Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu. Naendelea kusema na nitatizidi kusema Wizara hii ni muhimu sana na ukiangalia michango mingi ya Wabunge utaona kuwa suala la barabara ni janga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara limekuwa ni janga na ndiyo maana unaona kila Mbunge anayesimama hapa anazungumzia kwa habari ya barabara kwenye eneo lake kwa sababu hali ya barabara kwenye maeneo tunayotoka kiuhalisia hairidhishi, hali ni mbaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nitaanza kwa kuzungumzia barabara ya kutoka Mloo kwenda Chitete mpaka Kamsamba na niombe Wizara iangalie barabara hii kwa jicho la pili, kwa sababu barabara hii kwanza ina mchango mkubwa kwa uchumi wa Mkoa wa Songwe, lakini ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ya Mloo - Chitete kwenda Kamsamba inatumiwa na wakulima wengi sana na wavuvi ambao wanatoka huko Kamsamba na maeneo mengine. Sasa hatuwezi kusema barabara hii haina mchango katika pato la Taifa letu. Hebu tuona Wizara iangalie barabara hii kwa umuhimu wake kwa sababu barabara hii imekuwa na changamoto kubwa, wananchi wanapata shida kweli kweli lakini wakati huo wanachangia kwa asilimia kubwa katika pato la Taifa letu. Tuombe Wizara iangalie barabara hii kwa umuhimu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naomba kuzungumzia kwa suala la Mji wa Tunduma. Sisi sote tunajua kwamba Mji wa Tunduma ni lango kuu, ni mji ambao upo mpakani kwanza, lakini ni lango kuu la SADC. Nchi nyingi zinatumia mpaka huu wa Tunduma na ukiangalia asilimia 70 mizigo inayoshushwa katika bandari yetu inakwenda kupitia katika Mji wa Tunduma. Lakini kumekuwa kuna changamoto kubwa sana ya barabara kutokana na ule mrundikano wa magari makubwa wananchi wetu wamekuwa wakikutana na adha kubwa sana, jambo ambalo kwanza linawacheleweshea katika masuala ya uchumi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa umuhimu wa barabara hii hebu tuombe, wizara ione umuhimu na ilichukulie jambo hili kwa dharura kuhakikisha inafanya upanuzi wa haraka wa barabara ili kuweza kuwanusuru wananchi wa Mji wa Tunduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi mmoja uliopita kulikuwa kuna maandamano na mgomo wa madereva wa magari makubwa ambao wanavuka katika huu mpaka wa Tunduma, jambo ambalo liliwapelekea wananchi wa Mji wa Tunduma kupata adha kubwa sana. Hebu fikiria mwananchi anatoka Tunduma kwenda kupata huduma ya kiafya kwenye Hospitali ya Mkoa anachukua siku tatu kufika Vwawa, hili ni jambo la ajabu sana. Hebu tuombe Wizara ichukulie jambo hili kwa dharura na barabara hii iweze kupanuliwa kwa udharura wake kwa sababu tunajua sisi sote mpaka huu namna gani ambavyo unachangia katika pato la Taifa letu. Hebu tuombe jambo hili wizara ilichukulie jambo hili kwa udharura.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili ambalo nataka kuishauri Wizara, niombe Wizara ione umuhimu wa kujenga bandari kavu ndani ya Mji wa Tunduma. Kwa sababu sisi sote tunajua ili kurahisisha huduma kwa nchi jirani ambazo zinapata huduma katika mpaka wa Tunduma, Wizara ione umuhimu wa kujenga bandari kavu ndani ya Mji wa Tunduma ili tuweze kuepuka changamoto zingine ambazo hazina ulazima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la kibajeti katika Wizara hii ya Ujenzi hasa katika bajeti ya barabara. Kwa mwaka huu wa fedha katika miradi ya maendeleo ya barabara kiasi ambacho kilikuwa kimetengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ya barabara ni shilingi trilioni 1.588. Lakini kiasi ambacho kilikuwa kimetolewa ni shilingi trilioni 1.093; fedha hizi hakuna fedha yoyote iliyoelekezwa katika miradi ambayo tuliipangia ndani ya Bunge hili. Hakuna fedha yoyote iliyokwenda kutekeleza mradi hata mmoja, badala yake fedha hizi zimekwenda kulipa madeni ya nyuma na kilio cha barabara kimebaki palepale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana leo hii ukiona kila Mbunge anainuka na kulia kwa habari ya barabara kwenye eneo lake kwa sababu katika bajeti tuliyokuwa tumepitisha hakuna mradi wowote uliotekelezwa hili ni ajabu sana. Leo hii msione Wabunge wanataka kuruka sarakasi mezani wana uchungu ni namna ya kuhakikisha ujumbe wao unafika na Wizara hii iweze kuwaelewa. Tunafanya mambo gani, ikiwa tunapoteza muda tunakaa ndani ya Bunge hili, tunachangia tunashauri kwa habari ya barabara katika maeneo yetu, tunaelezea changamoto zilizopo huko kwenye maeneo yetu na barabara nyingi zinagusa uchumi wa Taifa letu, halafu tunatenga bajeti, bajeti inakwenda kulipa madeni yote, ni jambo la ajabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kukaa kupoteza muda kwenye Bunge hili tukiwa tunajadili bajeti ya kulipa madeni ya nyuma, haiwezekani. Hebu tuombe Wizara inavyotuletea bajeti zake humu wawe wanatuambia katika kiasi cha maendeleo tunachotenga ni kiasi gani kitakwenda kulipa madeni na kiasi gani kitakwenda kutekeleza miradi ya maendeleo ili tutoke tukiwa wamoja. Nje na hapo hatuwezi kueleweka kwa wananchi wetu kwa sababu mwisho wa siku wananchi wetu hawawezi kutuelewa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naomba nizungumzie suala la wakandarasi; kuna hasara kubwa ambayo tunaipata Serikali imekuwa ikiingia hasara ya shilingi 2,900,000,000 kila mwaka na hasara hii inatokana na wazabuni kucheleweshewa kulipwa fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii fedha tunayoisema leo hii kama naweza kuzungumzia barabara ya Mloo – Chitete kwenda Kamsamba hivi hii fedha si ingeweza kutusaidia hata watu wa Mkoa wa Songwe jamani. Fedha hii ingeweza kutusaidia, lakini wewe fikiria kila mwaka Serikali inaingia hasara ya shilingi bilioni 2.9; hii haikai sawa. Hebu tuombe Wizara hii ijitahidi ikae na iangalie ni namna gani inayakwepa haya hatuwezi kila siku tukawa tunapiga kelele tunapigia haya haya. Mwaka jana nimesema hapa hasara ambazo tunazipata kutokana na kuchelewesha malipo ya wakandarasi, lakini leo hii bado tunaingia kwenye Bunge hili tunajadili haya haya mambo hii haikai sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna uhitaji mkubwa sana kwenye maeneo yetu wananchi huko hawatuelewi kwa sababu hali ni mbaya na kodi wanatoa hii haikai sawa. Hebu tuombe Wizara iangalie namna bora ya kutatua hizi changamoto ili tutoke tukiwa wamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ahsante. (Makofi)