Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwakunipa nafasi. Na mimi nianze kupongeza Wizara ya Ujenzi kwa hotuba nzuri ambayo tunayo mbele yetu na tunaendelea kuijadili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze na jambo la Njombe Mjini, nashukuru kwamba ahadi ya Rais naona inaelekea kwenye ukweli kwamba nimepata kilometa nne za barabara za mjini nashukuru sana naomba hiyo kazi ifanyike. Kwa sababu iko hapa kwenye kitabu bado sijajua utekelezaji utakuwaje lakini naona mtunda na mategemeo ni mazuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja tu ambalo linaleta shida katika mji wa Njombe, ziko alama za “X”. Alama zile zimewekwa na TANROADS, alama zile zinawatia umaskini wafanyabiashara na wananchi wa Njombe. Alama zile zimewekwa miaka mingi hazijulikani lengo lake ni nini, nyumba zile wananchi wanalipia kodi, Wizara ya Ardhi bado inawatambua kama ni wamiliki halali wa vile viwanja, lakini wale wananchi zile nyumba hawawezi kukarabati, kuziendeleza na wala wakienda nazo benki hawawezi kupata mkopo kwa kuweka dhamana zile nyumba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huku ni kuwatia umaskini wananchi, naomba Wizara ifanye maamuzi kama haina fedha za kuwalipa fidia ama kufanya marekebisho ya zile barabara basi ifute zile “X” mara moja na iwaruhusu wananchi waendelee na maendeleo yao na ifanye kwamba barabara ya Mjini Njombe iwe nyembamba kama ilivyo sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tutaridhika kabisa na ile barabara ilivyo, na tuko tayari kufanya mji wetu uendelee kuwa bora, kuliko sasa mmetuweka katika maisha magumu, nyumba zimetiwa alama za “X” haziendelezwi, mji ni mchafu watu wanashindwa kuuendeleza. Naomba sana Mheshimiwa Waziri uliangalie hilo suala la mji wa Njombe na alama za “X”.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la barabara ya Ludewa - Njombe. Barabara hii inaanzia katika msitu wa Itoni pale Nundu, barabara hii naona imetengewa fedha shilingi bilioni 35; ni fedha kidogo mno kwa barabara hii. Lakini kingine ambacho ni cha kushangaza, barabara hii inaanzia kujengewa Lusitu kwenda Mawengi. Barabara inaanza kujengwa kilometa 50 ndani, naomba Mheshimiwa Waziri arudishe barabara hii ianzie Itoni kuelekea Ludewa na iongezwe fedha kwa sababu huku ndiko tunakozungumza kila siku habari ya Mchuchuma na habari ya Liganga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, habari ya Mchuchuma na Liganga imeanza kuzungumzwa kwenye mabunge tangu Bunge alijahamia Dodoma, tangia watu wengine humu ndani hawajazaliwa mpaka sasa wanakuwa Wabunge, Mchuchuma - Liganga na tunalalamika nchi haina fedha lakini tumeacha mali inalala Ludewa. Chuma kipo pale, tunataka kuanzisha viwanda, tutaanzisha viwanda gani bila chuma? Niwaombe sana tutengeneze barabara ya Ludewa ili kusudi tuweze kutoa kile chuma tufanye maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la TAZARA. Tunazungumza habari ya reli ya standard gauge, ni jambo jema na wengi wamesema sana juu ya reli na kwamba reli ni uchumi. Lakini hebu tujifunze kule TAZARA kuna shida gani? Tunahangaika na barabara ya Tanzania Zambia kuikarabati kila mwaka, mizigo yote ipo barabarani, reli tupu haina kazi. Tunazungumza habari ya bandari kavu, sisi wa Kusini na sisi tunasema kama bandari kavu inatakiwa na ni muhimu tuiweke Mbeya ili kusudi mizigo ya Kusini mwa majirani zetu ipite kwenye bandari kavu itakayojengwa Mbeya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sikusema toka mara ya kwanza lakini dakika zangu tano namuachia jirani yangu ili na yeye apate nafasi ya kuchangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la madaraja. Sisi tumeomba katika Halmashauri ya Mji wa Njombe, tujengewe daraja katika kijiji cha Mamongolo kuvukia kijiji cha Lupira, Wilaya ya Makete ili kusaidia wananchi kule waweze kuvuka kwenda hospitali kupata matibabu. Kuna mto mkubwa pale hauna daraja, lakini nimejaribu kuangalia kwenye kitabu sijaona, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri utakapo…
MWENYEKITI: Ahsante.