Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo Kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Kumi na Mkutano wa Kumi na Moja pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Nane na Mkutano wa Tisa

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo Kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Kumi na Mkutano wa Kumi na Moja pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Nane na Mkutano wa Tisa

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA SHERIA NDOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nihitimishe hoja yangu. Napenda kusema nawashukuru sana niseme nawashukuru sana Wabunge kwa kuchangia hoja yetu kwa kuiboresha. Tumepata wachangiaji kumi na moja na nitumie nafasi hii kuwashukuru sana Mawaziri na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuongezea pale ambapo palistahili kuongezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria Ndogo ni sheria muhimu sana. Ninaweza kusema ni muhimu kuliko hata sheria kubwa (sheria mama) kwa sababu kwanza zipo nyingi kuliko sheria mama. Unaweza kukuta sheria mama moja ina Sheria Ndogo kumi au ishirini chini yake. Pia Sheria Ndogo zinaathiri wananchi moja kwa moja ndio zinawagusa kwenye barrier, kwenye majumba yao, biashara zao, usafiri na siku hadi siku ndizo zinazowaathiri katika maisha yao. Kwa hiyo, sheria ndogo ni sheria muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeeleza hapa na Wabunge wamechangia kwa urefu kabisa. Kuna upungufu mkubwa ambao tumeyabaini kwenye sheria hizi ndogo. Sasa nafikiri ni vizuri tukasisitiza kwamba wale ambao tumewakasimu mamlaka ya kutunga sheria ndogo, wizara, halmashauri na mashirika mbalimbali ya umma wawe makini zaidi katika kazi hii ambayo tumewakasimu. Bunge limewakasimu na tunategemea kazi yao itakuwa nzuri, isiwe ya hovyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, wasikiuke Katiba kwa kuwa ipo na wanaijua, kwenye mamlaka hizo kuna wanasheria, kuna wataalam, wanasiasa na wanajua madhara ambayo wakikiuka sheria mama au katiba basi wanakuwa wamesababisha madhara makubwa kwa wananchi. Kwa hiyo, waongeze umakini ili kuondoa adha hiyo ya kuathiri wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii tumeisema mara nyingi sana. Nimekaa Kamati hii mwaka wa tatu huu nikiwa Mwenyekiti na kila nikisimama hapa tunasema rekebisha hiki, rekebisha hiki. Wapo wanaorekebisha lakini wapo ambao hawarekebishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuwashukuru ambao mmerekebisha wengi tu. Mwezi wa pili nilisimama hapa nikatoa Taarifa ya Kamati na moja ya mambo niliyoyasema ni makelele kwenye makazi ya wananchi. Baa zinapiga muziki mpaka asubuhi, kumbi za harusi na sherehe mbalimbali, makanisa na misikiti yanapiga kelele. Baada ya kutoka hapa BASATA na NEMC wakachukua hatua, leo shida hiyo imekwisha. Hawa nawapongeza sana kwa kazi nzuri walioifanya lakini wapo wengine ambao hawafanyi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninamshukuru sana Waziri Mchengerwa wa TAMISEMI ameshawaambia watendaji kwenye Wizara yake waache kuchukulia yale mambo ya business as usual, bora liende, na mazoea. Wajirekebishe na waongeze umakini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wachangiaji kati ya wale kumi na moja tuliowapata wapo ambao wamependekeza. Tatizo hili kubwa inawezekana kwa sababu sheria hizi zinatumika kwanza, kabla ya kuja Bungeni. Mheshimiwa Luhaga Mpina ni mojawapo Mheshimiwa Aida Khenani na wengine. Nafikiri ni hoja ya msingi kwa sababu hizi sheria zinatungwa kule kwenye mamlaka ndogondogo, zinatumika kabla ya kuja hapa kuchambuliwa na zinaadhiri wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni janga kubwa (disaster) mtu akionewa na sheria kwa sababu hana pa kwenda, ukimuendea aliyemuonea anakwambia mimi nina sheria bwana, utampeleka wapi? Anaonewa na sheria ambayo ipo imetugwa na ni sheria halali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaelekea kukubaliana na Mheshimiwa Mpina na Mheshimiwa Khenani kwamba ni vizuri sheria zije kwanza hapa Bungeni, zipitiwe kwanza kabla ya kutumika ili wananchi wasiathirike. Sheria zije kwanza Bungeni zichambuliwe kwenye Kamati, kamati iongezewe uwezo na muda ifanye kazi hii kwa umakini zaidi. Inawezekana sio ngumu kwa sababu, hii nchi sio mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi hii imekaa miaka 60 na kitu ikiwa huru na sheria nyingi zipo. Kwa hiyo, inayokuja ile mara nyingi ina-replace sheria mbalimbali au ina-amend. Kwa hiyo, ikiwa imekuja hapa ikachelewa kule hawatakosa sheria, hakutakuwa na vacuum. Sheria itakuwepo hadi hii tuipitie hapa ikamilike ndiyo iweze kutumika, isitumike kwanza hadi ipite hapa tumalize kuirekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.