Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia katika Wizara ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kutoa pongezi kubwa kabisa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Samia Suluhu Hassan, kupitia filamu ya Royal Tour Mheshimiwa Rais ametoa muda wake, Mheshimiwa Rais ametuheshimisha Watanzania na faida nyingi tunaziona zimeanza kutokea, lakini tunaamini baada ya mwaka mmoja tutaona manufaa makubwa katika nchi yetu kupitia filamu ya Royal Tour iliyotambulishwa na Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mfupi huu tu tayari mapato yameanza kuongezeka, lakini pia imesababisha kuendelea kutambulika kitaifa na kuendelea kuongeza mahusiano kati ya Tanzania na nchi mbalimbali huko ulimwenguni, huko duniani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuupongeza Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (CCM), kupitia Katibu Mkuu wa Vijana kwa kuwahamasisha vijana wa Kitanzania na hivi leo tunavyoongea wameondoka Dodoma vijana kutoka mikoa mbalimbali wakielekea Ngorongoro kwa ajili ya kuendeleza muendelezo wa filamu hii ya Royal Tour na vijana wa Kitanzania hawa wanaenda kushuhudia maajabu ya nchi yetu ya Tanzania. Ni zaidi ya vijana 963 kwa hiyo, tumpongeze Katibu Mkuu wa Umoja wa VIjana, Ndugu Kenani Kihongosi, Wenyeviti wa Vijana wa Mikoa pamoja na Makatibu wao kwa kuhamasisha vijana wengine wa Kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri Mheshimiwa Pindi Chana, Naibu Waziri, lakini pia Katibu Mkuu. Ni kwa muda mfupi wameteuliwa kwenye Wizara hii, lakini tunaona namna gani ambavyo wamejipanga kuifanya kazi na kwa nini wamejipanga kuifanya kazi?

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo changamoto mbalimbali ambazo ziko ndani ya Wizara, lakini unaona wameendelea kuungana na Serikali kupitia timu ya Mawaziri nane kuweza kutatua changamoto mbalimbali za kimipaka kati ya hifadhi pamoja na vijiji. Niendelee kutoa rai ya kushirikisha Wenyeviti wa Serikali pamoja na viongozi wa ngazi za chini katika kutatua na kubaini mipaka kati ya vijiji na hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuipongeza Wizara kwa kuendelea kusimamia miradi mbalimbali ndani ya Wizara ikiwemo mradi wa REGROW kule Iringa, mradi wa Saanane kule Mwanza, Geti la Nabi kule Serengeti na miradi mingine mbalimbali katika nchi yetu ya Tanzania. Kwa namna ya kipekee niendelee kukushukuru na niishukuru Wizara kwa kufungua mlango unaopita Mamire katika Hifadhi ya Tarangire njia ambayo inakuja Babati, tunawashukuruni sana kwa sababu tunauona sasa Mkoa wa Manyara utaunganika na Kanda yake ya Kaskazini kwa maana ya utalii wa kuanzia Tanga, Kilimanjaro, Arusha na sasa hivi sasa Manyara imeenda kufunguliwa kwa kufunguliwa Geti la Mamire. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuiombe Serikali kwenda kutengeneza changamoto tuliyokuwanayo kwa sasa ni barabara. Tunaomba tutengenezewe barabara ili sasa Mkoa wa Manyara uweze kufunguka na bahati nzuri Mkoa wa Manyara una vivutio vingi vipya na Mheshimiwa Waziri nichukue nafasi hii kumpongeza RC wetu Makongoro Nyerere pamoja na ma-DC wote wa Mkoa wa Manyara kwa kuendelea kuutangaza utalii na kuibua vivutio vipya vya utalii. Kufunguka kwa geti hilo kutasaidia Mlima Hanang, kule Mbulu kuna kanisa la kipekee kabisa na maeneo mengine mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siku ya leo katika Wilaya ya Hanang, DC wetu Janeth Mayanja atakuwa na shughuli ya kuitambulisha Royal Tour ndani ya Wilaya, lakini kwa kuwakaribisha wadau mbalimbali na kuendelea kutangaza Wilaya, lakini Mkoa, kwa ujumla wake Wizara ya Maliasili na Utalii. Nikuombe Mheshimiwa Waziri baada ya kumaliza kupitishiwa bajeti karibu sana Mkoa wa Manyara uje ujionee kazi wanazozifanya viongozi wa Serikali, lakini kazi wanazozifanya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa kipekee niwashukuru vijana wa Mkoa wa Manyara kwa kutengeneza filamu ya Royal Tour ya kwetu ya Mkoa. Nimuombe Mheshimiwa Waziri, uniruhusu siku moja nikuletee vijana wale uje utambue kazi kubwa ambayo wameifanya ya kuungana na Mheshimiwa Rais ya kutangaza utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa kipekee niwashukuru vijana wa mkoa wa Manyara kwa kutengeneza filamu ya Royal Tour ya kwetu ya mkoa nimuombe Mheshimiwa Waziri uniruhusu siku moja nikuletee vijana wale uje utambue kazi kubwa ambayo wameifanya ya kuungana na Mheshimiwa Rais ya kutangaza utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende sasa kwenye changamoto wanazozipitia vijana katika masuala ya ajira na mazingira ya kazi na leo nitaongelea vijana ma-tour guide pamoja na wapagazi ambao ni vijana wanaohusika na kupandisha mlima. Miaka kumi iliyopita Wizara pamoja na makampuni ya utalii pamoja na wapagazi na tour guides walikubaliana haya yafuatayo; kwanza, vijana kwa siku watakuwa wanalipwa dola 10 ambao ni wapagazi, lakini ma-tour guides watalipwa dola 20. Sasa kiwango hiki cha fedha kwa kwelli kwa sasa hivi hakikidhi mahitaji ya vijana wa kitanzania tunaomba sheria ije na ibadilishwe ili vijana hawa waweze kupata maslahi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, lakini sambamba na kutangaza wageni wetu kuja nchini kwetu watu namba moja ukiachana na Migration wanaofanyakazi kubwa ya kuwa-handle wageni na wanaoishi nao na kuisemea vizuri nchi yetu ni hawa vijana ambao wanaopandisha watu milimani ama wanatembea nao kuwaonesha vivutio mbalimbali vya nchi yetu. Tunaomba Wizara isimamie makampuni vijana hawa wanawapandisha watu milimani wakiwa wana masweta ya kawaida. Kwa hiyo, tuombe Wizara isimamie vijana hawa wapandishe na wafanye shughuli hizi wakiwa na vifaa ambavyo vinastahili, lakini kwa kuzingatia maslahi ya vijana hawa.

Tatu, tuombe Wizara imefanya vikao mbalimbali na wadau wa utalii, lakini tuombe Wizara sasa ikutane na vijana hawa ili kuweza kujua changamoto mbalimbali ambazo zinawakuta kwa sababu wana kero nyingi na wanatamani Serikali yao iwasikilize ili kuweza kuboresha sasa idadi kubwa hii ya wageni wanapokuja waweze kupokelewa na picha nzuri ya vijana wa Kitanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunao watu wanaitwa waiter ama waitress kwenye mahoteli, kwa asilimia kubwa vijana hawa wa Kitanzania wanasomea na baada ya kusoma wakienda kuajiriwa hawaajiriwi wanaitwa ni ma-trainee anakaa trainee mwaka wa kwanza, mwaka wa pili miaka mitano mtu anaenda kuzeeka hapa kuna kichaka cha kuficha ajira ya Watanzania, ajira ya vijana haki stahiki zao. Kwa hiyo tuombe vijana hawa iwe kuna kikomo cha mtu awe amefuzu elimu yake na anapoenda kuajiriwa awe ni mwajiriwa na siyo ni trainee tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuiombe sasa Serikali kwenye ripoti ya CAG imeeleza kwamba kuna vitalu vilitangazwa na vikalipiwa, sasa tuombe tusichafue na tusijitie doa vile vitalu ambavyo vimelipiwa wale watu vitalu hivyo wapatiwa na kuendelea kuhakikisha kwamba ni kweli tumeutangaza utalii ni kweli zile fursa na faida tunaziona kwa watu hawa kuondolewa usumbufu huo katika kupewa vitalu vyao. Lakini pia tukumbuke kwamba tuna kila sababu sasa ya kuweza kuongeza muda wa vitalu kwa sababu vitalu mtu anapochukua ana...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na naendelea kupongeza Serikali kwa kazi nzuri. (Makofi)