, baada ya michango yangu hapo juu, naunga mkono hoja.