Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue pia nafasi hii kukushukuru kunipa nafasi ili niweze kuhitimisha hoja ambayo tumekuwa nayo toka asubuhi. Lakini nikushukuru sana kwa usimamizi wa Bunge lako hili Tukufu; lakini pia nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia hoja hii toka asubuhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge ambao wamechangia hoja hii ni 22 kwa sababu ni wengi siwezi kuwataja kwa majina; lakini hawa wamechangia kwa kuzungumza lakini pia wapo waliochangia kwa maandishi Wabunge watatu; pia nitambue mchangiaji na hotuba ya Mwenyekiti wangu wa Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji wamechangia kwa sehemu kubwa sana juu ya bajeti yetu hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu muda ni mchache nadhani nitatumia muda huu kufafanua hoja chache tu kwa sababu ya muda. Na hoja nyingi ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge tutazijibu kwa maandishi lakini nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Wabunge ambao wamechangia kwa maandishi au kwa kuzungumza kwa sababu yote waliyoyazungumza ni masuala yaliyokuwa yanalenga kutuelekeza, kutushauri lakini kutoa mapendekezo ambayo yakifanyiwa kazi yamkini kazi yetu ya mwaka wa fedha ujao 2022/2023 ikawa kazi njema na ikaendelea kuwasaidia watanzania na ikaendelea kuleta tija kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa nchi yetu, mama Samia Suluhu Hassan kwa kutuongezea bajeti lakini pia kwa kujali sana sekta hizi za uzalishaji kwa sababu safari hii sekta za uzalishaji karibu zote zimeongezewa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo, nianze sasa kujibu hoja moja moja kwa kifupi lakini kama nilivyosema tutajibu kwa maandishi kwa kueleweka vizuri na Wabunge wote ambao hoja zao wamezitoa zitajibiwa vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja ya Mheshimiwa Mariam Ditopile kuwawezesha wavuvi wadogo, limekwisha kusemwa na Mheshimiwa Naibu Waziri, tutafanya hivyo. Tuna mpango wa kuwapa boti 320 tena zaidi lakini boti hizi zitakuwa ni special sana; zitakuwa na GPS, Fish hold, vifaa vya ubaridi, Fish finder, hizi boti zinauwezo wa kubeba tani 1.5.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri hebu rudia; boti ngapi?

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni boti 320.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tunza umeisikia hiyo? Haya endelea bwana. (Makofi/Vicheko)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kupitia TAFIRI tumefanya utafiti kutambua maeneo yanayofaa kwa uvuvi na program tunaikamilisha ili kutumia kitu kinaitwa lango la simu ili kuwezesha wavuvi kupata taarifa za maeneo ya uvuvi moja kwa moja kwenye simu zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mariam pia alikuwa ana hofu juu ya upungufu wa samaki kwenye viwanda vyetu. Kupungua kwa rasilimali za uvuvi katika Ziwa Viktoria, hususan samaki aina ya sangara, kunatokana na sababu mbalimbali na suala kubwa kabisa lililosababisha mojawapo ni uvuvi haramu. Sasa alitaka kujua mkakati wetu wa kudhibiti uvuvi haramu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli, kuanzia mwaka uliopita umekuwa ule wa kushirikisha wadau wote wa uvuvi. Ni kweli tumefanya kazi kubwa kupitia operations tulizozifanya, lakini kufanya operations peke yake tuligundua kwamba haitoshi, tukaona ni vizuri tushirikishe wadau wote kuanzia wavuvi wote wanaovua kwenye maziwa na kwenye bahari, lakini pia kuzishirikisha Serikali zetu za Mitaa, Halmashauri zetu pamoja na Serikali za Mikoa zihusike moja kwa moja kwenye masuala haya ya kudhibiti uvuvi haramu, kwa sababu Serikali ni moja. Haiwezi kuwa ni Serikali inayotoka Dodoma kwenda kudhibiti uvuvi haramu kule Bunda au Rorya ni mbali sana wakati kuna Serikali pia kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mkakati wetu ulikuwa ni huo wa kufanya zoezi hili liwe shirikishi, Serikali nzima ihusike, pia wadau wote wahusike ili tuweze kudhibiti uvuvi haramu kwenye nchi hii. Tunajua wote samaki ni rasilimali inayomsaidia kila Mtanzania. Samaki hawa wakitusaidia leo tu kesho wasitusaidie ni bahati mbaya sana maana kesho watakuwepo watoto wetu, wajukuu zetu, na wanadamu wengine watakuwepo, sasa watakuta nini kama hatushirikiani kwa pamoja kudhibiti rasilimali hizi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendelea kutoa elimu, pia tumeendelea kufanya maboresho ya kanuni zetu ili tuweze kudhibiti sawasawa suala hili, tumeendelea pia kutoa elimu ya uvuvi endelevu kwa jamii za wavuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda ambavyo vimefungwa siyo lazima sana kwamba vilifungwa kwa sababu, sangara hawapo. Vingine vimefungwa kwa sababu ya management, matatizo ya ki-management, vingine kwa sababu ya matatizo ya uendeshaji, na kadhalika. Si sawa sana kusema viwanda vimefungwa kwa sababu, sangara walikuwa kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, biashara ya dagaa kwenye Ziwa Tanganyika. Mheshimiwa Naibu Waziri ameieleza vizuri sina sababu ya kuirudia, lakini nieleze labda kuhusiana na kuongeza thamani ya dagaa na kupunguza upotevu wa mazao ya dagaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika Ziwa Viktoria, Serikali kupitia mradi au kupitia pesa za mkopo wa masharti nafuu ambazo tumezitangaza leo asubuhi sisi kupewa pia, tumetenga fedha kwa ajili ya kununua mitambo ya ukaushaji wa mazao ya uvuvi kwa kila Mkoa ili kuongeza thamani na kupunguza upotevu wa mazao. Kwa ukanda wa bahari Mheshimiwa Naibu Waziri ameeleza namna ambavyo mradi wetu wa IFAD bado upo, tunazo zaidi ya Bilioni Thelathini na Sita kwa ajili ya kazi hiyo kwa upande wa ukanda wa bahari wote. Kwa hiyo, tutafanya kazi hii kwa upande wa dagaa ili kusudi tuweze kupunguza upotevu wa mazao ya samaki, hususan dagaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na suala la leseni za Bahari Kuu kuwa ni kubwa. Suala hili lilianzishwa na Mheshimiwa Simai. Kwa mujibu wa Kanuni ya Usimamizi na Uendelezaji wa Uvuvi wa Bahari Kuu ya mwaka 2021 bei za leseni za uvuvi wa bahari kuu kwa meli za Kitanzania zilipunguzwa kati ya asilimia 70 hadi asilimia 86 ikilinganishwa na bei za leseni kwa meli za kigeni. Mfano, uvuvi wa mishipi ni Dola 8,000 tu kwa mwaka kwa wazawa, ikilinganishwa na dola 50,000 kwa wageni. Kwa hiyo, utaona zimepunguzwa kwa sehemu kubwa sana hizi bei za leseni ambazo Mheshimiwa Mbunge alikuwa akizitaja.

Mheshimiwa Naibu Spika, juu ya suala la mwani imeelezwa vizuri na Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini kulikuwa na suala lililosemwa na Kamati kuhusu biashara ya mwani inakua kwa kasi na inatekelezwa na wanawake, Wizara iandae mpango wa kuwaelimisha na kuwawezesha wakulima wa mwani mbinu bora za kilimo hicho. Sasa Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa mwaka wa 2021/2022 tumetoa mafunzo ya uzalishaji na uhifadhi wa zao la mwani kwa wakulima 4,569 katika Mikoa ya Tanga, Lindi na Mtwara, pia Wizara tumewezesha wakulima wa mwani katika Mikoa ya Tanga na Lindi kwa kuwapatia kamba zenye thamani ya shilingi milioni 20. Mwaka wa 2022/2023 Wizara tutaendelea kuhamasisha na kuwawezesha wakulima 2,000 ili waweze kutumia teknolojia bora za uzalishaji na uongezaji thamani wa zao la mwani katika Mikoa ya pwani. Vilevile kujenga vichanja 10 vya kukaushia mwani katika Halmashauri za Wilaya za Mtwara, Lindi, Lindi DC, Lindi MC, Kilwa, Mkuranga, Mafia, Bagamoyo, Pangani, Tanga, Mkinga na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu muda wangu unakimbia sana niende nigusie pia masuala machache yanayohusiana na mifugo. Kulikuwa na suala la udhibiti wa magonjwa ya mifugo ambalo Mheshimiwa Kenneth Nollo alilisema. Kwa mwaka wa 2021/2022 Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi, sekta ya mifugo tumejenga majosho 192, na ninadhani kwenye taarifa yetu yapo, kwa gharama ya Shilingi 3,458,000,000 katika Halmashauri 45 kwenye Vijiji vyenye mifugo mingi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa 2022/2023 Wizara tutajenga tena majosho mengine 406 yenye thamani ya shilingi 7,304,441,000 yakiwemo majosho 128 kwa gharama ya shilingi 2,304,441,000 kwa fedha za ndani na majosho 278 kwa kiasi cha shilingi 5,000,000,000 fedha za nje, majosho haya yatajengwa katika maeneo ya malisho kwa lengo la kupunguza magonjwa yaenezwayo na kupe. Kwa hiyo, kazi hii tunaendelea kuifanya na kwa mwaka huu unaokuja tutaifanya kwa sehemu kubwa sana. Waheshimiwa Wabunge kila mmoja angehitaji majosho mahali ambapo kuna ng’ombe kwenye Jimbo lake, nadhani safari hii tutajitahidi angalao kila Mbunge kupata josho moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na suala la ufugaji wa punda na kufungwa kwa kiwanda cha punda kule Shinyanga. Mheshimiwa Khadija Aboud alisema Serikali ihamasishe kufanya kazi hiyo. Kwa kifupi ni kwamba, nchi nyingi duniani zimepiga marufuku biashara hii ya nyama ya punda. Zimepiga marufuku kwa sababu ya uzalianaji wa punda, punda wanazaliana kwa nadra sana. Punda anaweza kuchukua miaka mitatu ili aweze kuzaa na baada ya kuzaa hapo anaweza akachukua miaka mingine sita au zaidi ili aweze kuzaa. Kwa hiyo, punda hawaongezeki kama ng’ombe wanavyoongezeka au kama wanyama wengine wanavyozaliana. Kwa hiyo, bila kuwa na tahadhari tunapowatumia kama kitoweo basi wanaweza wakatoweka kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, punda wanatumika pia kwa shughuli nyingine za uzalishaji. Siyo nyama tu na ngozi na vitu vingine, wanatumika pia kwa njia za uzalishaji. Kulikuwa na suala lingine la ufugaji katika ranch za Taifa. Hili suala limezungumzwa sana, lakini kwa uzito sana limezungumzwa na Mheshimiwa Mwijage, Mheshimiwa Dkt. Kikoyo na Waheshimiwa wengine wamelizungumza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niseme pengine kwamba Kampuni yetu ya Ranchi za Taifa - NARCO inamiliki ranchi 14 na inazitumia. Inawezekana isiwe kwa uwezo wake uliopo, lakini nadhani ni vizuri tungeenda taratibu kwenye suala hili kwa sababu Serikali imeweka maeneo hayo kama buffer areas ili wakati Serikali itahitaji ardhi kwa jambo mahsusi ambalo linahusu maslahi ya nchi yetu inaweza wakati wowote ikaenda kwenye ranch. Sasa tukisema ranch hizi zipo tu halafu sasa tuzitumie kama tutakavyotaka, mimi naamini tunaweza kuonekana kama hatujatumia vizuri rasilimali hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya Ranch ya Mwisa na Kagoma, Mheshimiwa Dkt. Kikoyo na Mheshimiwa Mwijage nimewasikia na hoja yenu nimeichukua, lakini pia Mheshimiwa Mwijage alihitimisha vizuri sana baada ya kusema Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Wizara ya Mifugo, Wizara ya Ardhi, tukutane chini ya Waziri Mkuu ili tuweze kulizungumza suala hili. Nami naunga mkono hoja hiyo kwamba ni vizuri tuzungumze suala hili na mamlaka za nchi ili tuone tunalimalizaje, kwa sababu tukiendelea kuzungumza NARCO pamoja na Waheshimiwa Wabunge wawakilishi wa wananchi, tunaweza tusifikie muafaka ambao utakuwa mzuri sana kwa sababu ninaposikia Mheshimiwa Dkt. Kikoyo anasema hata Ranch ya Mwisa na Kagoma hazipo kwa mujibu wa sheria, basi nadhani linakuwa suala zito kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nadhani tutakutana ili tuweze kuzungumza, nami naamini tutafikia muafaka sawasawa, tutafikia muafaka mzuri ili kwamba rasilimali hizi ranch, pia wananchi wetu na wenyewe wakae kwa amani, wakae kwa starehe kwenye hayo maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja ya Kamati ya Bunge kutokana na umuhimu wa vitalu katika kuzalisha mifugo bora zoezi la kupanga vitalu lizingatie manufaa ya kufuga kisasa badala ya kuchunga. Tunauchukua ushauri huo na mimi wakati wote nimekuwa nikikutana na wafugaji na kuwaeleza kwamba, ndugu zangu lazima tuanze sasa kufikiria kufuga badala ya kuchunga. Kwa sababu, tumechunga miaka yote hii, lakini tija bado haijaonekana kwetu wafugaji wenyewe, pia hata kwa Taifa lenyewe. Sasa tunayo haja ya kufanya mabadiliko, kuna haja ya kuboresha ili tuingie kwenye kufuga mifugo. Wafugaji wetu siyo wagumu sana ndiyo maana kwenye hotuba yangu, kama mmesoma vizuri, hii mliyokuwa mnanisikiliza hapa ni summary lakini hotuba ndefu ilikuwa kwenye vishkwambi vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mmenisoma vizuri nimesema kwa mwaka huu wa fedha 2022/2023 nitaanza kampeni kwa kukutana na wafugaji, hawa ambao tunawaita ni wachungaji, tuelimishane juu ya kufuga kwa tija, tuelimishane juu ya kufuga kibiashara, tuelimishane ni kwa namna gani tunaweza kutumia rasilimali hizi za mifugo zikanufaisha familia na zikanufaisha Taifa letu. Kwa hiyo, tutafanya kampeni kubwa, pia zaidi ya kampeni tutatumia viongozi walioko ngazi kuanzia ya Kijiji mpaka ngazi ya Mkoa ili tuweze kuelewana, mbali na hivyo tutaendelea pia kutenga maeneo ili kwamba, tuwe sasa na maeneo maalum ya kufugia mifugo yetu ikiwa ni pamoja na wafugaji wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu suala hili linataka kuachwa kwa Serikali kana kwamba, Serikali ina ardhi kibao imelala mahali, sasa ikipungua itaenda ichukue impe mtu aende aweze kufuga, Hapana! Wafugaji pia tuna ardhi na maeneo ambayo mifugo yetu ipo, maeneo hayo tunaweza kuanza kuyaboresha, tukiondoka hapo ndiyo tuende kwenye maeneo ya wazi. Na maeneo haya ya wazi pia yako chini ya Halmashauri. Tumezungumza na Halmashauri nao wayaboreshe, siyo kuyaacha kama yalivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli ziko Halmashauri nyingi ambazo zimetenga maeneo kwa ajili ya malisho, lakini bado maeneo hayo hayajaboreshwa, hayana miundombinu stahiki inayotakiwa, majosho, maji, na kadhalika. Sasa tuchukue hatua sisi wote wadau kwenye suala hili la mifugo, kuanzia wafugaji wenyewe. Ndiyo maana tunasema lazima tuanze sasa utaratibu wa kupanda malisho, suala la malisho haliepukiki kutokana na mabadiliko ya tabia ya nchi, lakini kutokana na tunavyoongezeka Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, binadamu tunapoongezeka shughuli zetu za kiuchumi zinaongezeka pia. Sasa zinapoongezeka lazima ardhi itapungua ile ambayo utachunga huria, sasa lazima tuanze kufikiria kuwa na mashamba ya malisho yanayomilikiwa na wafugaji wenyewe. Ndiyo maana kwenye mashamba yale 100 ambayo tutayaanzisha ambayo tumeita ni mashamba darasa, haya mashamba tutayakabidhi kwa mfugaji mmoja-mmoja na baadaye tutatathmini ni mfugaji yupi anaelekea kwenye kufuga kiuendelevu. Badala ya kuyaweka kwenye taasisi za Serikali tutawapa wafugaji na hawa wafugaji ndiko wafugaji wengine watakwenda kujifunza namna ya kulima na kutunza hayo mashamba ya malisho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, masuala ni mengi, huduma za ugani, Mheshimiwa Nollo pia anasema Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo ni vya zamani. Nakubaliana na wazo hilo ni kweli…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa bado una dakika mbili.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ooh, nakushukuru sana. Ahsante sana kwa kunipa muda, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.