Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nianze kwa kuunga mkono mapendekezo haya ya Bajeti Kuu ya Serikali lakini kipekee nitoe pongezi nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais lakini vilevile kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha Ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu na Naibu Waziri na uongozi mzima wa Wizara ya Fedha kwa kuona umuhimu wa kuja na mapendekezo haya, mapendekezo ya kimapinduzi, mapendekezo ya kimaendeleo lakini vilevile mapendekezo ya Bajeti ambayo yameangalia makundi mbalimbali pamoja na sekta zote nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika Bajeti hii ni Bajeti ambayo inataka tuelekee zaidi katika kujitegemea. Ukiangalia zaidi ya takribani shilingi trilioni 31.38 zitatokana na mapato ya ndani. Kwa kweli ni hatua kubwa sana na nitoe pongezi sana kwa Wizara nzima ya Fedha chini ya Mheshimiwa Waziri kwa kuja na mapinduzi haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nishukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia hoja hii na ambao wameweza kugusa katika maeneo ambayo Ofisi ya Rais TAMISEMI tunayasimamia katika utekelezaji. Kulikuwa kuna hoja ambayo ilijitokeza huu mchango kuhusiana na utaratibu mpya wa utoaji wa mikopo ya 10% katika halmashauri zetu kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kuhakikisha kwamba mfumo huo mpya unaopendekezwa basi uwe ni mfumo rafiki kwa walengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende tu kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge tayari kikosi cha wataalamu kinaendelea kufanya uchambuzi na mapendekezo na kimeweza kukutana na wadau mbalimbali kwa ajili ya kweza kupata maoni zaidi na pindi utaratibu mpya utakapokamilika basi tutaweza kuutangaza na utoaji na urejeshwaji wa mikopo hiyo utaweza kuendelea. Niwahakikishie kwamba azma yetu ni kuhakikisha kwa kiasi kikubwa inakuwa ni mfumo ambao utakuwa na ufanisi lakini mfumo ambao utakuwa rafiki ambao utaweza kuwasaidia vijana wetu, wanawake na watu wenye ulemavu kuweza kuendeleza shughuli zao mbalimbali za uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna mchango kuhusiana na TARURA kuweza kuongezewa fedha. Kwanza nipende kumshukuru sana Ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu kwa mapendekezo ya nyongeza ya takribani shilingi bilioni 350. Mtakumbuka mwezi wa nne Ofisi ya Rais, TAMISEMI ilipowasilisha Bajeti yake hapa tuliweza kuwasilisha Bajeti ya takribani shilingi bilioni 855.37 kwa ajili ya TARURA na ukiangalia tangu miaka miwili Mheshimiwa Rais Dkt. Samia alipoingia madarakani tulianza na Bajeti ya shilingi bilioni 275.03. Mwaka huu tumeweza kuwasilisha hapa Bajeti ya shilingi bilioni 855.37. Utaona ndani ya miaka miwili tu peke yake takribani mara tatu mpaka mara nne Bajeti imeongezeka lakini hiyo haikutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais bado akaweza kumuelekeza Waziri wa Fedha na wataalamu wake wakafanya uchambuzi na wametuletea mapendekezo ya nyongeza ya shilingi bilioni zingine 350 ambayo endapo Waheshimiwa Wabunge mtapitisha Bajeti hii basi TARURA kwa Mwaka huu wa Fedha wa 2023/2024 itakuwa ina Bajeti ya shilingi trilioni 1.235. Sasa hebu angalia kwa miaka miwili nyuma ilikuwa na Bajeti ya shilingi bilioni 275, nani kama Mheshimiwa Rais Samia? (Makofi)

MBUNGE FULANI: Hakuna.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge kwa kweli nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa usikivu wake lakini zaidi kwa ushirikiano na kuweza kutambua umuhimu wa barabara katika maeneo yetu lakini namna ambavyo tutaweza kufungua maeneo mbalimbali ambayo yalikuwa na vikwazo. Tutajenga madaraja ya kutosha, tutaweka vivuko lakini vilevile tutahakikisha kwamba tunakuwa na barabara ambazo zinapitika wakati wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo katika nyongeza hiyo tutajitahidi kwa kiasi kikubwa kuweza kuweka nyongeza katika fedha ile ya Jimbo ambayo kila Mbunge alikuwa akipata. Tutaongeza shilingi milioni 500 nyingine ya ziada ili kuhakikisha kwamba maeneo yenu mengi zaidi yanaweza kupitika na kuweza kufunguka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukisikia pia mapendekezo kwa kiasi kikubwa Waheshimiwa Wabunge wakihoji ahadi mbalimbali za Viongozi wa Kitaifa. Tumeweka pia walau fedha za kutosha katika eneo hilo kupitia nyongeza hii ya Bajeti ambayo Mheshimiwa Waziri Fedha amependekeza ya shilingi bilioni 350. Kwa hiyo, niendelee kuweka msisitizo tunaomba Waheshimiwa Wabunge waweze kuiunga Bajeti hii mkono na yote haya yametokana kwa kweli na mapendekezo yao kwa namna mbalimbali na vipaumbele vyao kwa kweli niwahakikishie tumekuwa tukivipokea na tutaweza kuvifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kweli nikushukuru sana sana sana na timu yako. Umeturahisishia kazi yetu kubwa na ninaamini haitaishia hapa na ninaamini na mwaka kesho pia mtaendelea kutuangalia katika nyongeza ya Bajeti ili walau sasa TARURA tuendelee kufikika zaidi kwa wananchi, TAMISEMI ya wananchi lakini zaidi wananchi wetu kule na sisi tutakuhakikishia Mheshimiwa Waziri tutakuonyesha kwa vitendo. Barabara hizi tutazielekeza katika maeneo ya uwekezaji, katika maeneo ya kiuchumi, katika maeneo ya uzalishaji ili kuhakikisha kwamba na ule mfuko pale ulipo punguza basi tuweze kukuongezea fedha nyingi zaidi na tuweze kuonyesha matokeo chanya kupitia Bajeti hii na nyongeza mliyotupatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya kuongeza idadi ya shule za kidato cha tano na cha sita. Nipende kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge tumeendelea kupokea mapendekezo mbalimbali na kwenye hili pia tena niweze kuwashukuru sana Wizara ya Fedha kupitia maelekezo ya Mheshimiwa Rais ambayo tumeona fedha nyingi zimeendelea kutolewa. Tutakuwa na takribani zaidi ya shilingi bilioni 248.5 ambazo tutazielekeza katika kuongeza miundombinu mbalimbali kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunakuwa na shule nyingi za kutosha za kidato cha tano na cha sita. Kwenye hili pia nimshukuru Waziri wa Elimu kupitia Kamishna wa Elimu ambao walipopata mapendekezo mbalimbali ya kupandisha hadhi shule ambazo unakuta zilikuwa hazijafikia vigezo baada ya kuweka miundombinu basi wamekuwa tayari kuweza kupandisha hadhi shule hizo tunashukuru pia nao sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa pia kuna hoja ambayo ilitolewa na Mheshimiwa Asenga. Alitaka kuweza kuona Serikali inatoa tamko na haswa katika usafirishaji wa mazao yaliyo chini ya uzito wa tani moja. Nipende tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kupitia jedwali la kwanza la Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa sura ya 290 imeweka zuio la kutokutoza ushuru wa mazao kwa mzigo wenye chini ya tani moja unaosafirishwa kutoka halmashauri moja kwenda nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niendelee kusisitiza tu katika halmashauri zote ziweze kufuata masharti ya jedwali hili la kwanza la Sheria hii ya Fedha ya Serikali za Mitaa na tusije tukaleta usumbufu kwa wananchi wetu mbalimbali ambao wanasafirisha idadi hiyo ndogo ya mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kwa kuhitimisha niendelee kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge wote tumesikia hoja mbalimbali kuhusu hitaji la watumishi. Tuendelee kuwahakikishia kwamba tutaendelea kupeleka watumishi kwa kadiri Bajeti ya Serikali itakavyokuwa ikiendelea kuruhusu na niendelee kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge tayari tumeshapeleka takribani watumishi wa afya 5,319 na tunakamilisha mchakato wa ajira zingine 2,751 na pindi watumishi hawa watakapopatikana pia tutaweza kuwasambaza katika maeneo mbalimbali ya kutolea huduma za afya katika halmashauri zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa vifaa vya afya na vifaatiba. Nimewasikia Waheshimiwa Wabunge tumetenga katika mwaka ujao wa fedha zaidi ya shilingi bilioni 116.92 ambazo tutaweza kuzisambaza katika hospitali zaidi ya 31, katika vituo vya afya 278 pamoja na zahanati mbalimbali 367 nchini na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge mikoa yote mtaweza kuguswa na usambazaji huo wa vifaa na vifaatiba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa pia na hoja kwa upande wa magari ya wagonjwa na kwenye hili pia niendelee kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge tumeendelea kuyapokea tunaamini muda siyo mrefu tutaweza kukabidhi magari mawili mawili katika kila halmashauri lakini vilevile gari moja kwa ajili ya usimamizi wa huduma mbalimbali za afya na uratibu katika maeneo yenu katika halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa pia na hoja ya mfumo wetu wa TAUSI. Niendelee kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge tumeendelea kuuimarisha na sasa tunatoa leseni zote za kibiashara na leseni nyingine mbalimbali katika mfumo wa kidijitali. Tuendelee kuwaomba Waheshimiwa Wabunge waendelee kusaidia kuwahamasisha wananchi wetu watoe ushirikiano na kuweza kutumia mfumo huu wa TAUSI kwa ajili ya ukusanyaji wa mapato lakini vilevile katika kupata huduma mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipatia nafasi na nipende kusema ninaunga mkono hoja hii kwa 100%. (Makofi)