Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwanza, napenda kuwapongeza wananchi wa Jimbo la Mlalo kwa imani yao kubwa ambayo imenifanya leo nasimama mbele ya Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niungane na Wabunge wenzangu kuchangia Hotuba ya Mheshimiwa Rais kama alivyoitoa tarehe 20 Novemba, 2015.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanzia na zoezi zima la utunzaji wa mazingira. Duniani kote sasa hivi tunazungumzia mabadiliko ya tabia nchi. Nadhani tutakubaliana sote kwamba hata haya matatizo ya maji tunayoyazungumza kutoka kwenye Majimbo tofauti yamesababishwa
na namna ambavyo tumeharibu mazingira yetu. Tunapozungumzia utunzaji wa mazingira, tunamaanisha pamoja na utunzaji wa vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitatoa mfano katika Jimbo langu la Mlalo, tunao Msitu wa Asili wa Shagayu mwaka 2012 uliungua moto takribani hekari arobaini na tisa lakini ni hekta kumi na moja tu ndizo ambazo zimepandwa. Cha kusikitisha mvua za Desemba zimesababisha maafa makubwa kwa sababu ardhi imekuwa loose, imesababisha maporomoko na mafuriko katika kata za Mtae, Shagayu, Mbalamo na Mnazi. Hii yote ni kwa sababu ya uoto wa asili ambao umeondoka.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na tatizo la uharibifu wa mazingira katika maeneo ambayo yanazunguka msitu wa Shagayu vilevile kuna tatizo la nguvu kazi. Msitu wa Shagayu unazungukwa na takribani vijiji kumi na tano lakini wako Watendaji wawili pekee na wanatumia
pikipiki moja. Nimuombe Waziri wa Maliasili kupitia Serikali yetu sikivu ahakikishe kwamba anawasaidia Watendaji ili waweze kufanya kazi hii ya utunzaji wa mazingira na misitu kwa ufanisi unaotakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili nitajikita kwenye kilimo. Kama sote tunavyotambua kilimo ndiyo mhimili wa uchumi wa nchi yetu ya Tanzania. Kwa wakazi wa Jimbo la Mlalo na Halmashauri ya Lushoto kwa ujumla wake, ni takribani asilimia tisini na nane wanategemea
kilimo. Tunaomba kupitia hotuba hii ya Mheshimiwa Rais, Wizara inayohusika itufanyie yafuatayo katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto. Tunayo maeneo ya aina mbili, ya milimani ambapo tunaendesha kilimo cha mbogamboga na matunda katika kata za Lukozi, Malindi, Rangwi, Sunga na Shume. Kuna tatizo kubwa la wakulima kunyonywa pindi wanapovuna mazao yao kwa kutumia mtindo wa lumbesa. Lumbesa imekuwa ni sehemu ya unyonywaji wa wakulima, hivyo mwisho wa siku hawaoni faida ya yale mazao ambayo wanayavuna. Hivyo, naomba Bunge lako Tukufu, tuisimamie Serikali kuhakikisha kwamba kunakuwa na udhibiti wa ufungaji wa mazao kwa njia ya lumbesa. Tunatambua Wizara ya Viwanda na Biashara ina Wakala wa Mizani na Vipimo, tunaomba ilisimamie suala hili ili liweze kupatiwa ufumbuzi wa mwisho.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni ukanda wa tambarare. Ukanda huu tunapata changamoto kwamba mvua zinazoshuka katika mabonde yetu na makorongo zinaelekea baharini na maji yanapotea bure. Tunaomba Wizara ya Kilimo ije na mpango wa kutujengea
mabwawa ili tuweze kuhifadhi maji yanayotiririka wakati wa msimu wa mvua. Maji haya yatasaidia wananchi kuendesha kilimo chenye tija kwa msimu mzima wa mwaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika maeneo hayo tunayo mapori mazuri ambayo yakitumika vizuri kwa kuzingatia rasilimali ardhi, tunaweza tukaanzisha benki ya ardhi ambayo itakuwa ni kivutio kimojawapo kwa wawekezaji ambao wanatafuta maeneo ya kuwekeza. Pia
kwa kutumia mipango ya ardhi, tunaweza pia tukawatengea wafugaji ambao nao pia wanapatikana katika eneo hili, wakapata maeneo ili waachane na kasumba ya kuswaga ng‟ombe kila mahali. Tutakuwa tumewajengea uwezo wa kukaa mahali pamoja ambapo hata
Serikali inaweza ikapata kodi yake stahiki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia hotuba hii nzuri ya Rais lazima pia tufungue fursa mpya za kuwawezesha wananchi wetu. Jimbo la Mlalo, Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto inapakana na nchi jirani ya Kenya. Tunao mpaka kule ambao unatumiwa kwa ajili ya shughuli za kupitisha magendo pamoja na kupitisha Wasomali ambao wanapita kwa njia za panya.
Niiombe Serikali ione kwamba hii ni fursa ya kufungua kituo cha mpaka katika eneo la Kata ya Lunguza ili tuweze kufanya biashara na nchi jirani ya Kenya. Ni jambo jema kabisa kwamba ulinzi wa mipaka yetu ni jukumu ambalo halikwepeki lakini tukiweza kuweka kituo cha biashara na mpaka itasaidia wafayabiashara kuweza kwenda nchi jirani na pia itatusaidia na sisi kuuza mazao yetu katika nchi jirani ya Kenya.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua suala zima la umeme vijijini. Tunashukuru umeme vijijini umesambazwa kwa kiwango cha kutosha lakini pia niombe Waziri anayehusika na nishati katika Jimbo langu bado kuna kata zaidi ya nne hazijaguswa na nguzo hata moja. Naiomba
mamlaka inayohusika kupeleka umeme vijijini atambue Kata za Shagayu, Mbaramo, Mbaru na Sunga ili nazo ziweze kupewa kipaumbele katika usambazaji wa umeme vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo napenda kulizungumzia ni rushwa.
Mheshimiwa Rais ameanza vizuri, anapambana na majipu makubwa katika ngazi ya kitaifa. Kupitia Bunge lako Tukufu, naomba pia Waziri wa TAMISEMI, ashuke huku chini katika Halmashauri zetu, miradi mingi inafanywa chini ya utekelezaji uliokusudiwa. Huku nako kuna
mchwa wanatafuna pesa, miradi haina tija, miradi haikamiliki kwa wakati, wanawazungusha Madiwani kwa sababu wanatumia uelewa hafifu wa Madiwani wetu walioko huko vijijini pamoja na Watendaji wa Vijiji. Naiomba Wizara husika ilisimamie hili kwa jicho la karibu zaidi.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo naomba kuwasilisha, ahsante sana.