Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kuungana na viongozi wenzangu wote kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia baraka zake. Aidha, nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, viongozi wote na watendaji wote Serikalini kwa jinsi walivyosimamia utekelezaji wa Ilani ya CCM yam waka 2020 – 2025; hongereni sana na Mwenyezi Mungu awabariki sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kutoa mchango wangu kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii muhimu sana kwa mustakabali wa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tunaiomba sana Serikali iiongezee bajeti ya Wizara hii kwani kuna mahitaji makubwa sana ya rasilimali watu, miundombinu, vitendea kazi na mahitaji makubwa ya kukabiliana na majanga ya ukame, magonjwa na upungufu wa maeneo ya malisho.

Pili, kwa kuwa sekta hii ya mifugo imekuwa na mchago mkubwa katika pato la Taifa na wafugaji wanakabiliwa sana na maeneo ya malisho ni wakati muafaka kwa Taifa letu kusimamia mkakati wa kubadilisha koo za mifugo kwani hatua hii itawafanya wafugaji kuwa na mifugo wachache na watakaohimilika kutunzwa, kuhudumiwa na kuongeza mapato kwa mfugaji na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kuondoa upungufu wa Maafisa Ugani Serikali iangalie utaratibu wa kuwaajiri na kuwapanga kulingana na wingi wa mafugo na kuwapangia majukumu ya kila siku kwenye vituo vya mafunzo kila kata na kijiji badala ya wao kutafutwa na wafugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo wengi wao hupenda kupangwa kwenye Makao Makuu ya Halmashauri hata kama wako wachache badala ya tarafa, kata na kijiji, hali inayowafanya mchango wao wa kitaalamu kutokuonesha matokeo makuu kwa Serikali na wafugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa minada yetu tunaishauri Serikali iweke mizani ya kupima mifugo kwani hakuna uhalisia wa pande zote mbili (muuzaji na mnunuzi) hivyo basi hapo ni lazima matumizi ya vipimo vitumike kuleta uhalisia kwa kuanza na minada mikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa sekta ya uvuvi Serikali itoe waraka wa maelekezo ya usimamizi kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya kwa kuwatumia Maafisa Maliasili wa ngazi hizo katika kuzuia uvuvi haramu kwenye mabwawa na maziwa madogo kwani hakuna Maafisa Uvuvi wa kutosha na athari ni nyingi sana kutokana na uvuvi unaoendelea huko kwenye maziwa hayo kwa mfano Ziwa Tlawi Mbulu na Ziwa Babati na Basutu Hanang.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.