Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante. Muda wangu nitagawana na jirani yangu Mheshimiwa Japhary, kama atawahi, asipowahi nitaendelea mimi mwenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ya mwanzo jioni hii ya leo. Tunapoongelea uchumi wa viwanda, ni jambo la kufurahisha kwamba bajeti tunayoijadili jioni hii ina mchango mkubwa sana katika kutufikisha kwenye uchumi huo wa viwanda. Naomba nijielekeze katika eneo la kwanza la upembuzi yakinifu, mara nyingine usanifu wa kina na wakati mwingine wanapenda kutumia maneno Mhandisi Mshauri na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua sana umuhimu wa zoezi hilo la kabla ya miradi kutekelezwa, lakini niseme kwamba, zoezi hili limekuwa ni kichaka cha kujifichia kwenye Wizara hii, Mawaziri wakijibu asubuhi maswali utaambiwa mradi huo uko kwenye upembuzi yakinifu; baadaye utaambiwa uko kwenye usanifu wa kina; baadaye utaambiwa Mhandisi Mwelekezi anaendelea. Kwa hiyo, nataka kushauri, wananchi wetu kule nje wanachotaka kuona, ni miradi inatekelezwa. Pamoja na kwamba hatua hii haiepukiki na ni muhimu sana, nashauri hebu tupunguze muda wa mazoezi haya, ili hatimaye tuingie kwenye masuala ya utekelezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingine mazoezi haya yamechukua miaka ya kutosha miaka mitano, upembuzi yakinifu siku nyingine miaka mitano, usanifu wa kina na kadhalika, kwa hiyo, mradi utakuja kutekelezwa baada ya miaka 10, 15 mpaka 20. Tuna mfano hapa uwanja wa ndege wa Msalato, ukienda pale Msalato hadi leo ni pori tupu, lakini miaka kadhaa iliyopita mazoezi haya yalifanyika, yakatumia mabilioni ya fedha zetu. Pia baadaye zoezi kama hilo hilo likafanyika, kwa hiyo, ni kama duplication ya jambo hilo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye eneo la pili, la madeni ya wakandarasi, nimemsikiliza Mheshimiwa Waziri wakati anawasilisha hotuba yake, bado Serikali inadaiwa. Huwa najisikia vibaya sana napodaiwa, wanasema dawa ya deni ni kulipa, kwa nini Serikali hii isiwalipe hao Wakandarasi? Miradi mingi iliyotekelezwa huko nyuma tunadaiwa, iwe kwenye maji, iwe kwenye eneo hili la ujenzi na kadhalika na kadhalika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani Serikali ili kulinda heshima yake ikwepe jambo hili na tunaingia kwenye matumizi ya ziada ya kulipa fedha za hawa wakandarasi kwa kuwa tumekaa na fedha zao. Kwa hiyo, nashauri kama Serikali hii kweli iko makini, kama Serikali hii ni Serikali ya “Hapa Kazi” hebu tuwalipe wakandarasi ili pia pale wanapokosea tuwe na nguvu ya kuwasukuma na kuwasahihisha. Wakati mwingine hawa wakandarasi wanaishia kufanya kazi zetu vibaya kwa sababu tu wanatudai. Kwa hiyo, nataka kushauri, hebu haya madeni ya wakandarasi tuyalipe kwa muda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, ni eneo la zile barabara zilizoko kwenye ngazi ya Halmashauri. Barabara hizi ziko nyingi sana na barabara hizi zinahitaji fedha nyingi kwa ajili ya matengenezo, lakini fedha tunazopelekewa ni kidogo, hazitoshi. Nimesikia hapa ndani Waziri amesema yapo maombi zaidi ya 3,000 ya kupandisha hizi barabara. Nashauri hebu maombi haya yafanyiwe kazi ili hizi barabara kweli ziweze kuchukuliwa na TANROAD ambao wana nguvu kubwa kuliko sisi Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye eneo la kuunganisha mikoa, hili ni jambo la kisera na kwa kuwa ni jambo la kisera linahitaji kuwa ni jambo la kutekelezwa. Iko mikoa mingi ambayo mpaka sasa hivi bado haijaunganishwa; ukiwa Arusha ukitaka kwenda Musoma, inabidi upite nchi ya jirani; ukiwa Arusha ukitaka kwenda Mwanza inabidi upite barabara ndefu ya kupitia Singida na Shinyanga, lakini zipo barabara ambazo unaweza kupita ukafika mapema.
MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante, dakika tano hizo.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.