Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia kwenye hii Bajeti Kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba kwa niaba ya wananchi wa Buhigwe na wananchi wa Mkoa wote wa Kigoma nitoe pongezi za dhati kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi kubwa sana ambayo anaifanya kwa kufungua Mkoa wetu akishauriwa na Makamu wa Rais Dkt. Philip Isdory Mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru sana Mkoa wetu wa Kigoma umeendelea kufunguliwa katika Awamu hii ya Sita kupitia miundombinu ya Barabara, sasa Mkoa wa Kigoma tunaenda kuunganishwa rasmi na Mkoa wa Tabora. Tunayo barabara ambayo Mheshimiwa Rais ametoa fedha kulikuwa kumebakia na kipande kidogo cha kutoka Kazilambwa mpaka Magu mpaka Chabu pale Nguruka kilometa 36 Mkandarasi yuko site. Kulikuwa tumebakia kipande cha kilometa 51.1 cha kutoka Malagarasi hadi Uvinza Mkandarasi yuko site tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunaenda sasa kuunganishwa na Mkoa wa Kagera kuanzia Kakonko kuja Kibondo sasa ni lami, tuna kipande kingine ambacho sasa ni cha Mvugwe – Nduta kilometa 59 Mkandarasi yuko site, tuna Mvugwe – Kanyani kilometa 70.5 Mkandarasi yuko site, na tuna Kasulu Manyovu kilometa 68 Mkandarasi yuko site, tunashukuru sana. Miradi hii inaenda kugharimu zaidi ya bilioni 560 katika mradi huu mkuu wa kutuunganisha na Mkoa wa Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na barabara hii ndani yake kulikuwa na miradi ya bakshishi inaitwa complimentary projects. Miradi hii ilitakiwa kwa kadri inavyotekelezwa tuliomba na inatakiwa kwenye mujibu wa mkataba na inatakiwa miradi ile ambayo ni bakshishi ya mradi huu nayo iwe imetekelezwa. Ndani ya hizi bilioni zaidi ya 560 zipo bilioni 23 kwa ajili ya kutengeneza shule ya Sekondari ya kisasa Buhigwe. Tunaomba Serikali sasa iandae utaratibu ili hii miradi ambayo ni complimentary projects ya mradi huu mama nayo ianze kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo ujenzi wa kituo cha mabasi kule Manyovu na ujenzi wa kituo cha forodha tuongeomba navyo utekelezaji wake uende sambamba. Upo ujenzi wa kituo cha afya Makere nao tungeomba ujenzi huo uanze mara moja. Pia upo ukarabati wa stendi ya Kibondo pamoja na Hospitali ya Wilaya ya Kibondo, tungeomba navyo viende sambamba. Tunashukuru sana Mheshimiwa Rais, sambamba na hilo tunamshukuru na Waziri wa Fedha Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya, endeleeni kutoa fedha kwenye miradi inayounganisha na inayoenda kuufungua Mkoa wetu wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kushukuru ni kuomba, tunaomba tena sisi tupo mpakani mwa Burundi na Congo, bado tunazo barabara muhimu ambazo hizo zikitengenezwa kwa kiwango cha lami zitaleta tija, zitaongeza mapato katika nchi yetu lakini zitachagamsha biashara kati ya nchi ya Tanzania na Burundi na Congo. Barabara hizi nazo zimekwishafanyiwa usanifu ningeomba kwenye bajeti hii ya 2023/2024 nazo zitengenezwe kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hiyo ni ya Kalela – Muzenze – Janda kilometa 57 na barabara ya Buhigwe – Muyama – Kilelema – Kitundu kilometa 120 na barabara ya Kakonko – Muhange kilomita 38. Hizo barabara zote zinakwenda kutuunganisha na nchi ya Burundi na Congo ambapo sasa tunaenda kufanya bishara nao. Tukifanya nao biashara, kama Kigoma itafanywa kuwa Mkoa wa kiuchumi, ikafanyika kuwa ndiyo hub ya uchumi, Tunaamini nchi hii itaenda kukuza uchumi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalo ombi lingine ambalo ni malalmiko ya muda mrefu ya wafanyabiashara. Wafanyabiashara wana mangung’uniko wana malalamiko kwenye mfumo wa ETS, ningeomba sana Serikali pamoja na Mkandarasi aliyepewa kazi hiyo ya ETS pamoja na wafanyabiashara, wakae pamoja waangalie namna gani ambavyo wanaweza wakaondoa malalamiko au minong’ono au manung’uniko ya wafanyabiashara ili bei iweze kushushwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kuchangia tena kuhusu kilimo. Sisi kwenye Jimbo letu la Buhigwe tuna kituo cha TaCRI ambacho kinazalisha mbegu na miche bora ya kahawa. Kwa mwaka 2022/2023 tumeona zao la kahawa ndiyo zao ambalo limeongoza kuipatia nchi zaidi ya bilioni 248 fedha ya kigeni. Ninaishauri Serikali ili iweze kupata fedha nyingi za kigeni ni lazima kuwepo na mkakati wa dhati wa kuhakikisha maeneo na mashamba yanayolimwa kahawa yanaongezeka, pia kuwepo na kusudi madhubuti kabisa la Serikali kusaidia Wizara ya Kilimo, iweze kuzalisha miche ya kahawa kutoka milioni 20 ambayo inazalishwa sasa ifike zaidi ya milioni 200. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ukiangalia wenzetu wa Uganda kwa mwaka wanazalisha miche milioni 161, ukenda Ethiopia wanzalisha miche zaidi ya milioni 360. Kwa nini sisi ambao tuna eneo kubwa kabisa linalofaa kwa kulima kahawa, zaidi ya Mikoa 16 sasa hivi inalima kahawa, kwa nini tuzalishe miche 20,000 kwa mwaka? Haitoshi! Hili zao lenyewe ndiyo linalotuingizia fedha nyingi za kigeni, ningeomba muangalie wakulima wa zao la kahawa, mtafute namna gani ambavyo mnaweza Serikali ikaongeza nguvu pale miche iongezeke na ikiwezekana zao hili la kimkakati nalo liangaliwe ni namna gani ambavyo hawa wakulima wanaweza kupewa ruzuku, kwa sababu ni sehemu ambayo Serikali inapata fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa pili niende kwenye biashara. Mkoa wetu wa Kigoma umepakana na nchi ya DR Congo, Burundi na Zambia. Katika Ziwa letu Tanganyika, bado hatujapata meli. Meli zote zilisimama, tunahitaji meli ili biashara zilizokuwa zikifanyika siku za nyuma kwenda Zambia kwenda Moba, kwenda Kalemi, kwenda Ubwari, kwenda Uvira, kwenda Goma kwenda Gbadolite. Palikuwa pamechangamka na Mkoa ulikuwa umechangamka zirudi. Tunaomba bajeti hii ambayo imeelekeza na imetoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa meli mpya nazo zitengenezwe ili kupunguza changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)