Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Mifugo na Uvuvi kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa ustawi wa jamii na maendeleo endelevu, na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulingana na Sensa ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ya mwaka wa kilimo 2019/2020 inaonesha kuwa idadi ya ng’ombe ilikuwa milioni 35.3; kati ya hao, wakulima wadogo walikuwa na ng’ombe milioni 35.1 na mashamba makubwa yalikuwa na ng’ombe 142,968. Aidha, wakulima wadogo walikuwa na mbuzi milioni 25.5 na mashamba makubwa mbuzi 33,847. Kwa upande wa kondoo wakulima wadogo walikuwa na kondoo milioni 8.8 na mashamba makubwa kondoo 24,075.

Vilevile nguruwe waliofugwa na wakulima wadogo walikuwa milioni 3.2 na mashamba makubwa yalikuwa na nguruwe milioni 3.4 na kulikuwa na jumla ya kuku milioni 92.8 ambapo wakulima wadogo walikuwa na kuku milioni 80.1 na mashamba makubwa yalikuwa na kuku milioni 12.7. Pamoja na idadi hiyo kubwa ya mifugo, mchango wa sekta ya mifugo na uvuvi wa asilimia saba bado ipo chini sana na tija ikiboreshwa kuna fursa kubwa ya sekta hii kuchangia sehemu kubwa ya pato la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Tanzania kuwa nafasi ya tatu kwa nchi za Bara la Afrika na kuchangia katika uchumi wa Taifa, sekta hii ya mifugo na uvuvi inazalishwa kwa tija ndogo. Katika hali hii, sekta ya mifugo haijamsaidia mfugaji na mvuvi kwa kiasi kikubwa kunajinasua kwenye umaskini na kimeendelea kutoa mchango mdogo kwenye pato la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ichukue hatua zaidi ili kuboresha sekta ya mifugo na uvuvi ikiwemo ujenzi wa mabwawa, kuwezesha mashamba ya kuzalisha lishe/chakula cha mifugo, kuwezesha sekta binafsi kuzalisha mitamba ya kisasa na vifaranga wa samaki. Napendekeza Serikali ianzishe vitalu vya mifugo katika Kata ya Mjele na Mshewe, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, ikiwemo kuchimba mabwawa na visima. Pia napendekeza kuwezesha kuanzisha mashamba makubwa ya kuzalisha lishe ya mifugo ikiwemo ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Serikali imalizie kujenga kiwanda cha nyama cha Utengule (Mji Mdogo wa Mbalizi) ambacho kwa muda mrefu ujenzi umesimama pamoja na kuwepo vifaa vyote muhimu vilivyotolewa na wafadhili. Kutokana na kuwepo uwanja wa Kimataifa wa Songwe ambao ni wa kimkakati kusafirisha mazao ya kilimo na mifugo kwa masoko ya nje, napendekeza umaliziaji wa kiwanda hiki cha nyama na pia uwezeshaji wa vitalu vya kunenepesha mifugo katika Kata za Mjele na Mshewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iongeze Maafisa Ugani, waliopo kwenye Halmashauri ya Mbeya ni wachache na wale waliopo hawaonekani kutoa huduma za ugani kwa wananchi. Wizara iweke msukumo wa kuhamasisha, kuanzisha na kutoa elimu kuhusu kilimo cha malisho ili kuwezesha malisho kutosheleza mifugo mwaka mzima. Pia Serikali iongeze kasi ya uzalishaji wa mitamba kutokana na idadi ndogo ya ng’ombe wazazi kwenye mashamba ya Serikali na matumizi madogo ya teknolojia ya uhimilishaji kwa kutumia mbegu bora za mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuwepo na mkakati wa kuongeza mazao ya uvuvi ili kuwezesha samaki wapatikane kwa tija kuwezesha ushindania kwa soko la nje. Vijana wenye nia thabiti na wanaopenda kujishughulisha na ujasiriamali wa ufugaji samaki kwenye mabwawa watambuliwe na uwekwe utaratibu maalum wa uwezeshaji kupitia Halmashauri zao kupata mitaji na utaalam wa kufuga samaki kwenye vizimba na mabwawa na hivyo kuweza kujiajiri wenyewe na kujipatia kipato.

Aidha, Serikali ishughulikie changamoto ya chakula cha samaki na uhaba wa vifaranga hapa nchini. Vijengwe vitotoleshi vingi katika vituo vya ukuzaji viumbe maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.