Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa ili na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii. Kwanza kabisa nimshukuru sana Mwenyezi Mungu aliyenipa fursa ya kuwepo hai na kutoa mchango wangu leo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uimara, uhakika na usalama wa miundombinu ni muhimu sana kwenye jamii yetu, na tafiti mbalimbali zimeonesha mahusiano ya moja kwa moja kati ya uimara, ubora na uhakika wa miundombinu na maendeleo ya jamii inayohusika.

Ninatambua suala la miundombinu ni mchakato ili iweze kuwa imara nakwenye nchi yetu kwa ujumla tumejitahidi kwa kiasi kikubwa na ndiyo maana nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya kuhakikisha kwamba miundombinu yetu inakuwa imara, lakini nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri na Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara hii kwa kweli kazi kubwa wanaendelea kuifanya pamoja na changamoto kadhaa ambazo bado zipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utakuwa kwenye maeneo mawili; eneo la kwanza ni suala la vivuko; Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi Ibara ya 57 inatoa maelekezo kwa Serikali kuimarisha miundombinu hasa barabara na vivuko na ukisoma ukurasa wa 84 Ilani inaelekeza si kwa bahati mbaya, kwa makusudi kwamba Serikali ihakikishe pamoja na maeneo mengine yote lakini eneo la Ukerewe, Kivuko cha Bukondo kwenda Bwiro kitengenezwe, kivuko cha kutoka Murutanga kwenda Irugwa kitengenezwe, kivuko cha kutoka Ghana kwenda Kakukuru kitengenezwe pamoja na vingine kikiwemo cha Kisorya kwenda Lugezi.

Niipongeze Serikali, nimpongeze Mheshimiwa Waziri angalau kwenye bajeti hii nilisikiliza hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, lakini nimepitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameonesha dhamira ya Serikali kukamilisha matengenezo ya kivuko cha kutoka Bukondo kwenda Bwiro, lakini vilevile kivuko cha kutoka Kisorya kwenda Lugezi, ni jambo jema sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizi bado kuna umuhimu mkubwa wa kuhakikisha kwamba hivi vivuko vingine hasa cha kutoka Kakukuru kwenda Ghana na kutoka Murutanga kwenda Irungwa vina kamilika ili viweze kutoa huduma kwa wananchi wetu. Ukiongolea mazingira na maisha ya visiwa inawezekana watu wengine wasiweze kuelewa, lakini yanachangamoto nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kusema hapa mwaka 2017 nikataadharisha bahati mbaya mwaka 2018 tukio likatokea, lakini bado niendelee kutaadharisha ni muhimu sana mazingira ya visiwani yachukuliwe kwa uzito mkubwa na suala la vivuko lipewe umuhimu mkubwa. Juzi hapa kulikuwa na matatizo ya usafiri baada ya mafuta kupanda, boti hii ya kutumia engine yenye uwezo wa kuchukua abiria 50 mpaka 40 wanachukua abiria mpaka 80 kitu ambacho kinaatarisha maisha yao.

Kwa hiyo ni muhimu sana Serikali ika-intervene ikahakikisha kwamba vivuko hivi vinakuwepo ili kuweza kusafirisha wananchi wakaweza kusafirisha katika mazingira yaliyosalama, lakini nimeona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameongelea dhamira ya Serikali kukamilisha majengo ya abiria ya kusubiria. Ni jambo jema sana lakini niombe sana abiria wanataabika sana kwenye maeneo yale, kasi iongezeke ili majengo haya ya abiria kusubiria yaweze kukamilika haraka. Jengo kwa mfano la Bugolola, Jengo la Ukara, Bukimwi pale lakini hata Kisorya ni muhimu sana wakati wa mvua wakati wa jua wananchi wanataabika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka nizungumzie ni juu ya ujenzi wa barabara. Barabara inayojengwa sasa ya kutoka Bunda kuja Bulamba mpaka Kisorya na kimsingi inatakiwa kwenda mpaka Nansio inajengwa kwa lots tatu, lots mbili zile sasa moja imekwishakamilika kilometa 51 lakini inayojengwa sasa ni kutoka Bulamba kwenda Bunda sawa imekamilika kwa asilimia takribani 30 ni jambo jema, lakini barabara hii ili kukamilika inatakiwa ijumuishe vilevile lot ya tatu inayotoka Kisorya kwenda Nansio.

Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yako sijaona unaongelea chochote juu ya eneo hili ambalo linajumuisha barabara na kilometa 14 za kutoka Lugezi kwenda Nansio. Kilometa hizi utakumbuka Hayati Dkt. Magufuli wakati ule akiwa Rais alivyokuja Nansio alitoa maelekezo eneo hili lijengwe kwa haraka kutokana na umuhimu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile Mheshimiwa Waziri Mkuu alivyokuja pale Nansio vilevile akatoa maelekezo kwamba kama ilivyoahidiwa mwanzo itekelezwe kwa haraka, lakini sijaona unaongelea chochote juu ya eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna barabara nyingine vilevile ambayo Mheshimiwa Waziri nimeteta na wewe mara kadhaa, Mheshimiwa Naibu nimeteta na wewe, lakini mama yangu Katibu Mkuu tumezungumza wote vilevile, nikawaambieni kuna barabara hii ya kutoka Bukongu kwenda Bukonyo mpaka Masonga, lakini vilevile kuna barabara ya Bukongo kwenda Rubya ambayo kuna msitu mkubwa sana mpaka Bukonyo ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa wananchi wa Ukerewe. Nikawaomba kwamba sawa tunatenga nimeona hata katika bajeti hii imetengwa shilingi milioni 100 kwa ajili ya matengenezo ya kawaida hayatusaidii sana haya kwa sababu barabara ile kwa nature yake inamatatizo makubwa na kwa nature ya udongo wa Ukerewe hatuwezi kupata kifusi cha uhakika cha kuweza kutengeneza barabara ile kwa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikaomba basi tutengeneze barabara hii hata kama ni kwa awamu, lakini angalau tuwe na uhakika wa ubora wa barabara ile na kwa sababu inapitisha magari mengi sana kwenda kwenye lango la uchumi wa wananchi wa Ukerewe mtusaidie angalau tuweze kuijenga kwa awamu iweze kukamilika kusaidia kuimarisha uchumi wa waanchi wa Ukerewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado niwaombe sana Mheshimiwa Waziri zingatieni ushauri wangu, lichukueni hili mtusaidie na bahati njema sana kuna kilometa takribani 10 zishafanyiwa upembuzi na usanifu wa kina mtusaidie muweze kuijenga barabara hii iweze kusaidia kuimarisha uchumi wa wananchi wa Ukerewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wetu pale Ukerewe lango lake ni kutoka kwenye eneo la Kakukuru ambako barabara hii inaenda, niwaombe sana Mheshimiwa Waziri mtusaidie barabara hii iweze kujengwa na mtakuwa mmeimarisha uchumi wa wananchi wa Ukerewe ambao sehemu kubwa inategemea mazao ya ziwa, kwa hiyo niombe sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la mwisho, nimeona kwenye hotuba yako kupitia TEMESA mna mpango wa kujenga karakana pale Nansio, ni jambo jema sana natumia nafasi hii kuwapongeza kwa sababu tumekuwa tunapata mazingira magumu sana wakati mgumu sana kusafirisha vyombo vyetu kwenda mpaka Mwanza Mjini kwa ajili ya matengenezo. Kwa hiyo, iwapo itatengenezwa karakana hii itakuwa ni msaada mkubwa sana kwetu kama wananchi wa Ukerewe kuondoa usumbufu ambao tumekuwa tunaupata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ya yote niwashukuru sana kwa hotuba yenu, lakini yale ambayo mmeyaweka kwenye mipango hasa kujenga vivuko mtusaidie kazi hii iweze kufanyika kwa haraka, lakini ombi langu juu ya barabara yetu ile kujengwa kwa awamu ni jambo muhimu sana lipeni uzito mkubwa sana ili muweze kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru na ninaunga mkono hoja. (Makofi)