Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Kwanza kabisa naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa John Pombe Magufuli, Rais wetu wa Awamu ya Tano, kwa kuunda Baraza zuri, Baraza lenye kuleta matumaini kwa wananchi wote. Nimpongeze Waziri wa TAMISEMI, Waziri wa Utumishi na Naibu wake na wataalam wote ambao wako Wizarani kwa juhudi zao walizoonesha ndani ya muda mfupi huu ambao wametuletea matumaini mapya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo machache naomba niendelee kuishauri Serikali ambayo wamendelea kuyafanyia kazi ili tuendelee kuboresha. Kazi ya Wabunge siku zote ni kuendelea kuboresha yale ya Serikali na kuisimamia kuhakikisha yale ambayo tunayapitisha basi, Serikali iendelee kufuatilia vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja naomba suala la utawala bora. Suala la customer charter ni muhimu sana lirudishwe na huduma ile wananchi wapewe mafunzo, waelimishwe kutokana na suala la customer charter, pia kila mtumishi yale masuala yarudiwe na wananchi wajue kabisa kwamba huduma ambayo wanaenda kuipata kwenye ofisi yoyote au taasisi yoyote wanatakiwa kupata haki gani, lakini muhimu pia muda wa kazi kwamba, ndani ya muda wa masaa nane au ndani ya muda wa kazi wa mtumishi anatakiwa kufanya kazi kiasi gani, ili tuwe na ufanisi, tukifikia huko naamini ufanisi utakuwepo kwa sehemu kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaomba wataalam kwa mfano hawa wa mipango, wengi wasibakie huku ngazi ya Taifa, tunao mmoja mmoja kwenye Halmashauri, Maafisa Mipango wangetakiwa kuwepo ngazi zote, hasa pangekuwa na timu kubwa ndani ya Wilaya ambapo wangeenda mpaka ngazi za vijiji ili kuibua miradi ambayo wananchi wanataka itekelezwe hasa kwenye huu mpango wa TASAF kwa sababu wananchi wakiambiwa tuchangie basi kwa sababu kero ni darasa, watachangia wataomba kujengewa darasa. Kumbe wangekuwa na mipango wangeomba miradi ambayo wangewekeza kwenye ile miradi, ikawapatia kipato na wakajenga darasa, zahanati na hayo mengine yote. Kwa hiyo, suala la mipango liwekewe umuhimu wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, tunaomba suala hili la kumaliza masuala ya watendaji ngazi ya vijiji, kata, wao ni muhimu, ndiyo mahali ambapo pesa zote hizi tutazowekeza asilimia 40 ya maendeleo inaenda kufanya kazi huko. Kwa hiyo, ni jambo muhimu kwamba, awamu hii mmalize hawa wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri alipotoa tamko kwamba mapato yote ya Halmashauri sasa yakusanywe kwa njia ya elektroniki; nakupongeza kwa hilo ni jambo zuri sana. Ombi langu litakuwa moja, kwenye sehemu moja tu kwenye kukusanya ushuru wa mazao, ninaomba hilo sasa lifanyiwe kazi kwa namna yake kwa sababu tukienda moja kwa moja kukusanya ushuru wa mazao kwa kupitia watumishi wetu hatutafanikiwa, kwa sababu leo hii kwanza hatuna watumishi wa kutosha kwa kazi hiyo kwa ngazi zote na ile kazi ni ya saa 24. Ombi lilikuwa ni kwamba kwenye hiyo sehemu moja tu watumike mawakala wa kutumia elektroniki halafu tuelewane na wakala kwamba, asilimia ngapi atakapokusanya, basi Halmashauri ielewane na huyo wakala la sivyo tutajikuta tunapoteza mapato mengi sana kwenye section hiyo moja, mengine yote napongeza ni jambo jema na nina uhakika kwamba, tutapata mapato mengi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba TAMISEMI itusaidie, makampuni mengi ya simu hayalipi kabisa ushuru ule wa huduma kwenye Halmashauri zetu. Tunaomba TAMISEMI kwa niaba ya Halmashauri zote ikusanye ule ushuru halafu mtugawie kwa uwiano siyo kwamba ambaye hana minara asipate. Ile ni haki yetu wote kwa sababu, simu kila mahali tunapiga. Mkusanye zile pesa, badala ya zile pesa kwenda headquarters pale Dar es Salaam kwenye Wilaya moja, pesa yote nyingi inalipwa pale, ni haki yetu wote tupate hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala la hotel levy, kuna suala la hizi tozo mbalimbali kwa mfano ya maliasili, ardhi, zile zikikusanywa na Halmashauri zetu zinachelewa kurudi. Sasa tungeboresha mfumo kwa sababu ni electronic ile tunayokusanya ya Serikali Kuu tuwaachie Serikali Kuu ile ya kwetu tubakinayo kwa sababu, inapoenda mpaka irudi inachelewa sana. Kwa hiyo, jambo hilo kwa sababu, tunaenda na mfumo huu wa TEHAMA ninaomba mlifanyie kazi, ili zile pesa ziende kwenye maendeleo moja kwa moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine muhimu ni kwa ujumla. Kwa sababu pesa nyingi sana itaenda kwenye maendeleo ni Sheria ya Manunuzi. Naomba sheria ile iletwe mapema tuifanyie kazi, tuibadilishe kwa sababu bila hiyo, utaendelea kuhalalisha wizi ambao unafanywa huko kwa kupitia hii Sheria ya Manunuzi kwa sababu gharama zote ni mara mbili au mara tatu. Hizi pesa zote zikienda tukishabadilisha Sheria ya Manunuzi ina maana maendeleo utayaona mara tatu ya hiyo ambayo tunaiona leo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingne ni TEMESA, tunaomba muingalie upya. Kazi ndogondogo ambazo hata dereva anaweza kubadilisha fan belt inabidi upeleke TEMESA! Fan belt ya shilingi 90,000 kwenye cruiser, dereva anaweza kufunga mwenyewe, unachajiwa karibu mpaka shilingi 500,000! TEMESA ni kero, TEMESA ni moja katika majipu ambayo yanatakiwa yatumbuliwe moja kwa moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi kazi ndogondogo za service ya magari na nini, naomba maeneo penye VETA tungewapa VETA ili wale wanafunzi wa pale kwa sababu, wana wakufunzi wapate mafunzo na pia watatusaidia ku-service haya magari kwa bei ya kawaida kabisa. Kwa hiyo, huku tutasaidia kwenye sekta ya elimu, lakini pia itakuwa tumepunguza gharama nyingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwa sababu tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda, ninaomba Serikali ikae kwa sababu sehemu kubwa itakuwa inahusika na utawala bora na pia, masuala ya TAMISEMI, hizi regulatory boards. Hizi ndiyo zimekuwa kero na ni matatizo makubwa, tozo nyingi. Hata tukiwekeza kwenye viwanda, siyo kwamba watu hawapendi kuwekeza. Wala huhitaji kutafuta mitaji nje, Watanzania wana uwezo wa kuwekeza, lakini wenye kupiga mahesabu, utaweka kiwanda bado itakuwa rahisi wewe kutoa vitu nje kwa gharama nafuu kuliko hapa kwa sababu, mfano mzuri ni kwenye ngozi; tumepandisha ngozi asilimia 90 ku-export, korosho tumepandisha, lakini bado inaenda ghafi kwa sababu ukizalisha hapa badala ya asilimia 90 utakayolipa export levy unajikuta unalipa asilimia 125 kwa sababu ya tozo mbalimbali na kodi ambayo unatakiwa kulipa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuelekee huko Serikali nzima ikae, m-regulate, mhakikishe kwamba, huko tunakoelekea tusije tukakwama kwa sababu ya urasimu na mambo mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa afya nipongeze kazi inayoendelea, kazi inayofanyika ni kubwa na juhudi zimeonekana. Tutakachoomba kuna vitu wananchi mahali ambapo wamejitahidi na Halmashauri zetu vituo vya afya, zahanati, mahali ambapo wamewekeza vizuri, kuna kada za watumishi ambao hawajapangwa kwenda ngazi hizo; kwa mfano Kituo cha Afya Magugu, tuna uwezo sasa hivi kimefanana kabisa na hospitali, sasa tunaomba mtupangie watumishi ambao wataweza kuendesha kituo cha afya hicho kwa sababu vifaa vingi tayari tumeweza kununua. Kwa hiyo, maeneo ambapo wananchi wanajitahidi ngazi ya kijiji, zahanati na vituo vya afya, basi mtuunge mkono.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala jingine ni suala la elimu. Mimi ningeomba Serikali ichukue hatua zaidi, tuna vyuo vingi sasa hivi na shule nyingi na nyingi ni private zinadahili watu ambao hawana vigezo, baadae shule hizo hazijasajiliwa, badae tunakuja kupata kesi. Moja ni kama hii St. Joseph. Sasa tayari inakuwa mpira kwa kila mtu. Sisi tumewekeza kwa wanafunzi wetu tumewachangia huko wengi na kwa nini wale Wakaguzi kuanzia siku ya kwanza kama walikosea hawakuchukuliwa hatua?
Kwa hiyo, ni jambo ambalo naomba mlifanyie kazi, wanafunzi wako 504, kama walikuwa hawana vigezo wamefika mpaka mwaka wa nne tulikuwa wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wale wote waliohusika wapelekwe mahakamani. Kama ni upande wa Serikali, kama ni mwenye chuo, wote wafikishwe mahakamani, muda huu hawa Watanzania waliopoteza hauwezi kwenda bure. Kwa hiyo, naomba kwenye hilo Serikali ijitahidi na tulifanyie kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande mwingine kulikuwa na suala la maji. Mimi naomba Serikali iwekeze zaidi kwa wataalam kwenye upande wa maji vijijini. Huko katika Halmashauri zetu hatuna wataalam wa kutosha. Pesa inayoenda huko ni nyingi, miradi mingine inakuwa chini ya viwango kutokana na kukosa wataalam, pia ninaendelea kuishauri, kama nilivyosema juzi, kwenye ile shilingi 200 niliyopendekeza iongezwe kwenye mafuta, tena shilingi 70 nyingine iende kwenye maji, shilingi 70 kwenye umeme, shilingi 50 kwenye suala la utafiti na shilingi 10 kwenye suala la mazingira ili tatizo la maji huko vijijini liweze kuisha.
Mheshimiwa pia tunaomba kwamba Sekretarieti ya Utumishi katika Ofisi ya Rais waboreshewe ili waweze kuwa katika kanda zote, waweze kufanya kazi na namna ya kushauri Halmashauri zetu na uko Wilayani ili tuweze kuwa na watumishi bora na wao pia wawe na jukumu hilo la kutoa elimu hiyo ya mambo ya customer chater ili kwenda vizuri, muhimu kwamba watumishi wetu wangekuwa wanatoa hizo huduma vizuri ninaamini kabisa kwamba Tanzania tungesonga mbele na huduma ingekuwa nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la TASAF, ninaipongeza Serikali kwa mradi mzuri, lakini bado naendelea kusema mtuletee wataalam wa mipango wakati inapofika ngazi ya kuanzisha miradi, tuwe na wataalam watakaoibua miradi huko chini ili tuweze kufanya vizuri zaidi, wananchi wawe na miradi ambayo itawapatia kipato na uchumi ambao wao baadaye watachangia katika miradi mbalimbali. Huko ndiyo tuanzishe mfumo ambao tuna mifuko mingi ambayo tunapeleka huko, kwa mfano Mfuko wa Wanawake na Vijana, hii ya TASAF zote tuziratibu ziwe moja ili maendeleo yaonekane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo naunga mkono hoja asilimia mia moja. Ahsante.