Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. JUMAA H. AWESO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwanza kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia hotuba iliyokuwepo mbele yetu. Lakini pia niungane na Mbunge wa Muheza kuhusu malalamiko yetu na masikitiko yetu kwa Wizara hii kwa namna mkoa wetu ulivyosahaulika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapata uchungu leo kuona baadhi ya maeneo ya wenzetu yanatekelezewa miradi mbalimbali lakini sisi Mkoa wetu wa Tanga tunasahaulika. Leo tunaona wenzetu wanashangilia wanakaa safu za mbele lakini sisi mkoa wetu wa Tanga tunawekwa katika jiko kazi yetu kusugua masufuria na sisi Mkoa wetu lazima atutizame kwa jicho la huruma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wa Tanga tumekuwa watu wa kupembuliwa tu. Ukiangalia bandari tunapembuliwa, ukiangalia sijui nini tunapembuliwa hivi sisi ni lini tutatekelezewa miradi yetu ya maendeleo? Kwani tumemkosea nini Mwenyezi Mungu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumza haya kwa masikitiko makubwa kwa kuwa kila kukicha sisi tumekuwa watu wa kupewa ahadi tu. Wali ni mtamu sana kwa maini lakini ukikaa sana unakuwa kiporo na kiporo kikaa sana kinachacha na kikichacha kinaumiza tumbo, leo wananchi wa Tanga tunaumizwa kutokana na kutotelekelezwa miradi mbalimbali, inakuwa kazi ya kusuasua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine nataka nizungumzie kwa masikitiko makubwa barabara yetu ya Pangani – Tanga – Saadani. Barabara hii mimi tangu sijazaliwa, nimezaliwa, nimesoma msingi, sekondari mpaka Chuo Kikuu leo nimefika na mimi nimekuwa Mbunge lakini barabara yetu tumekuwa watu wa ahadi tu. Amekuja Mheshimiwa Rished miaka 15 tunaambiwa itajengwa, Mheshimiwa Pamba akaambiwa ipo kwenye upembuzi, mimi leo naambiwa pia barabara yetu African Development Bank wameonyesha nia sasa hii nia inaisha lini ili barabara hii sasa itengenezwe? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Pangani tupo pangoni, tuna fursa nyingi katika Wilaya yetu ya Pangani, leo tuna Mbuga Saadani ambayo ni kichocheo kikubwa cha kiutalii, ni mbuga pekee katika Afrika ambayo imeungana na bahari. Barabara hii ya Tanga - Pangani ndiyo inaunganisha na Mkoa wa Tanga na nchi jirani ya Kenya, tukijenga barabara Tanga - Pangani - Saadani tutaweza kuinua sekta ya utalii katika Wilaya ya Pangani na Mkoa wa Tanga. Lakini kwa kuwa tuna mahusiano vizuri na Zanzibar na Mombasa, Kenya ina maana tutainua sekta ya utalii katika Wilaya ya Pangani, lakini pia tutaweza kunyanyua sekta mbalimbali za kiutalii, uvuvi na kilimo kutokana na barabara hii ya Tanga - Pangani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sina maneno mengi sana ya kusema, ila nilikuwa namwomba Waziri katika majumuisho yake atuambie amejipanga vipi kuhakikisha kwamba atatutekelezea barabara hii ya Tanga - Pangani, Bandari ya Tanga pamoja na reli ya kutoka Tanga - Arusha na Musoma ili tuchangie katika pato la Tanzania.