Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu. Pili, nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi pamoja na Naibu wake kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakiendelea kuifanya pamoja na changamoto mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa unyenyekevu kabisa, kwanza nawashukuru sana kwa josho ambalo walitupa la kule Iringa, limekamilika na soko ambalo limejengwa pale Mbambabay nalo limekamilika. Nawashukuru sana. Siyo kawaida kwa Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi kuweza kufanya kazi kubwa kama hiyo, kwa sababu tulizoea kuwasikia tu katika masuala ya kukamatakamata nyavu na nini, lakini sasa naona mnaenda kuwezesha hawa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na fedha ambayo imetolewa mwaka huu 2022 katika bajeti yao, lakini bado tunaona kwamba Wizara hii inastahili kuongezewa bajeti ikizingatiwa kwamba asilimia kubwa ya wananchi wanaishi katika miambao ya maziwa yetu ambayo ni makuu matatu, Ziwa Rukwa na pia ukanda wa bahari. Watu hao mara nyingi ukifuatilia, kwa kweli wengi wao bado ni masikini. Kwa hiyo, wanahitaji kuwezeshwa zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nililoongelea kuhusu suala la soko, lile soko inawezekana lisikidhi matumizi yake kutokana na wananchi wa maeneo yale ya mwambao wa Ziwa Nyasa, ambapo urefu wa ule mwambao ni takribani kilomita 150, lakini zana zao za kuvulia ziko duni sana. Mara nyingi nimekuwa nikiomba kwamba kwa nini hao vijana wasiwezeshwe hasa kupata injini za boti kwa mkopo, siyo bure? Ninachopingana nacho ni jambo moja tu la kuwalazimisha kukaa kwenye vikundi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye masuala ya uvuvi kuna watu wana tabia ya kuwa na mazao ya aina tofauti tofauti. Kuna siku mtu anaweza akaamka akasema mimi leo Hapana, siendi ziwani. Leo sitaingia kwenye maji, na kwa hali ya Ziwa Nyasa linahitaji sana kuwa na chombo ambacho ni madhubuti. Sasa kwa misingi hiyo, akipewa mkopo huyo kijana ambaye amethubu, bado hawezi kuvua peke yake, atakuwa anashirikiana na wenzake. Kwa maana hiyo, ajira nyingi zitatengenezwa na wakati huo tutaweza kupata mazao yanayotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi sana kunatokea vifo kutokana na mitumbwi duni wanayoitumia ambayo haina injini za boti. Kwa hiyo, naomba sana, kwa unyenyekevu kabisa, katika mwambao wa Ziwa Nyasa kwa kweli hawajapewa zana za kutosha hasa hizo injini za boti. Nimekuwa nikizungumza mara kwa mara, hata ukisikiliza leo katika maelezo ya bajeti hii, mambo mengi yaliyozungumza mazuri, yako kwenye ukanda wa bahari, yako angalau kule Ziwa Victoria, lakini haya maziwa mawili; Tanganyika na Nyasa ni kidogo sana, yaani yanatajwa tu kiujanjaujanja fulani hivi. Huoni kamili kwamba kuna mradi gani madhubuti unaopelekwa huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, msitake tuwe tunaanza sasa kusema kwa nini unapeleka huko? Kwa nini unapeleka huko? Hii ni nchi moja, na kama ni nchi moja itendewe haki. Haiwezekani bajeti kubwa katika hiyo mliyopewa yote inaenda upande mmoja au sehemu chache wengine wanabakia kuwa masikini. Ukizungumzia sijui mambo gani, huko huko. Hata kaka yangu Mheshimiwa Katani pale, alifikia kusema hivyo akaonywa, lakini bado tunasema ndiyo ukweli. Kwa nini maeneo mengine hayaangaliwi inavyotakiwa? Yanapewa fedha kidogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hayo mliyosema sijui kujenga vizimba sijui vitu gani, ukiuliza vizimba vingapi vinaenda Ziwa Tanganyika au Ziwa Nyasa utakuta pengine ni sawa na hakuna. Ndugu zangu hii nchi ni moja, na pengine maeneo hayo ndiyo yanapiga kura nyingi kuliko hata maeneo mengine. Kwa nini mnatufanyia hivyo? Naomba safari hii kwa kweli nisikie kinagaubaga katika hizo injini za boti zitakuwepo, na zitapelekwa kiasi gani katika upande wa Ziwa Nyasa?

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, niseme tu kwamba vilevile tumezungumzia juu ya kuwawezesha vijana kupata ajira zao, kwa sababu sio wote wanapitia mpaka elimu ya masomo ya juu, lakini hakuna mitaala ile ambayo inaweza ikaelimisha watu kwa vitendo kujua kwamba watajifundisha kuvua au kutengeneza zana mbalimbali kama boti na wakapata vyeti. Unakuta watu kama hao hawatambuliki, kumbe watu siku hizi wanapenda kutembea na vyeti. Ni namna gani Wizara yenu itaunganika na Wizara ya Elimu katika huu mchakato unaoendelea wa kutoa mafunzo kwa vijana hasa wale ambao hawajamaliza masomo yao yaani wale dropouts, wanaweza wakajikita katika maeneo hayo, kwa sababu wao wanapenda kwenda katika masuala ya kiuvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tumeona katika Wizara ya Kilimo wanapima afya ya udongo. Ninyi Wizara ya Mifugo na Uvuvi, hasa kwenye uvuvi mnapima vipi afya ya ziwa kujua kwamba eneo hili lina samaki wengi na eneo hili halina samaki wengi? Ninyi mnatumia mbinu gani kuwaelimisha wananchi ili wajue kwamba eneo fulani usiwe unaenda, nenda eneo fulani ambalo mara nyingi utapata samaki na kuna mazalio, labda muepuke kuvua hapo, vueni hapa ili mradi wapate faida inayokusudiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama wenzenu wanapiga hatua katika maeneo yao na ninyi vilevile sasa mtusaidie kuweza kuona kwamba mtu asiwe anatembea usiku kucha anavua, usiku kucha anaparaza mtumbwi, anahangaika kutafuta Samaki, mpaka inafika asubuhi hajapata hata samaki mmoja, kumbe amepigananao chenga humo humo kwenye ziwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi kwenye suala la mifugo. Wilaya ya Nyasa hasa maeneo ya mwambao kuna changamoto kubwa sana ya ugonjwa wa mapafu ya ng’ombe. Hawana ng’ombe wengi sana, lakini huyo huyo mmoja au watatu walionao ni muhimu sana kwao. Sasa unakuta mara nyingi utaambiwa ng’ombe alipochinjwa alikuwa na konokono; anaumwa sijui konokono; wanaita konokono, lakini hakuna tiba zinazoeleweka kabisa kwamba kukitokea tatizo fulani wanaenda mahali fulani.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata zile ruzuku zinazotolewa kwa ajili ya ng’ombe, kule sijui kama hata zinafika. Nimefuatilia, hakuna ruzuku iliyofika siku za karibuni, na zile dawa ni ghali, nyingine zinafika mpaka Shilingi 35,000/=, wakati mwingine wanamtibu ng’ombe kwa madawa chungu mbovu, yaani ni ile tu kukisia sasa tumtibu kwa magonjwa ambayo wanahisi ndiyo yatakuwa yenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, wataalam wa mifugo pia ni wachache sana katika Wilaya ya Nyasa. Kwa hiyo, naomba kuiangalia wilaya hiyo ili kuiwezesha sasa kuweza kupata wataalam watakaoweza kusaidia katika maeneo hayo ya mifugo hususan katika ng’ombe na mbuzi vilevile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijamalizia ya kwangu, nisije nikasahau, nilikutana pia na viongozi wa Chama cha Wavuvi pale Canteen, wamenipa maelezo yao, naomba niwakabidhi na yenyewe, mtayapitia kadiri walivyoandika wao wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba, vilevile kuna kuwezesha vijana katika masuala ya mabwawa ya samaki hasa Ukanda wa Juu katika Tarafa ya Mpepo, yaani Kata ya Kingerikiti, Mipotopoto, Luhangarasi, Tingi na Lumeme; tuseme kata nane za Tarafa ya Mpepo. Naomba wawezeshwe kwa sababu hao wangependa sana kufuga Samaki. Nilileta barua kwako Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo, naamini katika bajeti hii utakuwa pia nao umewakumbuka ili waweze kupata kitoweo na pia afya njema kutokana na samaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kimsingi tunaona Wizara hii ikijitahidi kwenda lakini bado tunasisitiza umuhimu wa wavuvi na watu wa mifugo kupewa fedha ya kutosha ili nao waweze kufanya kazi zao vizuri.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante, kengele ya pili hiyo.

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)