Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, nianze mchango wangu kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, kwa maono yake ya kiubunifu na hatimaye kubuni filamu ya Royal Tour, filamu hii sio tu imeitangaza nchi yetu kimataifa lakini pia imefungua ajira nchi kwa kuleta watalii wengi. Filamu ya Royal Tour itaongeza pato la Taifa letu na kuinua kipato cha mtu mmoja mmoja na hatimaye nchi mzima. Viko vivutio vingi nchini ambavyo hapo awali havikujulikana kama viko nchini, wapo waliodhani viko nchi za jirani vivutio kama vile Mlima Kilimanjaro, Mbuga ya Serengeti, na kadhalika. Leo dunia nzima inatambua vivutio vyote vilivyo nchini na hivyo kukuza utalii nchini.

Suala la pili ni kuhusu uwepo wa wanyama pori jamii ya tembo na mamba. Wanyama hawa wanaongezeka kwa kasi huku ardhi ikibakia ile ile, lakini pia binadamu tunaongezeka kila kukicha. Madhara ya ongezeko la wanyama pori kwa jamii zetu ni makubwa sana ikiwa na watu kupoteza maisha, mazao ya biashara na chakula. Jambo linalokwenda kuchangia kwa kiasi kikubwa ukosefu wa chakula hapa nchini na kuongeza umasikini kwa watu wetu. Kwa mfano katika Wilaya ya Liwale kwenye Kata za Miruwi, Nangano, Mlembwe, Mkutano, Lilombe na Liwale B. Wakulima kwenye kata hizo wamesharudi kutoka mashambani bila ya chakula baada ya mazao yao kuliwa na tembo, tayari watu hawa wanahitaji msaada wa chakula. Hivyo naiomba Serikali kulitambua jambo hilo.

Mheshimiwa Spika, niliwahi kushauri huko nyuma kutuongezea askari wa wanyama pori, ushauri ambao haukutiliwa maanani na matokeo yake ndio haya. Sasa nazidi kuishauri Serikali ione ni jambo gani bora kuwa na wanyama wengi nchini, huku wananchi wengi wakitaabika na umasikini wa kukosa chakula na mahitaji mengine au kuajiri maaskari wengi zaidi na kusambaza kwenye kata zetu wakasaidia kuwadhibiti wanyama hawa waharibifu.

Mheshimiwa Spika, mwisho naomba mambo mawili yafanyike kwa haraka; kwanza, viwango vya kifuta mchozi viboreshwe ili vibebe uhalisia wa maisha ya leo, baada ya kuviboresha basi vitolewe kwa wakati kulingana na majira ya mwaka ya kilimo nchini. Si vyema mkulima akasubiri miaka miwili kwa mazao yaliyo liwa kwa miaka miwili nyuma, jambo linaloongeza si tu chuki kwa wakulima wetu kwa Serikali yao, pia linaongeza umasikini kwa jamii husika.