Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kwa kunipa nafasi nichangie kwenye hotuba hii ya bajeti ya Maliasili na Utalii na moja kwa moja niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais Mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anawafanyia Watanzania hakika tumeshuhudia akihangaika huku na kule akituhangaikia sisi kama mama anavyohangaikia familia yake tunampongeza sana. Lakini amekwenda mbali zaidi akaamua kutengeneza filamu ya Royal Tour ambayo kimsingi imekuja kufungua nchi yetu kwenye biashara ya utalii na tunaamini kabisa kwamba sasa hivi tutapata watalii wengi na nimedodosa kule Arusha kuna makampuni mengi ya utalii wanasema booking zipo nyingi sana ni juu yetu sasa kujipanga kwa ajili ya kupokea wageni wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Balozi Dkt. Pindi Chana kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais na kumpa nafasi ya juu kwenye Wizara hii kama Waziri. Lakini pia nimpongeze Naibu Waziri Mheshimiwa Mary Masanja kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais akambakiza kwenye nafasi yake ya Unaibu Waziri kwenye Wizara hii, hawa wote viongozi wetu hawa wanafanya kazi nzuri wanatosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii pia kumpongeza sasa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu watendaji wote pale Wizarani kwa kazi nzuri ambayo wanafanya hakika tunawaona tunashuhudia, hata ukisoma hotuba ya Waziri mapato yatokanayo na maliasili nyuki wenyewe tu inachangia percent 3.3 kwenye pato la Taifa, si hivyo tu inachangia percent 5.9 kwa biashara ya nje ya nchi hii lakini biashara ya utalii inatupatia kwenye pato la Taifa percent 17 lakini pia percent 25 ya fedha kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli ni kazi nzuri nilibahatika nilipata neema ya kutembelea Hifadhi ya Ngorongoro mwezi wa tatu nikiwa na Kamati yangu pamoja na Hifadhi ya Mkomazi kwenye mradi wa faru kazi zinazofanyika kule zinafurahisha tunaamini kabisa kwamba uhifadhi na utalii unakwenda kukua kwa kiwango kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naendelea kupongeza Wizara, lakini pia niseme kwamba kwa jinsi utalii unavyokua nchini mwenzangu asubuhi alizungumzia kuhusu cable cars, hakika milima yetu kuna milima miwili Mlima Kilimanjaro na Mlima Meru ni vivutio vikubwa sana kwa utalii nchini hapa. Nilipata neema ya kwenda South Africa nikashuhudia jinsi ambavyo cable cars zinafanya kazi naamini kabisa kama huku tunakokwenda tutajenga hizo cable cars kwenye Mlima Kilimanjaro na Mlima Meru tutasomba watu wengi kule mjini ambao watakwenda kupanda mlima na kushuhudia vivutio vya utalii, lakini pia kuingiza na kuongeza pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na salamu zangu hizi za pongezi, kule kwenye jimbo langu kuna changamoto ya mpaka wa Kijiji cha Olkung’wado na Hifadhi ya Arusha. Changamoto hii ilisababishwa na TANAPA kununua mashamba mawili yaliyopo kwenye Kitongoji cha Momella na inavyoelekea ni kwamba Serikali ya Kijiji na wananchi hawakuhusishwa vizuri matunda yake ni kwamba sasa hivi kuna sheria mbili zinafanya wananchi wanapata shida, wanateseka kidogo. Sheria ya Uhifadhi inawafanya wananchi pamoja na kwamba kile kijiji yale mashamba walikuwa wanaishi pale, wamezaliwa pale wanaonekana kwamba wamevamia. Kwa hiyo, wahifadhi wakiwaona wakiwa palepale kwenye mashamba yale wanawaona kama wameingilia hifadhi. Pia Sheria ya Ardhi inaona kama wame trespass, wamevamia sehemu ambayo si ya kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nishauri Sheria ya Ardhi ina sehemu ambayo inasema kwamba yaani inatoa mwanya kwamba kama mwananchi amekuwa kwenye ardhi kwa zaidi ya miaka 12 anaweza akapewa kwa kutumia kipengele cha address possession.

Mheshimiwa Spika, nasema kwamba Wizara hizi mbili Maliasili na Wizara ya Ardhi wakae chini, waangalie ni wapi makosa yalifanyika kwa sababu kile kijiji kina Mwenyekiti wakati mashamba haya yananunuliwa alikuwepo Mwenyekiti na Mwenyekiti ardhi ipo chini yake sijui kama aliridhia hayo manunuzi. Kwa hiyo, kwa kweli nashauri kwamba Waziri wa Maliasili na Waziri wa Ardhi wakutane waone ukweli wa hili jambo kwa sababu ukifuatilia mgogoro huu wananchi wanavurugwa mara kwa mara, wanapigwa mabomu wakati mwingine, wanafukuzwa, mifugo yao inafukuzwa, lakini pia mashamba yao yanaharibiwa na jambo hilo si sawa ni tofauti na ni kinyume kabisa na azma ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi ambayo inazungumzia maisha bora kwa Watanzania wote, hilo ni ombi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matukio yaliyotokea mwaka 2017/2018 hayafurahishi hata kidogo na ndiyo maana nilisema niliseme hili kwa sababu wahifadhi wana element ya kupenda wanyama na misitu yao kuliko binadamu na hilo si kosa ndiyo kazi waliyopewa, lakini pia tukubali kwamba na binadamu wana value yao na tunataka wananchi wafurahie maisha yao katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)