Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye bajeti ya Wizara hii ya Maliasili na Utalii. Naomba nianze kwa kumpongeza tour guide wetu namba moja Tanzania naye sio mwingine ni Mama yetu Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuifungua nchi yetu kiuchumi, lakini vilevile kwa kuendelea kuitangaza nchi yetu kiutalii na kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia filamu ya Royal Tour tumeona mafanikio yake yameanza kuonekana na mimi binafsi pamoja na wananchi wa Mkoa wa Arusha hususani wadau wa utalii ambao baadhi yao wako hapa siku ya leo tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa jitihada zake hizi za kuendeleza sekta hii ya utalii, lakini vilevile tunamuunga mkono na tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Wizara pamoja na taasisi zake pia basi zijitahidi kwenda na kasi ya Mama Samia Suluhu Hassan ili tuweze kukuza utalii wetu hapa nchini. Mkoa wa Arusha ukiangalia uchumi wake kwa kiasi kikubwa unategemea shughuli za utalii. Sekta hii ya utalii pia ni sekta ambayo inachangia sana kulisha sekta zingine kama kilimo, ufugaji, usafirishaji na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii mtalii akitua pale uwanja wa ndege wa KIA wanufaika ni wengi na sio tu sekta zile zilizo rasmi kama kwenye mahoteli, tour guides nakadhalika, lakini vile vile madereva teksi ambao wapo kwenye sekta ambazo sio rasmi wanafaidika, wakulima wa mazao mbalimbali wanafaidika, wafugaji wetu wanafaidika na vile vile wakina mama wanaouza shanga, wanaouza vinyago wanafaidika na ujio wa watalii hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile sekta hii inachangia zaidi asilimia 25 ya fedha za kigeni ambazo ni muhimu sana katika ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. Kwa kuonesha mafanikio haya ya sekta hii naiomba sana Wizara nasisitiza iendane na kasi ya jitihada kukuza sekta hii ili basi sekta hizo zingine nilizozitaja ziweze vilevile kukua kutokana na faida hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia ripoti ya kidunia kwenye masuala ya utalii (World Economic Report) utaona Tanzania ni moja ya nchi ambazo inaongoza kwa vivutio vizuri vya utalii na vivutio vya asili vya utalii. Cha kusikitisha kidogo ni kwamba huduma zetu bado ziko chini kwenye masuala ya utalii na kwenye sekta ya utalii kikubwa kinachoangaliwa na mtalii akija hapa nchini ni jinsi gani tunaweza kumhudumia mtalii yule kwenye huduma ambazo ziko kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiongelea kuhusu huduma kikubwa kinachoongelewa hapa ni idadi ya vitanda tulivyonavyo kwa ajili ya kulaza wageni wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwenye tathmini mbalimbali zilizofanyika idadi ya vitanda tulivyokuwa navyo hadi mwezi Septemba, 2021 ni vitanda 560 tu, ukilinganisha na nchi jirani yetu ya Kenya ambayo ilikuwa na vitanda milioni 3.1 kwa kipindi kama hicho mwaka jana. Jumla ya vitanda vinaangaliwa kwenye mahoteli yenye hadhi za kimataifa ambazo zinaweza kulaza wageni wetu. Mahoteli mengi ukiangalia yamejengwa kipindi cha nyuma ambacho kilikuwa na msamaha wa kodi mbalimbali na hiyo iliweza kuwa-attract wawekezaji wetu wengi kuweza kuwekeza kwenye sekta hii ya maliasili na utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Wizara iangalie jinsi gani itaweza kurudisha misamaha hii ya kodi (deemed capital goods) ili kuweza kuwezesha wawekezaji zaidi waweze kuwekeza kwenye sekta hii ya utalii kwa kujenga mahoteli yenye hadhi za kimataifa kwa kulaza wageni wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi uliopita Katibu Mkuu wa Wizara hii aliweza kukutana na wadau mbalimbali wa utalii wa Mkoa wa Arusha na vilevile waliweza kuwasilisha changamoto zao mbalimbali. Changamoto kubwa ambayo wadau hawa waliwasilisha ni kuwepo kwa gharama kubwa ya viingilio wanayotozwa wataalii wakiingia hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, binafsi nimefanya tathmini mbalimbali na nimegundua kwamba kweli bei kwenye eneo moja tu la tozo, wageni wetu wanazolipa kwenye park fees nchi jirani ya Kenya wanatoza kati ya dola 30 mpaka dola 40 wastani, lakini sisi tunatoza wastani dola 50 hadi dola 70 na hiyo ni eneo moja tu. Kuna maeneo mengi ambayo gharama tunazowatoza watalii wetu ni kubwa na hii inapelekea watalii wetu, kuamua kwenda nchi jirani ya Kenya kwa ajili ya kutafuta unafuu wa bei hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namuomba sana Waziri wakati anahitimisha hapa hotuba yake basi aweze kutuambia mikakati iliyonayo Serikali kwa ajili ya kupunguza gharama hizi za utalii hapa nchini ili basi tuweze kuingia vizuri kwenye soko la ushindani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine ambayo wadau hawa waliwasilisha kwa Katibu Mkuu wa Wizara hii ni waongoza utalii wanalazimika kulipa leseni zao kwa dola. Naomba sana Waziri wakati anahitimisha hapa pia aweze kutueleza basi Serikali itafanya jitihada gani ili kuwawezesha wadau hawa wa utalii, waweze kulipa leseni zao kwa fedha za kitanzania ili basi kuwapunguzia makali pale thamani ya dola inapopanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)