Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Awali ya yote nawapongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa jitihada wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo ninalozungumzia zaidi ni eneo la Ziwa Tanganyika hasa kwenye Sekta ya Uvuvi. Ziwa Tanganyika ni ziwa ambalo lina kina kirefu na wavuvi ambao wanavua kwenye eneo la Ziwa Tanganyika wanavua uvuvi wa kubahatisha. Naiomba sana Serikali ielekeze nguvu kuwasaidia hawa wavuvi kwa kuwapelekea zana za kisasa ili waweze kujikwamua katika shughuli zao za kiuchumi, bila hivyo hawawezi kabisa kujikwamua. Kwa sababu eneo la Ziwa Tanganyika ni eneo ambalo mvuvi anaweza akakaa hata mwezi mzima asipate mazao ya uvuvi kutokana na kina kirefu kilichopo Ziwa Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo napenda kuiomba Serikali, punguzeni tozo kwa wavuvi. Eneo hili linawakwamisha sana wavuvi. Unakuta mvuvi mmoja analipia leseni ya mtumbwi, analipia leseni yake kama mvuvi, analipia leseni ya wavu na analipia leseni ya umiliki wa chombo. Kwa hiyo, mtu mmoja analipa leseni karibu nne. Naiomba sana Serikali ikae iangalie jinsi gani ya kuwasaidia hawa wavuvi kupunguza zile kero ili wavuvi waweze kujikwamua katika shughuli zao? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri alifanya ziara kwenye eneo la Jimbo langu. Amefika eneo la Ikola; ule mwalo ulishamezwa, nilimwomba awajengee mwalo kwenye Kata ya Karema ili wavuvi hawa wanaovua kwenye Ziwa Tanganyika, eneo la Kata ya Karema wapate sehemu ya kuhifadhi mazao yao. Naomba sana hili alifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine kwenye Sekta ya Uvuvi ni eneo la mazalia ya samaki. Eneo hili ni muhimu sana kwa Wizara ili itenge maeneo muhimu ndani ya Ziwa Tanganyika ambayo yatasaidia sana kuwa na mazalia ya samaki ambayo yatakuwa endelevu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni uthibiti wa nyavu haramu zinatokea nchi jirani ya Burundi. Zile nyavu za filamu ni mbaya sana ambazo kipande cha nyavu kikakatikia kwenye ziwa kinaendelea kuua samaki na vizalia vyote vilivyoko kwenye ziwa. Naomba hili mlifanyie kazi ili wavuvi wawe na uvuvi endelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie Sekta ya Mifugo. Tunamwomba Waziri aje na mpango mkakati wa kuboresha ranchi za Taifa ili ziweze kuwasaidia wafugaji wakubwa na wadogo. Pia tunamwomba aje kutujengea majosho kama alivyokuwa ameahidi alipokuwa amekuja kwenye ziara kwenye Jimbo langu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa hizo dakika tano…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)