Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Mifugo na Uvuvi Ndugu Mashimba Ndaki, Naibu wake Ndugu Abdalah Ulega, wataalamu wa Wizara na wadau wa sekta hizi kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kilimanjaro una fursa nyingi za kufuga aina mbalimbali za wanyama kama vile ng’ombe na mbuzi wa maziwa na nyama, kondoo, nguruwe, sungura, kuku, bata na samaki kwa kutumia rasilimali zilizopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ya mlimani (Kilimanjaro) yanaweza kutumika kwa ufugaji wa ndani (zero grazing) kwa ng’ombe wachache na mbuzi wa maziwa, nguruwe, sungura, kuku na bata.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la ukanda wa tambarare kwenye Kata za Arusha Chini na Mabogini lina wafugaji wa Kimasai na lina uwezekano wa kuzalisha kwa tija ng’ombe, mbuzi na kondoo wa nyama.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na juhudi za wafugaji wa Jimbo la Moshi Vijijini, aina za kienyeji za wanyama (ng’ombe, mbuzi, nguruwe na kuku) wanaofugwa ni kikwazo kikubwa kwenye maendeleo ya sekta ya mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ya uvuvi inaweza kuwapatia wananchi wa Jimbo la Moshi Vijijini kipato kikubwa iwapo itaendelezwa. Hili litawezekana ikiwa wananchi watapatiwa mafunzo ya kitaalamu ya jinsi ya kufuga na kukuza samaki kwa kutumia teknolojia ya mabwawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ufugaji endelevu wa samaki unaweza kutatua changamoto za umaskini kwa kuwaongezea kipato na kuchangia kikamilifu kwenye pato la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata ya Arusha Chini kwenye Bwawa la Nyumba ya Mungu, wavuvi wanaweza kusaidiwa na Maafisa Ugani wa uvuvi mbinu bora za ufugaji wa samaki, ikiwepo matumizi ya vizimba. Uwekezaji wa vizimba unaweza kufanyiwa majaribio kwenye Bwawa la Nyumba ya Mungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kufanikisha ufugaji wa ng’ombe, mbuzi wa maziwa na nyama, kondoo, nguruwe, sungura, kuku, bata na samaki katika Jimbo la Moshi Vijijini, ninaishauri Wizara itusaidie yafuatayo:-

Kwanza, naishauri Serikali kwa kushirikiana na wadau wa mifugo na uvuvi wafanye utafiti na kuangalia changamoto na fursa zilizopo katika Jimbo la Moshi Vijijini ili wajue pa kusaidia.

Pili, naishauri Serikali ipeleke wataalamu wa mifugo kutoa mafunzo ya ufugaji bora wa mifugo ya kimkakati yenye tija katika Jimbo la Moshi vijijini.

Tatu, naishauri Serikali iwe na programu maalumu ya kuzalisha mitamba wa maziwa wenye sifa zinazohitajika ikiwa ni pamoja na mifugo mingine kama mbuzi wa maziwa, ng’ombe wa nyama, nguruwe na kuku. Wafugaji wengi katika Jimbo la Moshi Vijijini hawana mbegu bora za ng’ombe wa maziwa. Kwa ujumla huwa wanabahatisha.

Nne, naishauri Serikali ihamasishe kuanzishwa kwa vikundi vya ushirika wa wafugaji mifugo na samaki katika Jimbo la Moshi Vijijini ambavyo itakuwa rahisi kuwapatia huduma za mitaji na utaalamu.

Tano, naishauri Serikali itupatie wataalamu wa kuchimba mabwawa katika Jimbo la Moshi Vijijini.

Sita, naishauri Serikali ianzishe Kituo cha Kanda cha kuzalisha vifaranga wa samaki jimboni kwangu ili wafugaji wavipate kwa urahisi kama vile vilivyopo kwenye Mikoa ya Morogoro, Tabora, Ruvuma, Lindi, Tanga na Geita.

Saba, naishauri Serikali iwezeshe wazalishaji vifaranga binafsi katika Jimbo la Moshi Vijijini ili wasaidie juhudi za Serikali kwenye kukuza hii sekta.

Nane, naishauri Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri ya Moshi, wawezeshe kupandikiza vifaranga bora vya samaki katika Bwawa la Nyumba ya Mungu, kwani wavuvi waliniambia kwenye kampeni kuwa samaki wamehama ikiwa na maana kuwa wamepungua. Hii ni pamoja na kuanzisha uvuvi wa vizimba.

Tisa, naishauri Serikali iwe na huduma za uhakika za ugani katika Jimbo la Moshi Vijijini ikizingatia lishe ya samaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumi, napendekeza Serikali ifanye majaribio ya kutumia vizimba kwenye Bwawa la Nyumba ya Mungu ili kuongeza tija kwenye ufugaji wa samaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naishauri Serikali iwekeze kwenye kuanzisha mashamba darasa ya ufugaji bora wa mifugo ya kimkakati na samaki jimboni kwangu Moshi Vijijini ili wajifunze kwa vitendo kama ilivyowasilishwa kwenye hotuba ya bajeti yam waka 2022/2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.