Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Mimi nianze kutambua kazi nzuri inayofanywa na Wizara ya Ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikipiga kelele sana Daraja la Munguri B, leo kwenye bajeti nimeona imetengwa shilingi milioni 600 na mwaka jana ilitengewa fedha za kufanya usanifu wa kina. Ninachoomba tu kwenye eneo hilo kwa sababu daraja hilo linategemewa na wananchi wetu wengi kabla mvua hazijanyesha daraja hilo lijengwe ili wananchi wetu sasa waanze kufanya biashara bila usumbufu, kwani wananchi wa Kondoa na wananchi wa Hanang tuna muingiliano mkubwa sana wa kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwa kawaida wananchi wetu wakienda kwenye mnada wa Mbicha, mnada wa Mitiyangi, wanalala kulekule mvua zikinyesha. Ninachoomba sana kabla mvua hazijanyesha daraja hilo liwe limejengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nishukuru kwamba kwenye barabara ya Katesh – Hydom ambayo iko kwenye Ilani, barabara hii iliahidiwa toka mwaka 2010, leo nimeona shilingi milioni 280 imewekwa hapo, ila ni ya muda mrefu, shilingi milioni 280 imewekwa kwa ajili ya kufanya usanifu wa kina. Tumezoea hapa kwamba, usanifu wa kina unaweza ukafanyika wakati huo huo unajenga. Barabara hiyo inategemewa na wananchi wa Hanang katika usafirishaji wa mazao mbalimbali kama ngano; Hanang imechaguliwa kuwa kitovu cha uzalishaji wa ngano, mashamba mengi yako ukanda wa juu yanategemea barabara hii, wananchi wa Basutu, wanaozunguka Ziwa Basutu, wanalima sana vitunguu. Vitunguu hivi vinasafirishwa maeneo mbalimbali mpaka nje ya nchi, wanaitegemea hii barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Mlima Chavda, kila siku mizigo inamwagwa pale, nguvu ya mwananchi amehangaika shambani kwa shida, sehemu kubwa inaangukia pale Chavda. Wakati mnafanya usanifu wa kina ninaomba eneo lile litengenezwe kwa dharura. Tumeshaongea na Naibu Waziri, Waziri nimekudokeza, Makatibu Wakuu mara tatu nimeongea nao kuangalia hili eneo kwa sababu linatukwamisha. Mara zote napambana na Engineer wa Mkoa angalia kokote kule hili eneo ulitengeneze. Ninachoomba wakati mnafanya usanifu wa kina eneo la Mlima Chavda muanze kulijenga kwenye bajeti ya mwaka huu. Muongezeeni Meneja wa Mkoa fedha kwenye eneo la matengenezo ili aweze kutengeneza eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza sana Meneja wetu wa Mkoa Engineer Bashiru anafanya kazi nzuri. Wakati wa mvua barabara zote zilifunga tukampigia kelele, baada ya muda mvua ilivyokatika barabara zote akazinyosha. Anafanya kazi nzuri naomba muwezesheni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niombe; tunayo barabara inayotoka Hirbado – Basodesh – Seche mpaka Bashnet, barabara hii tuipandishe hadhi iwe chini ya TARURA ili itengenezwe vizuri hali yake ni mbaya sana. Wananchi wakiangalia barabara hii upande wa Singida, ukitoka pale Hirbado kuna Kijiji cha Singa, kuanzia Singa ukienda Mtinku - Ilongero – Singida barabara iko TANROADS na inatengenezwa vizuri, lakini ukija upande huu wa Manyara kuanzia Bashnet – Dareda barabara iko chini ya TANROADS inapitika vizuri, wananchi hapa katikati wanasema sisi wa nchi gani? Kama upande wa Singida iko TANROADS, upande wa Bashnet – Dareda iko TANROADS, kwa nini kipande hiki kisiunganishwe barabara yote ikawa chini ya TANROADS ili itengenezwe vizuri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna muujiza, Wilaya ya Hanang yenye kata 33, vijiji 96 tunatenga fedha ndogo tunayopewa upande wa TARURA ika-cover barabara hizo zote. Hiyo barabara ipandishwe ili itengenezeke vizuri iweze kuwasaidia wananchi kwenye shughuli zao za kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini uwanja wetu wa ndege wa Mkoa wa Manyara. Mkoa wa Manyara ni kitovu cha utalii, mama amepiga Royal Tour kutangaza utalii wetu, ili sisi tunufaike na utalii lazima uwanja ule utengenezwe ili wananchi waweze kufanya shughuli mbalimbali zinazounganika na utalii ambao tumeutangaza sana kupitia Mama Samia Suluhu Hassan. Mama ameupiga mwingi basi na ninyi upande wa uwanja muupige mwingi ili tuendane. Tarangire pale tunakosa wageni kwa sababu usafiri ni mgumu, Lake Manyara tunakosa wageni kwa sababu usafiri changamoto, mtu mpaka atue KIA ndio anakuja mpaka Lake Manyara, safari ni ndefu. Tufungue ile corridor ya utalii, Mlima Hanang, vivutio kibao, lakini namna ya kufika. Tukifungua ule uwanja utatusadia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie kidogo upande wa bei ya usafiri wa anga nchini kwetu. Watu wanajitetea sana kwamba base yetu ya wasafiri ni chache, watu wanaotumia usafiri wa ndege ni wachache, lazima tuje na mkakati wa kuwahamasisha ili watu watumie usafiri wa ndege ili kurahisisha usafirishaji nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda nchi mbalimbali umbali uleule ambao unalipa shilingi laki nne kwa wenzetu laki moja. Fanyeni tathmini ya kina kama ni kodi zimezidi angalieni namna ya kurahisisha upande wa kodi tuangalie sehemu gani gharama zetu zinakuwa kubwa ili hatimaye tuweze kusaidia usafirishaji kwa sabahu kusafiri kwa basi unatumia saa nyingi unapoteza muda mwingi, ukichukua ndege saa chache umefika unafanya shughuli zako, unafanya shughuli nyingi kwa wakati, ndani ya siku moja unaweza kufanya shughuli nyingi. Bila kuboresha sehemu ya usafiri hatutaweza kufanya kitu cha maana. Hilo eneo tuliangalie, tusitafute excuses za kwamba, base ya wasafiri ni ndogo, hiyo haitoshelezi. Tutumie vichwa vyetu tuweze kutanzua eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nitambue kazi kubwa sana inayofanyika na Serikali yetu. Miundombinu mbalimbali inayotengenezwa ni kazi kubwa, lakini kama wenzangu walivyochangia lazima twende kimkakati, maeneo yale ambayo yanatufungua kiuchumi tuyatazame kwa kina. Nimeongelea barabara ya Katesh – Hydom, tumesema kilimo cha ngano, ile iwe ndio center ya kuzalisha ngano. Tuna nakisi ya ngano zaidi ya tani milioni moja, tujielekeze huko. Maeneo ambako vitunguu vingi vinalimwa tunasafirisha maeneo mbalimbali tujielekeze huko ili tufungamanishe sekta hizi za miundombinu na sekta ya uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa kampeni tuliwaambia wananchi kwamba, miundombinu ya barabara ni sawasawa na mishipa ya damu. Mshipa wa damu ukiziba hautakuwa na amani, utatafuta daktari popote ili uweze kupata matibabu uweze kurudi kwenye hali ya uzalishaji kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miundombinu ndio hivyo hivyo, ukiangalia maeneo ambayo barabara imefunguliwa, imewekwa lami maendeleo yanaenda kwa kasi, lakini miundombinu hakuna, hakuna maendeleo. Huwezi kumvutia mwekezaji yoyote ili akawekeze kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya mimi niseme naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)