Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Aleksia Asia Kamguna

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi. Awali ya yote sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupatia ruzuklu ya uhai. Pia nampongeza Mheshimiwa Rais Samia kwa kazi anazotupambania pamoja na wafanyakazi wake wote wanaomsaidia, Mawaziri, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri wote tunawapongeza pamoja na Watanzania kila mmoja kwa nafasi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais Samia, ametufanyia mambo makubwa sana katika hii miaka yake miwili ya Awamu ya Sita. Sisi hasa watu wa Malinyi ambao tuko pembezoni ya miji tulikuwa tunalalamika, kama mwaka juzi nililalamika sana kuhusu barabara, lakini tarehe 16 walienda kusaini mkataba huu wa EPC + F kwa ajili ya matengenezo ya ile Barabara. Ninaamini ile shida ya barabara ambayo tulikuwa tunaipata sasa tutaondokananayo, kwani itatuunganisha kutoka Lupilo – Malinyi – Namtumbo na hatimaye Ruvuma. Tunakushukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ametutendea mengi. Katika awamu yake hii ameimalizia miradi ile mikubwa ya kimkakati ambapo watu wengi, Watanzania tulikuwa na wasiwasi, lakini wasiwasi ule Mheshimiwa Rais ameumaliza. Mradi wa reli ya SGR, Mradi wa Daraja la Busisi, Mwanza na Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ambalo ni bwawa kubwa, tunajivunia na limetumia fedha nyingi sana. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais pamoja na watendaji wote tunawashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwenda kwenye hoja kwamba, katika Bwawa la Mwalimu Nyerere lile bwawa ni la mkakati katika nchi yetu ya Tanzania, lakini ni bwawa ambalo limepita kwenye Mikoa, na sehemu kubwal imepita katika Mkoa wa Morogoro. Katika ule mkoa kuna sehemu ambazo zimepitiwa. Kwa vyovyote vile, maendeleo yoyote huwa yakifika lazima kutakuwa na baadhi ya watu kuathirika. Katika kuathirika kule, wale wananchi wamekubali na wamesema kwamba bwawa liendelee kwa sababu faida yake ni kubwa kuliko hasara ambazo tumezipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukulia Mkoa wa Morogoro, hususan Bonde la Kilombero. Bonde la Kilombero ni bonde ambalo lile bwawa ni sehemu ambayo inapatikana maji kwenye chanzo, hasa katika Kijiji cha Ngombo. Kile Kijiji cha Ngombo kilifanyiwa tathmini mwaka 2022 mwezi wa kumi na moja mpaka mwezi wa kumi na mbili, 2022. Baada ya kufanyiwa tathmini ya nyumba, makazi, makaburi, na kadhalika, lakini Serikali tangu pale iko kimya. Wale watu hawajapata fidia. Hatujui wale watu ile fidia wataipata lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika kupata fidia, naiuliza Serikali, yule mwananchi wa Ngombo ambaye anatakiwa kuondoka; na tumekubali kuondoka, na ni wajibu wetu kuondoka kupisha lile bonde: Je, atakapoondoka, anakwenda wapi? Huko anakokwenda, ataishije? Maana hajapata fidia? Kule Ngombo kuna shule ya msingi, wale watoto wao watakapoondoka wataenda kusoma wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali ituelekeze hayo kwa sababu, wale ni wakulima, sasa hivi ni kipindi cha mavuno, watu hawaambiwi chochote kwamba mnatakiwa kuondoka, lakini hawajapewa ile timeframe. Kitakapofika kipindi cha kuanza tena kilimo, wale watu wataambiwa waondoke. Sasa kwa nini usimweleze mtu kipindi hiki ambacho anavuna, ajue kwamba nikimaliza kuvuna, nitaelekea wapi? Badala ya kumsubiria kipindi cha kiangazi ambacho anataka kuanza tena msimu mwingine wa kulima, watu wanaambiwa waondoke?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali, chonde. Tunajua Serikali ya Mama Samia ni sikivu. Tunaiomba itupatie fidia mapema iwezekanavyo ili wale watu waondoke eneo husika na hatimaye waweze kupata makazi mapya na waendelee na maisha yao kwa amani, kama walivyofanyiwa wenzetu wa Msowelo, wametoka Ngorongoro, wameenda Handeni, Tanga, wamepewa malipo yao, wameondoka kwa usalama. Nami naamini hata zoezi la Ngombo nalo litafanyika kwa amani ili nchi yetu iendelee kuwa na amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala langu la pili, nazungumzia kuhusu wanyama. Mkoa wa Morogoro ni Mkoa ambao kila siku nasema tumebahatika. Miongoni mwa mikoa iliyobahatika Morogoro ni mmojawapo. Tumepitiwa na mbuga ya Wanyama ya Selous ambayo sasa hivi tunaiita ya Mwalimu Nyerere, Mikumi, Udzungwa, na kadhalika, lakini Mkoa ule tuna adha. Tembo au wanyama wakali wanatusumbua. Sasa katika wale wanyama wakali jamani, ukiangalia sana kimkoa, unakuta ule mkoa sisi kama Serikali isipokuwa na huruma ya kutuangalia, kuwe na mkakati wa makusudi kwa ajili ya kuwaokoa wananchi wa mkoa ule. Ukweli sisi tutaisha kwa sababu, ule mkoa unapakana na hizo mbuga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ninapoongea hapa katika Wilaya ya Mvomero, kuna Wilaya ya Malinyi na Wilaya ya Kilosa. Mfano, Wilaya ya Mvomero ni Wilaya ambayo inapakana na Tarafa ya Mlali ambayo ina Kata za Doma, Lubungo, Merera, Msongozi na Mangai. Sasa hivi ninavyoongea hapa, katika mwaka huu tu, watu 42 wameshafariki katika Wilaya ya Mvomero, Tarafa ya Mlali. Ombi letu ni nini kwa Serikali? Hatuwezi tukasema kwamba zile mbuga hatuzipendi, tunazipenda sana, lakini sababu ni nini ambayo inafanya wale wanyama watoke kwenye njia zao au kwenye maisha yao ya asili waje kwenye miji ya watu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ni kwamba, unakuta kwenye zile mbuga za wanyama kuna watu wanaishi kule wenye mifugo. Wafugaji wameingia kwenye zile mbuga zetu. Sasa zile mbuga wanavyoingia kule wanasababisha wale wanyama wanashindwa kuishi kwenye maeneo yao ya asili. Wanapika na wengine wamejenga kwenye njia za wale Wanyama. Matokeo yake wale wanyama wanatoka, wanakuja kwenye makazi ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwenye mbuga kuna Askari ambao ni Askari wa Wanyamapori. Why yule mfugaji anajenga kibanda, ana ng’ombe labda 2,000? Ina maana wale Askari hawawaoni hao ng’ombe 2,000? Hawawaoni hao wachungaji? Hata hivyo wale wanyama wanatoka wanakuja kwa watu kwa sababu eneo lao la asili limekaliwa na watu ambao wanawasumbua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo ni kwamba, Wizara ya Maliasili kwa namna nyingine inahusika kupitia Askari wao. Inakuwaje wanyama na wale binadamu ambao wanaingia kwenye zile mbuga wasiwaone, lakini mwananchi wa kawaida akienda kutafuta kuni anaonekana? Ina maana wale wanyama hawaonekani? Ni wadogo kiasi kwamba mwananchi wa kawaida anaonekana? Tunaiomba Serikali, chonde ituonee huruma, ituwekee fence ikiwezekana. Tupate angalau tuweze kuzuia wale wanyama wasiingie kwenye makazi ya binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala langu la tatu, sisi Morogoro ni Mkoa ambao una mkakati. Ni Mkoa ndani ya mikoa yenye mikakati ya kilimo. Tunamshukuru Mungu na kweli Waziri wa Kilimo ametupelekea wataalamu kule. Nililalamika sana kuhusiana na suala la kwamba hatuna soko la mazao hasa ya mpunga, lakini kuna wataalamu wako kule, wanakaa wanafanya tathmini kuona ni jinsi gani ya kuendesha hilo soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika huu mkoa, kuna shida ya ushuru. Wakulima wengi wakienda kupeleka mazao yao, kwa mfano, Serikali mlituambia kwamba mtu anatakiwa kulipishwa mpaka ifikie tani moja ya mzigo, lakini sisi mtu akiwa hata na kilo 20 analipishwa; akiwa na kilo 80, analipishwa: Je, Serikali ule uamuzi wa kusema kwamba wananchi wanatakiwa walipie kuanzia tani moja umesahaulika? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja. Tunaomba Serikali mtusaidie, ule mkoa jamani ni wa kimkakati, ili tuweze kuishi kama wengine wanavyofurahia maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)