Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye bajeti hii muhimu sana kwa maisha ya Watanzania na maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametupa uzima, lakini na mimi kipekee nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri, lakini kipekee sana niipongeze sana Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri ambayo inaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti ambayo imewasilishwa kuna ongezeko la fedha kwenye upande wa fedha za maendeleo kwa asilimia 13.7. Jambo hili ni jambo kubwa, ni jambo zuri, tunaipongeza Serikali kwa kuwa tunajua tunaongeza nguvu ya kwenda kutatua changamoto tulizokuwanazo kwenye sekta mbalimbali zinazosimamiwa na Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe mchango kwenye maeneo matatu. Eneo la kwanza ni reli, eneo la pili barabara nae neo la tatu ni bandari.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa reli niipongeze Wizara, lakini nilipongeze Shirika la Reli kwa kazi kubwa na kazi nzuri inayofanyika kwa upande wa reli. Tumeshuhudia ukarabati mkubwa kwenye reli yetu ya zamani; reli ya Dar es Salaam mpaka Moshi, reli ya Moshi – Arusha, lakini pia na ile ya kutoka Mwanza inayokwenda mpaka kwa wenzetu wa Uganda. Kazi hii ni kubwa, kazi hii ni nzuri, tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na tunapopongeza sio kwamba tunapongeza tu, tunapongeza kwa sababu kazi tumeiona na kuna sababu za kupongeza. Sio tu kwenye kukarabati hii reli ya zamani, lakini hata ukusanyaji wa mapato kwa shughuli zinazosimamiwa na Shirika la Reli umeongezeka kutoka bilioni 30 mpaka bilioni 50 sio jambo dogo tunawapongeza sana, lakini kubwa kwa upande wa reli tunaendelea kuipongeza Serikali na Wizara kwa kazi kubwa ya ujenzi wa reli ya kisasa ya Standard Gauge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Standard Gauge alipoingia Mheshimiwa Rais kulikuw na hofu, kulikuwa na maneno, wengine walikuwa na hisia kwamba pengine miradi mikubwa ya kimaendeleo ambayo ameikuta kasi ya utekelezaji wake itapungua. Mheshimiwa Rais amechukua nchi akakuta kuna vipande vile viwili, lot zile mbili ya kwanza na ya pili, lakini leo tunapozungumza kazi inakwenda vizuri kuna mikataba imesainiwa, tumeona kazi imeanza kufanyika. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuhangaika na miradi hii mikubwa ambayo aliikuta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo machache ya kushauri kwa upande wa reli. Niwashauri sana wenzetu wa reli, Mheshimiwa Rais ametoa maelekezo juu ya reli ya kutoka Tabora kwenda Kigoma inayokwenda mpaka DRC. Ni reli muhimu sana kwa uchumi ukiangalia kwamba DRC ni eneo muhimu sana kiuchumi na kwenye soko. Tuwaombe sana maagizo yale ya Mheshimiwa Rais myafanyie kazi kwa haraka ili kazi ya reli kwa kipande hiki ianze tuweze kuliwahi soko hilo la DRC. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili, tumefufua reli ya zamani, tumefanya ukarabati mkubwa, yapo maeneo mengine ambayo bado, ikiwemo reli ya kutoka Kilosa – Malinyi ambayo muda mrefu iliachwa. Ni reli muhimu kuongeza thamani na kazi ya reli ya SGR, lakini pia ukumbuke reli hii ndio kuna makutano kati ya reli ya kati na reli ya TAZARA. Tungeomba sana Wizara muweke kwenye mipango yenu jambo hili liweze kufanyika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho la kushauri kwenye upande wa reli, hii kazi nzuri mnayofanya ya kufufua reli hii ya zamani, yako maeneo ya reli yaliachwa, yako maeneo ya reli yalikuwa hayafanyiwi kazi wananchi wetu waliingia wakafanya shughuli mbalimbali za kimaendeleo ikiwemo shughuli za biashara. Natoa mfano wa eneo la Mombo kule Korogwe Vijijini, niwaombe sana wenzetu wa reli yale maeneo ni muhimu. Kwa yale maeneo ambayo hakuna madhara kwa wananchi wetu kuendelea kufanya shughuli za kujipatia kipato ruhusuni wananchi wetu wafanye shughuli za kujipatia kipato tuweke utaratibu mzuri wa namna gani watu wetu watatumia maeneo haya kujipatia kipato na sio kuwaondoa kabisa ili tuendelee kuwapa Watanzania mazingira mazuri ya kufanya shughuli zao za kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ninalotaka kuchangia ni eneo la upande wa barabara; wiki mbili zilizopita niliuliza swali Bungeni kuhusu barabara ya kutoka Korogwe – Dindira – Bumbuli mpaka Soli; na yale majibu niliyopewa nilisema kama majibu ni haya tukifika kwenye bajeti hatutaelewana hapa ndani. Kipekee kabisa nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri, nimesoma hotuba yako kwenye ukurasa wa 162 nimekuta umetenga fedha shilingi bilioni moja ya kuanza maandalizi ya kuanza ujenzi wa lami wa barabara ya kutoka Korogwe – Dindira – Bumbuli mpaka Soli, nikupongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nisingeiona hii hali ingekuwa tofauti hapa leo, lakini nikupongeze niseme tu kwamba, jambo hili tumelisubiri muda mrefu. Ni ahadi ya Chama cha Mapinduzi kwa zaidi ya chaguzi mbili. Umefika wakati sasa wa kukiheshimisha chama chetu kwa kutekeleza ahadi hii kwa Watanzania ili wananchi wa Korogwe na Lushoto waendelee kuwa na imani na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni barabara hii muhimu sana ya kutoka Korogwe – Mashewa – Bombo Mtoni – Mabokweni na kwenda mpaka Tanga. Barabara hii ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu, lakini kwa ulinzi na usalama wa nchi yetu. Hii ni barabara mbadala ambayo mtu aliyetoka Kenya akipita Horohoro sio lazima aende Tanga, aje Muheza kuja Korogwe kwenda Mikoa ya Kilimanjaro na Arusha. Kupitia barabara hii mtu anayetoka Kenya akitoka Horohoro anaweza kupita barabara hii ni barabara mbadala. Ni muhimu sana kwa ulinzi na uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, Wizara mlituahidi kwamba, mtatenga shilingi bilioni mbili kuanza upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hii, mpaka sasa kuna ukimya mkubwa. Wakati wa kuhitimisha bajeti yako Mheshimiwa Waziri ningefurahi kusikia nini kinachoendelea kwenye barabara hii kulingana na umuhimu wake mkubwa iliokuwanao kwa ajili ya uchumi wa watu wa Tanga, Kilimanjaro, Arusha, lakini na uchumi na ulinzi na usalama wa nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho napenda kuchangia ni eneo la bandari, kipekee niipongeze sana Serikali. niipongeze Mamlaka ya Bandari na watendaji wake kwa kazi nzuri mnayoifanya, kwa miaka zaidi ya sita bandari imekuwa ikijiwekea lengo la makusanyo ya shilingi trilioni moja kwa mwaka mmoja wa fedha, lakini kwa miaka zaidi ya sita hatujawahi kufika wala kukaribia, tumejitahidi sana bandari imeishia kwenye shilingi bilioni 800. Nimesoma hotuba yako Mheshimiwa Waziri, nimeona tuna bilioni mia tisa kasoro kidogo mpaka mwezi Aprili. Nina uhakika kazi ikifanyika vizuri kwa mwezi huu wa tano na mwezi wa sita inawezekana kwa mara ya kwanza tukafikia mipango na malengo tuliyojiwekea ya kufika angalau shilingi trilioni moja kwenye mwaka mmoja wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaongeze sana bandari kwa kazi hii nzuri ambayo mmeifanya. Tunajua kazi hii ni kubwa, lakini endeleeni kuifanya tunawategemea bandari ni eneo muhimu katika mapato na uchumi wan chi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia niipongeze Mamlaka ya Bandari. Mmefanya kazi nzuri kwenye bandari ya Tanga kwenye kuongeza kina na kupanua eneo lile la kufanyia shughuli za bandari, mmefanya kazi nzuri sana na sisi tunawapongeza watu wa Tanga kwa kazi mliyoifanya. (Makofi)

Ombi langu kwenu watu wa bandari, baada ya kazi hii nzuri mliyoifanya na mnayoendelea kuifanya ya kuboresha Bandari ya Tanga, sasa ni wakati muhimu mje na mpango mahususi wa masoko namna gani ya kuongeza mizigo inayopita kupitia Bandari ya Tanga, inayoingia na inayotoka kupitia Bandari ya Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuoni sababu kwa nini mkonge wa Korogwe usafirishwe kwa gari mpaka Dar es Salaam upelekwe bandarini, upelekwe kwenda kutafuta masoko nje, hatuoni sababu. Ni wakati sahihi sasa mjitahidi kuongeza kuitangaza na kutengeneza mpango wa masoko kwa ajili ya bandari ya Tanga ili bandari ya Tanga iendelee kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine la pili kwa upande wa bandari. Tuna mfumo wetu wa Single Window System, unafanya kazi, unatusaidia kuondoa na kuingiza shehena kwenye maeneo yetu ya bandari na maeneo yetu ya mipakani, lakini kumekuwa na changamoto. Ni wakati sasa Serikali iangalie namna ya kuboresha mfumo huu ili tusihangaike na network inatupotezea muda mrefu inatuchelewesha kuweza kuongeza muda wa kusafirisha bidhaa zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mara nyingi system inasumbua na system ikiwa chini maana yake uondoaji wa shehena unachelewa. Ni wakati sasa wa kuangalia namna nzuri na mkakati mahususi wa kuboresha system hii ili mambo yaweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kwenye system hii sehemu kubwa ya uchakataji wa taarifa zote iko centralized makao makuu. Ni wakati pia wa kuangalia kwenye bandari kama ya Tanga, bandari kama ya Mtwara, sio lazima taarifa zichakatwe makao makuu, tufanye decentralization ya huu mfumo ili na kwenye bandari husika Mtwara, Tanga, taarifa zichakatwe, sio wachakate Dar es Salaam wamalize watume, watu wa Tanga wakati mwingine inachelewesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nashukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)