Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Fatma Hassan Toufiq

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia hoja ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Nami niungane na Wabunge wenzangu kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu na watendaji wote kwa kuandaa bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi leo muda ukiniruhusu nitaongelea kuhusu Royal Tour na pia nitazungumzia kuhusu uendelezaji wa fukwe pamoja na umuhimu wa mafunzo mara kwa mara watoa huduma wa kitalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami niungane na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Mama yetu Samia Suluhu Hassan ambaye ni mhusika mkuu katika filamu hii ya Royal Tour. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ana dhamira ya dhati ya kutangaza utalii wa Tanzania na vivutio vyake ili kuliongezea pato Taifa letu, pongezi sana kwa Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ameimarisha utalii katika Tanzania katika ile filamu ya Royal Tour sambamba na hilo Mheshimiwa Rais ameibeba Wizara ya Maliasili na Utalii katika nchi yetu pia Mheshimiwa Rais ameiweka Tanzania katika anga za kimataifa kwa kuitangaza hii filamu ya Royal Tour. (Makofi)

Mheshimiwa Rais pia amevutia wawekezaji wengi sana, ninaamini kabisa baada ya hii filamu ya Royal Tour watalii wengi wameanza kuja na wengine wengi sana watakuja. Halikadhalika hivi karibuni tumeona tija kwamba mwekezaji mkubwa sana kutoka Marekani ambaye ni Munir Walji amefika nchini kuhusu uwekezaji katika hoteli za kitalii. Hii ni hatua ya mwanzo na tunaamini kabisa watalii wengine wengi watakuja hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika mimi naamini watalii wataongezeka sambamba na hilo safari za ndege zitaongezeka, lakini sambamba na hilo uelewa wa Watanzania kuhusu utalii nao utaendelea kuongezeka na watalii wa ndani wa nchi yetu yaani Watanzania wengi zaidi watakwenda kutalii kwa hiyo hivyo pato la Taifa litazidi kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa ujumla hii ni faida kubwa sana kwa Royal Tour ambayo Mheshimiwa Rais wetu ameifanya na tuendelee kumpongeza, tumtie shime na tuendelee kumuombea Mwenyezi Mungu ampe afya njema ili kusudi aweze kuliongoza Taifa letu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kuwa Wizara iendelee kuweka juhudi katika kutangaza na kuimarisha huduma zenye hadhi ya kimataifa, lakini sambamba na hilo wanafunzi wengi waendelee kuelimishwa umuhimu wa utalii ili kusudi wajenge tabia na wao watakapokua waweze kuwa watalii. Lakini sambamba na hilo ushauri mwingine waandishi wa habari waweze kupewa uwezo wa kuweza kuripoti habari zaidi zinazohusiana na masuala ya maliasili na utalii ili kusudi waweze kuitangaza vizuri nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo Watanzania nao pia waendelee kuhabarishwa kuhusiana na masuala ya utalii ili kusudi na wenyewe nao pindi wanapokutana na wageni waweze kuwaelezea kuhusiana na vivutio vya nchi yetu vilivyopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba pia nizungumzie kuhusiana na uendelezaji wa fukwe ili kuboresha utalii; kuna haja ya Serikali kutafuta wawekezaji watakaojenga mahoteli ili kuweza kuboresha huu utalii wa fukwe kwani hii itasaidia kwamba wale wageni watakaokuwa wametoka kwenye mapori, wametoka kwenye misitu basi wanakwenda kwenye fukwe ili kusudi nako kule waweze kufanya utalii na kupumzika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilipenda kulizungumzia ni mafunzo ya mara kwa mara kwa watoa huduma za utalii, hili nalo ni eneo muhimu sana kwa sababu watalii wanaokuja sasa hivi Tanzania yaani wanaokuja kwa kurudia kwamba wakija mara ya kwanza wakitaka kurudia tena hawazidi asilimia 20. Kwa hiyo, ipo sababu ni kwamba hawa waongoza utalii waweze kupewa mafunzo zaidi ili kusudi wawe na mbinu bora zaidi za kuweza kuwavutia watalii watakaokuja mara kwa mara ili kusudi kuweza kuendeleza utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo najua kwamba wenzetu Chuo cha Mweka wameweza kutoa mafunzo haya walau kwa waongoza utalii 1,060. Kwa hiyo, naomba waongezwe wengine ili kusudi mwisho wa siku waweze kupata ujuzi na wakipata ujuzi ina maana kwamba wataweza kusaidia katika kutangaza utalii, askari wanyama pori, wale askari wa misitu na kadhalika kwa hiyo hawa wote waweze kupewa mafunzo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilitaka kuzungumzia nikuhusiana na cultural tourism. Bado hatujalitumia sana eneo hili wenzetu kwa mfano wenzetu Ethiopia asilimia 70 ya utalii wao wanategemea kwenye cultural tourism, sisi tuna makabila mengi sana na tunaamini kabisa na sisi tukijikita katika cultural tourism naamini kabisa tunaweza tukapata watalii wengi sana zaidi.

Kwa hiyo, ushauri wangu tutume wataalam watakaoenda kujifunza kwani sisi tuna makabila mengi sana kwamba ukienda kule kwa wahehe the way wanavyo dress unajua kabisa hawa wanaonekana, ukienda labda usukumani the way wanavyo dress wanajulikana, ukienda umasaini uhayanina maeneo mengine yote. Kwa hiyo, tukiwa na ile cultural tourism mimi naamini kabisa watalii wengi watakuja basi na hiyo itasaidia kuongeza tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua muda siyo rafiki baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)