Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami niungane na wenzangu kwa dhati kabisa kuipongeza bajeti hii. Ni bajeti ambayo inaenda kuisaidia nchi, inaenda kumkomboa mwananchi wa chini kabisa. Naipongeza Serikali kwa nia ile ya dhati ya kupeleka mikopo kwa vyuo vya kati na pia kuwapeleka wanafunzi kwenye vyuo nao wakasome kwa elimu bure. Suala hili linaoenesha kwa kiasi gani Serikali hii ya Awamu ya Sita ilivyo sikivu. Kwa sababu maoni haya yalitolewa hapa, walishauri Mawaziri hapa, na muda siyo mrefu Waziri wa Fedha amekaa chini, ameshauriana na Mheshimiwa Rais, leo tunaambiwa watoto wataenda kusoma bure, kwa maana ya vyuo hivi, pia na mikopo kwa vyuo hivi vya kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli suala hili litapunguza kero kubwa kwa Mtanzania wa kawaida na kwa sisi viongozi, Wabunge baadhi yetu tulikuwa tunahangaika kusomesha hawa wanafunzi pale ambapo wamekuja maofisini kulia kwamba hawana ada. Serikali hii ya Awamu ya Sita imeliona hili na sasa inaenda kulifanyia kazi. Naipongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naendelea kuipongeza Serikali hii kwa kuendelea kutenga fedha nyingi kwenye kilimo. Tunajua tulianza na shilingi bilioni 294 bajeti ya nyuma kidogo, lakini bajeti ya mwaka 2022 na bajeti hii inaonesha wazi kwamba Serikali hii ina nia juu ya kilimo. Ina nia ya dhati kukitoa kilimo kule kulipokuwa na kukipeleka sehemu nyingine. Safari hii Mheshimiwa Waziri mmekitengea kilimo shilingi bilioni 970. Ni fedha nyingi sana hiyo, itaenda kufanya mambo mengi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikia hapa maoni ya Wabunge wenzangu, nami nina mchango kidogo hapo. Tunapokitoa kilimo kutoka sehemu moja kwenda nyingine kwa kutenga hizi fedha nyingi, tunatarajia uzalishaji mkubwa, tunatarajia wingi wa mazao. Kwa maana ya wingi wa mazao, tunatarajia kuwa na soko zuri. Sasa ziko hofu zinazoonekana hapa kwamba baadhi ya malighafi kutoka nje zimepunguziwa kodi. Kwa kupunguza kodi unasababisha mazao yetu tunayozalisha hapa nayo yashuke bei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja kwa Watanzania wenzangu hapa, zao likiwa halina bei hawalimi. Hawatalima. Hofu iliyopo hapa, tutarudi nyuma; watu wataacha kulima. Tunajua kuna maeneo waliacha kulima kahawa, kuna maeneo waliacha kulima mahindi, kuna maeneo waliacha kulima mbaazi, kuna maeneo watu waliacha kulima hata korosho. Sasa kwa nini ifikie huko wakati nia yetu ni njema, Mheshimiwa Rais amefanya kazi nzuri ya kutafuta hata wawekezaji huko nje wa mazao yetu. Kwa nini tukaribishe hizo bidhaa nyingine kutoka nje kwa kuweka kodi? Hata Mheshimiwa Waziri amesema kwamba kodi imebaki vilevile, mapendekezo yangu ni kwamba ingebidi wewe uongeze ili alizeti yetu ipate soko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, jana, juzi na majuzi yaliyotangulia, nimepigiwa simu nyingi sana na wananchi wangu. Sisi kule tunazalisha na tunamshukuru Mungu mwaka huu mvua ilinyesha kiasi cha kutosha. Kwa hiyo, tuna mahindi mengi sana. Mwaka 2022 niliuza swali hapa kwa Waziri Mkuu, na Waziri Mkuu alitoa maelekezo hapa kwamba hatufungi mipaka. Nami sijaona katazo hilo kwamba mazao sasa yasiuzwe nje, lakini sasa hivi ziko hofu huko mitaani, wanasema vibali vya kupeleka mazao nje vimezuiliwa. Hali hii imesababisha mahindi yetu pale jimboni yalikuwa yanauzwa shilingi 75,000 kwa gunia, sasa yanauzwa shilingi 35,400 mpaka shilingi 40,000. Hii inamkatisha tamaa mkulima. Juzi tu hapa tulikuwa tunaongelea mahindi, yalikuwa yanauzwa shilingi 80,000 mpaka shilingi 90,000, leo hii tuna vuna mahindi... (Makofi)

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: …kwa kusema yasiuzwe nje, mahindi tunaenda kununua shilingi 35,000 na shilingi 40,000/=…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Benaya, kuna taarifa.

TAARIFA

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kumpa taarifa Mheshimiwa Kapinga ambaye anachangia vizuri sana, kwamba tatizo hili kufungwa kwa soko la mahindi nje, limekuwa ni kero kubwa kwa mikoa yote ya Nyanda za Kusini. Hata Jimbo la Lupembe mahindi yameporomoka bei sana. Tunaomba Serikali itoe kauli, hili jambo likoje? Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Benaya Kapinga, unaipokea taarifa hiyo ya Mheshimiwa Swalle?

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea hii taarifa kwa sababu ni kweli. Nami hofu yangu ni kwamba sijasikia kauli ya kukataza mahindi yasipelekwe nje, nilichosikia tuwe na hifadhi ya chakula ndani ya nchi, lakini siyo kwamba tusiuze nje. Sasa naiomba Serikali, Mheshimiwa Waziri wakati anakuja kuhitimisha hapa, atuambie, ni kweli kuna katazo la mahindi kutouzwa nje? Ni kweli lipo hilo katazo? Nasema hivyo kwa sababu wananchi wetu wamelima vizuri, waliitikia vizuri wito na kweli uzalishaji ni mkubwa na wala hatutakuwa na njaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo ningependa kuiongelea hapa ni suala la miradi ambayo tunaendelea kuitekeleza katika nchi yetu. Niipongeze sana Serikali hii imekuwa na jitihada kubwa ya kupeleka fedha nyingi katika miradi kwenye kila eneo la nchi yetu na miradi inaonekana na katika Jimbo langu nashukuru sana tulikuwa na shida ya barabara tulipata barabara ya kwanza ya kutoka Songea – Mbinga hadi Mbamba Bay na kipindi hiki tumepata mkandarasi anajenga barabara ya kutoka Kitai kwenda Rwanda hadi Litui lakini barabara hii imesimama kwa muda mrefu. Toka mwezi wa pili barabara hii haiendelei hawajengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii inapitisha magari makubwa makubwa ya makaa ya mawe. Magari zaidi ya 3,000 mpaka 4,000 yanapita lakini barabara hii ni ya vumbi. Sasa hivi tayari tumeanza kupokea taarifa za vifo kwa sababu magari yale yanavyopita vumbi jingi wanagongwa watu, zinatokea ajali watu wanavunjika. Kwa kweli inakuwa ni hatari kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii tuliambiwa ingejengwa kwa miezi 12 lakini sasa miezi 12 kuanzia mwezi wa pili, wa tatu, wa nne, wa tano na huu wa sita miezi mitano kazi haiendelei. Kweli tutaenda kukamilisha hii barabara kwa miezi 12? Shida kubwa anayosema mkandarasi Mheshimiwa Waziri hajalipwa. Hajalipwa tangu, ameleta certificate huko hajalipwa. Kwa hiyo hawezi kufanya kazi ameleta certificate ya kwanza, ya pili, ya tatu. Ombi langu Mheshimiwa Waziri tumlipe huyu mkandarasi ili ile barabara ijengwe ikamilike, itumike kwa sababu ina manufaa makubwa sana kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama makaa ya mawe yote yanayosafirishwa kwenda nje na yanayoletea pato kubwa nchi hii yanatoka pale lakini hayana njia kwa kweli inakuwa shida kubwa sana. Kwa hiyo, niombe sana mkandarasi huyu alipwe ili ile barabara iendelee na ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine niipongeze Serikali kwa mradi huu wa ETS. Mradi huu una manufaa makubwa kwa sababu una faida kwa maana ya kwamba sisi kama nchi tunajua bidhaa zetu. Tunajua idadi ya bidhaa tulizonazo na inatuletea faida kubwa. Kwa hiyo, yapo malalamiko kidogo kwamba huyu mkandarasi huyu charge zake ziko juu. Kwa hiyo, niombe Waziri kaeni na huyu mkandarasi a-charge at a minimum price kiasi kwamba isilete kero kwa wananchi kwa kweli nikupongeze Mheshimiwa Waziri kwa kuendelea na mradi huu una manufaa makubwa kwa nchi yetu. Hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze pia Serikali kwa kazi ile kubwa tuliyoifanya mwaka jana ya sensa na bahati nzuri mwaka huu tumepewa takwimu pale kwamba sasa matokeo ya sensa yako tayari na tumeyaona na kwa kweli ni sensa ya kipekee kwa sababu ina idadi ya watu, ina idadi ya makazi lakini ina idadi ya vituo vya kutolea huduma mbalimbali lakini na mifugo. Kwa kweli wataalamu wanavyotuambia ni sensa ya kipekee. Naipongeza sana Serikali yangu hii ya Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo takwimu zile tuzitumie. Tusizitumie kwa idadi ya watu tu. Siku ile pale tumeoneshwa namna huduma zilivyo sambaa. Utakuta concentration ya baadhi ya huduma ziko upande mmoja na upande mwingine una watu wengi hauna huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali kupitia hii sensa tuitumie vizuri, tugawanye mgawanyo wa huduma vizuri. Pale ambapo kuna mapungufu tupeleke huduma siyo kwa sababu tu kwamba labda kuna huduma zigawike kwa idadi kubwa ya watu aah. Hata kwa kuona kwamba zile huduma zingine kwa mfano zahanati au kituo cha afya watu wako sehemu of course ni wachache lakini wanapata huduma mbali sana kwa mujibu wa sensa umeonesha pale kwamba kituo cha afya kipo sehemu fulani na sehemu fulani huku hakuna huduma kwa hiyo watu wanatembea zaidi ya kilometa 20. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano Kata yangu ya Ukata idadi ya watu kweli hiyo sifa haina lakini kwa idadi ya umbali na milima ina sifa ya kutosha kabisa. Kwa hiyo, niombe wataalamu wetu wagawanye hizi huduma kwa kutumia hizi takwimu. Wasilenge tu ile kwamba idadi ya watu ni chache. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo hivyo mwaka jana na mwaka huu pia nilikuja na ombi la kugawanya Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga. Ina watu wa kutosha lakini inawezekana pakawa na kigezo cha kwamba aah, huku ni vijijini na huku ni mijini, mjini kuna concentration kubwa ya watu tuka concentrate kugawa halmashauri za mjini. Kijiografia halmashauri hii ni kubwa sana kiasi kwamba mwananchi wa kule chini kuja kupata huduma anatumia muda mrefu, anatumia nauli kubwa, na wengine wanaishia tu kukaa nyumbani na kusema aah, acha tu hilo lipite hivyo lakini anainung’unikia Serikali yake. Kwa hiyo, niombe sana kupitia hii takwimu tugawe hizi huduma vizuri na zitusaidie kwa manufaa ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo ninaunga mkono bajeti hii kwa 100% kwa sababu inaenda kutusaidia sana sana, sana, ahsante. (Makofi)