Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii ili nami jioni hii ya leo niweze kutoa mchango wangu wa maoni katika Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, kwa upande wangu binafsi, kipekee kabisa lazima niishukuru Wizara na Uongozi wa Wizara kwa maana kile ambacho nilikiwasilisha mwaka 2021, karibu asilimia 66 kimechukuliwa na Wizara na kufanyiwa kazi. Naishukuru sana Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upekee kabisa niishukuru na niipongeze Serikali ambapo mwaka 2021 wakati nachangia Hotuba ya Bajeti ya Wizara hii, nilishauri kwamba katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo, lengo la Serikali la kujenga Bandari za Uvuvi, Kilwa Masoko ifikiriwe na iwekewe kipaumbele kwa sababu kuna kina cha asili. Nashukuru Wizara imepokea hili na limefanyia kazi na mpango huu sasa unakwenda kutekelezwa. Pongezi sana kwa Rais Samia, Serikali ya Awamu ya Sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, nini rai yangu katika mpango huu wa Bandari ya Uvuvi ambayo inakwenda kuanza kujengwa mwishoni mwa mwezi huu kama ambavyo Hotuba ya Mheshimiwa Waziri imeelezea katika ukurasa wa 104, kwamba ameshapatikana Mkandarasi ambaye ni China Harbour Engineering Co. Limited, na mchakato wa kuanza ujenzi unaanza mwisho wa mwezi huu wa Tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu nini katika hili? Moja, ni kwamba wakati tunajenga bandari hii, ilikuwa ni finyu kwa mahitaji ya wakati huo na kwa maana hiyo sasa hivi inakwenda kupanuliwa. Kwa maana hiyo, pembezoni mwa eneo la bandari na gati kuna miundombinu mingine ikiwemo makazi pamoja na nyumba nyingine kwa matumizi mbalimbali. Tafsiri yake ni kwamba kunahitajika kulipia fidia kwa waliokuwa wanahusika na maeneo haya. Naomba Wizara ikahakikishe inalipa fidia kwa wakati ili kuepukana na migogoro tunapokwenda kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati kama hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu ya pili katika eneo hilo, bandari hii inakwenda kufungua fursa nyingi sana ikiwa ni pamoja na viwanda vya kuchakata samaki pamoja na mazao mengine ya bahari. Naomba na nitoe rai sana kwa Wizara, viwanda hivi visiende kutengenezwa au kujengwa kilomita 100 kutoka maeneo ya uzalishaji. Itakuwa ni jambo la ajabu, na la kituko, na la kuongeza gharama zisizo na sababu. Sisi Kilwa tuna ardhi ya kutosha ya kuweza kupanua viwanda hivi vya kuchakata, kusindika, mazao ya bahari pamoja na samaki kwa sababu uzalishaji utakuwa mzuri kwa kuwa bandari iko pale pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu nyingine, tunapozungumzia bandari ya uvuvi, tafsiri yake ni kwamba tunakwenda sasa kunasibisha pamoja na masuala mengine yanayoendana na uwepo wa bandari ya uvuvi ikiwemo Chuo cha Uvuvi. Tunapozungumza, tuna chuo chetu kikubwa maarufu cha uvuvi Mbegani, pia kuna chuo kingine kidogo cha Mtwara Mikindani. Kwa fursa hii ya uwepo wa Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko, naomba Chuo cha Uvuvi kijengwe Kilwa Masoko na eneo la kutosha tunalo.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho katika rai yangu kwenye eneo hili la bandari, litaendana na uwepo wa miundombinu mingine rafiki kwa ajili ya kuwezesha bandari yetu sasa ifanye kazi vizuri. Hapa sasa nakusudia kuzungumza kwa Kimatumbi, maana yake tunahitaji access roads to the port. Kwa maana hiyo sasa, barabara tuliyonayo ya kilomita karibu 30 kutoka bandarini Kilwa Masoko mpaka Nangurukuru ilikuwa ya viwango vya wakati huo kwa matumizi ya kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, ihakikishe kwamba kilomita 30 hizi za kutoka Bandari Kilwa Masoko mpaka Nangurukuru, zinakuwa katika viwango kwa ajili ya matumizi bandari kubwa ya uvuvi. (Makofi)

Mheshmiwa Naibu Spika, baada ya eneo hilo la bandari ya uvuvi, niendelee kukumbusha rai ambayo niliitoa mwaka 2021 wakati nachangia Wizara hii, kwamba kutokana na uzalishaji mkubwa wa samaki Kilwa, hususan Kilwa Kivinje, tunahitaji soko la samaki pale Kilwa Kivinje. Bahati mbaya sana katika mapitio ya mpango wa bajeti hii inayoishia Juni, sijaona utekelezaji wala mipango.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba na nikumbushe kwamba Soko la Samaki pale Kilwa Kivinje ni muhimu. Kama macho yangu hayakupitia vizuri wakati napitia bajeti na randama, basi Waziri atakapokuja kufanya sum-up aelezee hilo kwamba tuna mpango gani sasa wa kujenga Soko la Samaki pale Kilwa Kivinje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe takwimu; hatuzungumzi kwa ajili tu ya kupendelea kwa sababu Kilwa Kivinje tunahitaji Soko la Samaki, hapana, Mkoa wa Lindi peke yake, wavuvi ni zaidi 6,000. Katika wavuvi zaidi ya 6,000 wa Mkoa mzima wa Lindi, wavuvi zaidi ya 5,000 wanapatikana Wilaya ya Kilwa. Ndiyo maana tukasema ni fursa ya kutengeneza Soko la Samaki Kilwa Kivinje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo, nije sasa katika Sera, Sheria na Kanuni kama ambavyo Hotuba ya Mheshimiwa Waziri imeelezea ukurasa wa 109 mpaka 110. Kwenye eneo hili, nashukuru hatua za awali zimeanza. Mwaka 2021 wengi tulichangia sekta hii ya uvuvi na tulikuwa tukilalamikia mabadiliko ya Kanuni za uvuvi za mwaka 2020, ndiyo kilio kikubwa cha wavuvi wetu. Masuala ya makatazo ya uvuvi wa usiku, makatazo ya ring net na mambo mengine mengi ambayo tuliyajadili, ni kwa sababu ya mabadiliko ya kanuni ya mwaka 2020. Hapa mmesema mnakwenda kubadilisha Kanuni za Mwaka 2009, hazikuwa na matatizo makubwa sana, matatizo makubwa yalijitokeza kwenye mabadiliko au marekebisho ya Kanuni hizi za mwaka 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upekee wa mwaka 2021 nilitoa kifungu ambacho ndiyo kimeleta changamoto zote hizi. Naomba nirudie hapa, hiki ni Kifungu cha 66 au Kanuni ya 66 ya mabadiliko ya Kanuni za Uvuvi za Mwaka 2020, Kanuni ndogo ya kwanza na kifungu dada (d) na Kifungu gaga (g), vikaangaliwe kwa umakini. Mmeitisha wadau wa uvuvi, mmeitisha Kamati ya kupitia mapendekezo yenu, Kamati ya Sheria Ndogo; nilitamani sana sisi ambao tunaotoka kwenye sekta za uvuvi tungealikwa ili tutoe hizi inputs ambazo sisi ndio wadau husika, tunajua taratibu za uvuvi. Kama mtaitisha tena Kamati ya kupitia, kwa maana ya Kamati ya Sheria Ndogo, nitoe rai sana, sisi tunaotoka kwenye sekta za uvuvi tualikwe tukatoe maoni yetu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa, ni kengele ya pili. Ahsante.

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, muda umeisha! Basi mengine nitachangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)