Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwa kidogo kwenye Wizara hii ya Kilimo, Wizara muhimu sana katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri anayofanya, pia pamoja na kuondoa vikwazo vya kufanya biashara na nchi jirani, kufungua fursa za uwekezaji pamoja na Royal Tour ambayo itapanua sekta ya utalii hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Waziri kaka yangu Bashe, Naibu Waziri na timu nzima ya Wizara ya Kilimo kwa kazi nzuri wanayofanya lakini pia kwa sura ya bajeti hii tunayoiona, ya kutoka bilioni 298.1 mpaka bilioni 751; ni mwanzo mzuri sana wa kuleta mapinduzi ya kilimo katika Taifa letu, tunawapongeza sana. Tuwaombe Wizara isimamie vizuri. Bajeti hii muhimu sana tunaamini kwamba itaongeza tija na faida kwa wakulima wetu hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia maeneo machache; eneo la kwanza ni eneo la umwagaliaji. Naipongeza Wizara, nimesoma bajeti hii imeongeza fedha kwaajili ya kuwekeza katika maeneo ya umwagiliaji. Sote ni mashahidi, kwamba kumekuwa na upungufu wa mvua kutokana na mabadiliko ya tabianchi kumekuwa na upungufu wa mvua. Kwa hiyo, ni vema kabisa wizara ikajielekeza kwenye umwagiliaji ili wananchi wetu waweze kufanya kilimo kwa msimu wa mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza maeneo machache eneo la Babati Mjini kwenye jimbo langu kuna Kata za Madunga, Nar na Kameyu, pamoja na Ziwa ambalo halikauki maji katika msimu mzima wa mwaka lina maji ya kutosha niombe sana wizara ijielekeze iwasaidie sana watu wetu hawa waweze kujenga miundombinu ya umwagiliaji maana kuna kilimo kizuri sana cha vitunguu maji pamoja na vitunguu saumu. Naamini kabisa Wizara ikijielekeza huku wananchi wetu hawa watazalisha vya kutosha na kutosheleza soko letu la vitunguu na vitunguu saumu ambalo ni muhimu sana hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Kata za Magugu, Magara, Kiru pamoja na Kisangaji kuna bonde zuri sana la kilimo cha miwa na Kilimo cha Mpunga. Najua wengi mmepita eneo la Magugu, mkipita pale mnanunua mpunga, mchele mzuri sana. Kwa hiyo, niombe sana Wizara hii ya Kilimo; na ninajua Mheshimiwa Bashe ameshafika pale Magugu amejionea milimo cha miwa kwenye shamba pale la Manyara Sugar. Kwa hiyo niombe sana Wizara yetu ya Kilimo iwekeze miundombinu ya umwagiliaji ili tuweze kulima miwa ya kutosha na tuweze kuzalisha sukari kwa manufaa ya wananchi wetu wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili la umwagiliaji niombe sana Wizara ya Fedha iiwezeshe Benki ya Kilimo (TADB) ili iweze kukopesha wakulima wetu kwa riba nafuu; ninaamini sana hii italeta tija kubwa sana kwa wananchi wetu atafanya kilimo chao na kitawasaidia sana katika kuwainua kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, enelo lingine ni eneo la masoko ya mazao. Kutokuwa na masoko ya uhakika ni changamoto kubwa kwa wakulima wetu. Mkulima anahangaika mwaka mzima anafikia kuvuna hajui pakuuza. Naomba sana wizara ifanye utafiti wa kutosha kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanapata masoko ya mazao yao hasa wavijijini ambao wanategemea kilimo kuendesha maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Kata za Galapo, Qash, Ufana, Secheda, nakadhalika kuna wakulima wazuri sana wa mazao kama mahindi, dengu, maharage, mbaazi na mazao mengine lakini kuna tatizo kubwa la masoko. Kwa hiyo, naomba sana Wizara iwasaidie wananchi wetu hawa wanaopambana mwaka mzima; wapatiwe masoko ili wajikwamue kiuchumi na kusaidia familia zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kuhusu eneo la upatikanaji wa pembejeo; naomba sana Wizara ya Kilimo iwasaidie wakulima wetu wapate pembejeo kwa wakati, kama mbegu bora na mbolea, ili waweze kufanya shughuli zao za kilimo na kurahisisha kilimo kufanyika kwa wakati; lakini pia kuna dawa za kuua wadudu. Kumekuwa na dawa nyingi sana kwenye maduka lakini haziui wadudu. Kwa hiyo, naomba sana kufanyike utafiti wa dawa bora ya kuua wadudu ili wakulima wetu waweze kuvuna mazao ambayo wanatarajia kuvuna katika msimu mzima wa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache nikushukuru sana kwa fursa hii naninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)