Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kukushukuru kwa kunichagua leo, lakini na mimi nimuombe Mheshimiwa Waziri, nimeona kwenye bajeti yake kwenye suala la barabara ya kutoka Mtwara kwenda Nanyamba - Tandahimba - Newala - Masasi wametenga pesa pale, lakini jambo hili kwa Mkoa wa Mtwara sio la kwanza. Ukisoma bajeti iliyopita ya Wizara ya Ujenzi walitenga pesa, lakini barabara haikujengwa. Sasa msije mkaendelea kutupa ngulai tukawa na matumaini mnatenga, mwisho wa siku hakuna utekelezaji; hili ni jambo la hatari sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2005 Mzee wangu kipenzi, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu, wakati anaomba kura kwa watu wa Mtwara aliwaahidi kuwajengea barabara hii kwa kiwango cha lami. Mwaka 2010 karudi tena akawaahidi kuwajengea barabara hii kwa kiwango cha lami, lakini hata Rais mpendwa sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli alipokuja Jimboni kwangu Tandahimba ameahidi kujenga kilometa zote 210 kwa kiwango cha lami. Leo mmekuja mmetenga kilometa 50, kwenye pesa mliyotengea ni shilingi bilioni 20. Mimi sijui kama kuna u-serious kweli wa kuijenga hii barabara yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hii ndiyo barabara ambayo nimeizungumzia; Wilaya yangu ya Tandahimba, Wilaya ya Newala, Mtwara Mjini, Vijijini ndio wazalishaji wakubwa wa zao la korosho. Hebu leo jiulize Mheshimiwa Waziri kutoka Mtwara Mjini kwenda Tandahimba Jimboni kwangu ni kilometa 95, lakini unatembea kwa saa saba kutoka Mtwara Mjini. Yaani ukitoka Mtwara kwenda Dar es Salam utafika mapema Dar es Salaam kuliko Mtwara kwenda Jimboni kwangu Tandahimba. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, hii pesa mliyoiweka basi muwe na nia ya dhati kabisa ya kuona barabara hii mnaanza kuijenga angalau kwa kilometa hizo mlizozitaja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Barabara ya Ulinzi ipo pale na barabara hii ni muhimu sana. Jambo ambalo nataka nikukumbushe Mheshimiwa Waziri, mwezi wa 12 wakati wananchi wa Jimbo la Tandahimba wamekwama Mto Ruvuma askari wetu walitumia boti kwenda Tandahimba kwa saa 12, lakini walipofika Tandahimba walishindwa kwenda hata barabara ya Ulinzi haipitiki. Mwisho wa siku wale watu wa Tandahimba wameokolewa na boti la kutoka Msumbuji, hii ni aibu kwa Taifa letu. Nione sasa Wizara yako inajipanga vizuri kuziona barabara zile za Mtwara mnazifanyia mambo mazuri sana. Mkumbuke kwamba Mkoa wa Mtwara ulisahaulika kwa kuona kwamba sehemu ile ni sehemu ambayo mlikuwa mmewaweka watu waliokuwa wanapigania uhuru. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo watu wameshapata uhuru tayari, mkishinda washaurini na watu wa Msumbiji wawaongezeeni pesa kwa sababu mliwaweka Mtwara ili mtuwekee lami watu wa Mtwara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Bandari ya Mtwara. Bandari hii ni fursa kubwa kwa uchumi wa Mtwara na kwa Taifa hili la Tanzania. Kama leo Bandari ya Mtwara ingekuwa inafanya kazi vizuri hata leo msingesafirisha maroli haya ya GSM mnapakia saruji kutoka Mtwara kuleta Dar es Salaam kwa gharama kubwa. Leo Bandari ya Mtwara ingekuwa inafanya vizuri watu wa Mtwara wangefanya biashara kubwa na watu wa Comoro ambao wana njaa, na sisi ni wakulima wazuri tu. Bandari ya Mtwara ingekuwa imewezeshwa vizuri leo watu wa Zanzibar tungekuwa tunapata fursa ya kukimbia kwenda Zanzibar, lakini ingekuwa ni fursa ya biashara baina ya nchi hizi za Malawi ambazo hawana bandari na wanatumia gharama kubwa sana kusafirisha mizigo yao kwenda sehemu nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mmetenga pesa ya kujenga gati moja, lakini wakati tunasoma Mpango tulizungumza suala la magati manne. Niwaombe hata hako kagati kamoja mlikokasema basi tuone sasa kanajengwa kweli, badala ya blah blah ambazo haziwanufaishi Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona bajeti ya suala la uwanja wa ndege wa Mtwara na nimeona mmetenga fungu pale, lakini jambo ambalo nataka nikukumbushe bajeti ya mwaka uliopita mlitenga shilingi milioni 500, sijui ile shilingi milioni 500 imekwenda wapi? Sasa watu wa Mtwara tusije tukaendelea kudanganywa. Niombe Serikali hii ina nia njema, na mimi naamini Waziri una nia njema, wakati ukiwa Wizara ya Mawasiliano ulifanya mambo mengi mazuri, nione haya uliyoyaandika unayafanya kweli ili tuone maendeleo ya nchi hii ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye jambo hili la nyumba za Serikali. Hili ni jambo la ajabu na ni la hatari sana, wenzangu walizungumza. Wenzangu wamezungumza hapa, na haya mambo msipochukulia serious wazee wangu wenye kumbukumbu za dhati mtaikumbuka miaka ya 1970, nchi ya Kenya Rais akiwa Mzee Jomo Kenyatta, alifanya mambo kama tunayofanya kwenye Taifa hili la Tanzania. Uuzaji wa nyumba hizi yalifanywa Kenya kwenye ardhi ya Wakenya leo mwanae anakuja kukiri mapungufu ya miaka ya 1970 iliyopita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, isomeni sheria ile mliyoiandaa wenyewe. Ukisoma Sheria ile ya Executive Agency Act namba 30 ya mwaka 1997 iko wazi, mmeipa TBA mamlaka kubwa ya kuuza, kujenga upya, kukarabati na kugawa zile nyumba zenye class A, B na C, lakini mkiangalia kwenye mambo haya ya TBA kama mtafuatilia mtaona namna wenyewe mlivyofanya na mnahusika, wenyewe mnajijua, sio jambo la siri hili. Wazee wangu mpo muda mrefu mnajua kwenye mambo yale. Sasa hizi ni pesa za Watanzania ambazo zinatumiwa kwa maslahi ya watu wachache. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tena nikuombe Mheshimiwa Waziri, suala hili la TBA uwe serious, ndani yake ukisoma magazeti yale ya zamani wapo watu wazito wa Taifa hili wanajua mambo haya. Wameingilia mamlaka ya TBA bila sababu za msingi. Tuone sasa mnakuwa serious kwa ajili ya Watanzania na muone Taifa hili la Tanzania ni la watu wote, wala tusikae hapa kwa ajili ya mambo ya vyama kama watu wa CUF, wa CHADEMA, wa CCM wanazungumza jambo kwa interest ya Taifa hili, tuwaunge mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, isionekane tu Upinzani unapoleta hoja hamuwi serious na hoja ya Upinzani, na Wapinzani pia CCM wakileta hoja tusione hoja zao si za msingi, kwa ajili ya Taifa hili ni lazima tuzungumze lugha moja, tuizungumze Tanzania moja, tuone Watanzania wananufaika na rasilimali zao badala ya kukaa hapa tunapiga ngonjera tu. Watu wanasimama hapa wanapiga mangonjera tu, mnataja majina ya viongozi waliopita, fanyeni kazi sasa huu ndio wakati wa kufanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikwambie Mheshimiwa Waziri naumia sana, binafsi niseme na ni-declare interest. Pande hizi za CCM, CUF, CHADEMA nani mnakaa mnakuja hapa mnawataja viongozi waliopita. Andaeni mikakati yenu kama hi mliyoileta leo, tekelezeni ya kwenu achaneni na kuzungumza mambo yaliyopita, kama mnashindwa kuchunguza fanyeni hayo mnayoyakusudia sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana na niendelee kukuomba sana; barabara hii ya kutoka Mtwara kwenda Tandahimba kama kuna sehemu kwa kudokoadokoa hebu waone Wamakonde hawa. Zamani mlikuwa mnasema Wamakonde sio watu, sisi ni watu tena majabali kweli kweli! mtuone kwamba, tupo kwenye Taifa hili. Ahsante sana.