Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza na mimi nianze kwa kutanguliza pongezi kwa Waziri na Naibu Waziri kwa kuendelea kuaminiwa katika Wizara hii, lakini niwapongeze pia watendaji wote katika Wizara hii na niwaambie tu waendelee kufanya kazi kwa bidii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nipongeze pia jitihada kubwa za Mheshimiwa Rais ambazo tumeona kwenye Royal Tour, tumeona Rais ameweza kuifungua Tanzania, kuitangaza, kuweza kuwavutia wawekezaji katika sekta mbalimbali ikiwemo utalii na haya mambo yote yanaenda kuleta tija kubwa sana katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mimi ningependa kwanza kuzungumzia migogoro mikubwa ambayo inatokea kati ya maeneo ya Hifadhi pamoja na Vijiji; na ukisikiliza hata katika michango ya Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia migogoro hii.

Kwa hiyo, pamoja na mambo mengine mimi ninadhani kwamba kuna haja ya kuangalia sheria zetu zinazungumziaje masuala haya ya changamoto au migogoro ya ardhi ambayo inatokana na hifadhi zetu pamoja na vijiji. Kwa mfano ukiangalia Sheria ya Wildlife Conservation Act ya mwaka 2009, kifungu cha 16(4) ambacho labda naweza nikakisoma, ambacho kinasema; “The Minister shall, within twelve months after coming into to operation of this Act and after consultation with the relevant authorities, review the list of game controlled areas for purposes of ascertaining potentiality justifying continuation of control of any of such area.”

Halafu kifungu kidogo cha (5) ambacho ndio cha msingi hapa kinasema; “For the purposes of subsection (4), the Minister shall ensure that no land falling under the village land is included in the game controlled areas.” (Makofi)

Sasa hapa sheria inatambua maeneo ya mapori tengefu, lakini sheria inasisitiza kwamba Waziri baada ya kuanza kwa hii sheria, baada ya kutungwa hii sheria ikianza kutumika ndani ya miezi 12, Waziri apitie orodha ya mapori haya tengefu na katika mapitio hayo ahakikishe kwamba maeneo ya vijiji hayatowekwa ndani ya mapori tengefu. Kwa hiyo, vijiji viachwe, maeneo ya vijiji yaendelee kuwa vijiji yasiwe ndani ya orodha ya mapori tengefu. Kwa hiyo, ukisimamia sheria hii inaweza ikandoa baadhi ya hii migogoro tuliyokuwa nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hatuishii hapo tu unajua sheria kwa mfano Sheria ya Ardhi ya Vijiji yaani Village Land Act inatambua kwamba kijiji kinaweza kuwa kile ambacho watu wameishi kwenye eneo hilo kwa zaidi ya miaka 12 kabla ya kuanzishwa kwa sheria hii. Kwa hiyo wamekuwa wakiishi kwa miaka kwa tamaduni zao, wameweka makazi na wameishi kwenye eneo hilo linatambulika kama kijiji. Kwa hiyo, leo hii unavyokuja kutengeneza mazingira ya kumfukuza mtu kwenye eneo ambalo ameishi tangu uhai wake unaanza mpaka anafikia umri huu, unamfukuza, yeye anafahamu eneo lile ni nyumbani kwa hiyo ukimtoa kwenye eneo kama hilo kidogo inakuwa ni changamoto. Lakini mwisho wa siku pamoja na kuwepo sheria hizi zote lengo letu pia ni kuzingatia uhifadhi, kwa sababu maliasili zote tulizokuwa nazo hapa Tanzania kuna haja ya kuhakikisha bado zinaendelea kuwepo zirithiwe, tuwarithishe vizazi na vizazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri na ninafahamu haya mambo ni yanaenda kwenye Wizara tofauti tofauti, Wizara ya Ardhi inahusika na Wizara hii inahusika. Kwa hiyo, waangaalie nafahamu kuna timu ambayo inatatua hii migogoro, lakini waharakishe kwa sababu migogoro imeendelea kuwepo kwa muda mrefu sana na inaleta changamoto kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo naweza kuishauri Serikali kuhusiana na migogoro hii ambayo inatokana na mwingiliano wa maeneo ya uhifadhi na maeneo ya makazi ya watu kwa maana vijiji ni kuhakikisha kwamba hivi vijiji na maeneo yake mipaka yake inakuwa inatambulika. Kwa sababu mipaka ya vijiji ikijulikana na vijiji hivi vikipimwa vizuri mimi ninaamini kwa kiwango kikubwa ule mwingiliano wa kati ya vijiji na hifadhi utapungua kwa asilimia kubwa. Kwa hiyo, naomba sana Serikali izingatie hayo kwa sababu migogoro hii haina tija kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ni kubwa sana na hili litalisisitiza sana nikiwa kama Mbunge kijana, lakini nikiwa kama mama ni uhifadhi. Wananchi inabidi waelimishwe hasa hawa wananchi wanaokuwa wanaishi kwenye vijiji vinavyopakana na maeneo haya ya hifadhi, waelimishwe umuhimu wa wa kuhifadhi maeneo haya ambayo sisi tumeyarithi kutoka kwa mababu zetu, waelewe umuhimu wa utunzaji wa maeneo haya na mchango wake na athari zake katika mazingira kwa ujumla. Kwa sababu wakifahamu na wenyewe watakuwa ni sehemu ya kuhakikisha wanayalinda maeneo haya ya Hifadhi, wanayatunza ili tuweze kuyarithisha kwa vizazi vijavyo. (Makofi)

Kwa hiyo, naomba sana na hili suala ukiangalia kwenye ukurasa namba 114 wa Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi kwenye kifungu cha 69(d) kimezungumzia mambo ya kuimarisha mahusiano kati ya wananchi wanaopakana na maeneo haya ya hifadhi ili kuwafanya wananchi na wenyewe waelewe kwa upana wake umuhimu wa hifadhi na waweze kulinda maeneo yetu ambayo tunayahifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho lakini siyo kwa umuhimu, kule kwetu Kigoma tuna hifadhi yetu ambayo inaitwa Gombe na Mahale. Gombe na Mahale wewe mwenyewe ni shahidi kwa sababu nafahamu umeshawahi kufika. Ulitembelea kule na Mheshimiwa Assa Makanika, Mbunge wa Jimbo. (Makofi)

Sasa hifadhi ile ni hifadhi ambayo wanapatikana viumbe ambao wana upekee sana, kule kuna sokwe mtu na duniani kote sokwe mtu hawa wamekuwa wana umaarufu mkubwa sana. Lakini sasa kuna uhitaji mkubwa wa kufungua njia kwa ajili ya utalii katika eneo hili. Kwa hiyo, naomba, kwa sababu Serikali ni moja waboreshe miundombinu ya kufika katika hifadhi hii na miundombinu ya kule mikubwa zaidi ni uwanja wa ndege. Sasa kwenye bajeti ya masuala ya uchukuzi kila mwaka huwa inatengwa fedha kwa ajili ya kupanua kiwanja chetu cha ndege cha pale Kigoma, mwaka wa fedha uliopita shilingi bilioni nane, mwaka huu imetengwa shilingi bilioni saba.

Kwa hiyo, tunaomba mboreshe miundombinu kwa sababu na yenyewe itakuwa kuchochea kwenye masuala ya Utalii na kwa sababu Serikali ni moja ndiyo maana nasema hapa hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)