Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo Kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Kumi na Mkutano wa Kumi na Moja pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Nane na Mkutano wa Tisa

Hon. Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo Kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Kumi na Mkutano wa Kumi na Moja pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Nane na Mkutano wa Tisa

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji leo hii. Awali ya yote natumia fursa hii kumshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Rais wa Zanzibar, kwa kazi kubwa wanazozifanya katika kuwatumikia wananchi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe kwamba, miongoni mwa majukumu mama na ya msingi ya Kamati ya Sheria Ndogo, ni kufanya uchambuzi wa Sheria Ndogo zinazowasilishwa Bungeni pamoja na kuangalia utekelezaji wa Maazimio ya Bunge. Miezi michache iliyopita nyuma, Bunge hili tukufu liliazimia jumla ya dosari 83 ziende zikarekebishwe kutokana na athari zinazowakuta wananchi. Wakati Kamati ya Sheria Ndogo ilipofanya mapitio ya utekelezaji wa maazimio yale, imebaini kwamba kumekuwa na dosari 19 ambazo zimeshindwa kurekebishwa licha ya kuwa baadhi ya Wizara husika tayari walikuwa wameshatangaza marekebisho yao katika Gazeti la Serikali. Ukiangalia ndani, dosari zile hawakuzirekebisha kama ilivyoazimiwa na Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni sawa na kusema kwamba, 22.89% ya Maazimio ya Bunge yaliyotolewa toka tarehe 8 Februari, 2023 hadi kufika tarehe 14 Agosti, 2023, wakati Kamati ya Sheria Ndogo ilipokutana katika vikao vyake vya kupokea taarifa ya utekelezaji, maazimio hayo hayakuwa yametekelezeka. Miongoni mwa Wizara ambazo tulibaini zimeshindwa kutekeleza maazimio hayo kwa kiwango ambacho Bunge liliazimia, ni Wizara ya TAMISEMI. Tulikuja kubaini walikuwa na dosari 16 ambazo wameshindwa kuzitekeleza. Wizara ya Madini na wao walikuwa na dosari tatu ambazo zimeshindwa kutekelezwa kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inatupa picha gani? Jambo hili la kushindwa kutekeleza Maazimio ya Bunge inatoa taswira kwa wananchi kwamba, Wizara hizi zimeshindwa kutii maagizo ya Bunge au zimeshindwa kutekeleza kwa sababu ya kuona kwamba Bunge hili halina nguvu na mamlaka ya kuwalazimisha wao kutekeleza jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kitendo ambacho hakiwezi kuvumilika, kuacha kutumika kwa dosari hizi katika mazingira ya kawaida, kwa sababu kuendelea kutumika kwa dosari hizi ni sawa na kuyakumbatia madhara yanayotokana na dosari ya sheria hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano wa dosari ambazo Bunge liliazimia ziende zikarekebishwe lakini hazikuweza kurekebishwa. Unaposoma Sheria ya Usafi wa Mazingira ya Wilaya ya Misungwi ya mwaka 2023, Ibara ya 22(2), Kifungu hiki kimekuwa na mkanganyiko mkubwa sana wa adhabu, unapoenda kusoma kifungu cha 36(1). Kifungu cha 22(2) kinatoa adhabu ya jumla kwa mtu yeyote yule atakayekiuka masharti yoyote ya Kifungu cha Sheria. Kinatoa adhabu ya kupigwa faini isiyozidi shilingi 200,000 au kifungo kisichozidi miezi 12. Mkanganyiko unatokea utakapoenda kusoma Ibara ya 36(1) ya Kanuni hii ambapo hicho kipengele kinasema; “Mtu yeyote atakayefanya kosa lolote katika sheria hii, atapigwa faini isiyopungua shilingi 200,000 au kifungo kisichopungua miezi sita.”

Mheshimiwa Naibu Spika, huu ni mkanganyiko katika utekelezaji wa adhabu unaotokana na sheria. Kwa sababu, wakati ambapo wananchi wanaenda kuadhibiwa kwa sheria hii, changamoto itakayotokea ni kipengele gani cha sheria kifuatwe. Aidha, 36(1) au 22(2). Huu ni mkanganyiko usiokuwa wa lazima na mkanganyiko huu unaendelea kuwepo na kuwaathiri wananchi, kwa sababu tu ya mamlaka inayohusika kushindwa kutekeleza Maazimio ya Bunge, kwa sababu, Bunge tayari walishawaelekeza waende wakaondoe dosari hizi lakini hawakufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge hili ndiyo chombo cha uwakilishi wa wananchi, haliwezi na halitoweza kuacha mamlaka yake ya kutengeneza sheria, yatumike kwa namna itakayoweza kuwakanganya wananchi katika kutekeleza majukumu yao. Dosari yoyote inayotokana na athari ya kushindwa kutekeleza au kushindwa kutekeleza kwa muda Maazimio ya Bunge, haikubaliki kuachwa kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge hili ndiyo chombo cha wananchi, lakini pia ndiyo sauti ya wananchi. Ikiwa kama ndiyo sauti ya wananchi, Bunge haliwezi kukaa kimya kwa zile dosari ambazo zinaendelea kuwaumiza wananchi wetu. Ndiyo maana Bunge hili lilitoa maazimio ya kwamba, dosari hizi 19 ziondoshwe ili zisiendelee kuleta madhara kwa wananchi. Kusema ukweli hakuna hata kimoja kilichofanyika, kwa mujibu wa Taarifa ya Kamati yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni uoni wa Kamati kwamba, Bunge hili litazuia utumikaji wa dosari hizi 19, zilizokuwemo katika Sheria Ndogo kumi ili zisiendelee kutumika kwa wananchi, kwa sababu, kama Bunge hili litaachilia kuendelea kutumika kwa dosari hizi, ni sawa na Bunge hili kuridhia kuendelea kukumbatia athari zinazowapata wananchi zinazotokana na Sheria hizi Ndogo. Vile vile, itatafsirika ya kwamba Bunge hili limekubali mamlaka yake iliyokasimu kwa mamlaka nyingine zakutunga sheria, zitumike kinyume na utaratibu unaokusudiwa ambao ndiyo dhamira halisi ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitendo chochote kinachotokana na madhara yanayotokana na dosari hizi ambazo Bunge limedhamiria ziondoshwe, hakitavumiliwa na hazitaachwa kuendelea kutumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema kitu kimoja kwa Waheshimiwa Wabunge wenzangu na Watanzania kwa ujumla, si udhaifu katika maisha kukubali kukosolewa, kuambiwa na kuelekezwa kwa maslahi ya wengi au wachache, ikiwa jambo lina maslahi kwa Taifa hili. Ni kweli kabisa makosa tunayo katika kuelekezana. Wengine wakali, wabishi na wengine wagumu kuelewa. Kibaya zaidi, wapo miongoni mwetu. Kupata mawazo yao, fikra zao, akili zao pamoja na elimu yao, zionekane hakuna wa kuzipinga kutokana na jinsi wao walivyoelimishwa. Kitendo cha kuwakosoa au kuwaelekeza, kwao wao ni sawa na udhaifu ambao Mungu kawajalia na hawakustahiki kuwa nao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge ndicho chombo chenye mamlaka ya kusimamia utungaji wa sheria zote za nchi hii. Kitendo cha kukasimu mamlaka yake kwa Wizara nyingine, haimaanishi kwamba Bunge halikuwa na uwezo wa kutengeneza sheria hizo, lakini limetekeleza majukumu yake ya Kikatiba ya kukasimu madaraka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaambie Waheshimiwa Wabunge wenzangu, leo hii ni vizuri tukaazimia na kuzitaka Wizara ambazo zimeshindwa kutekeleza Maazimio ya Bunge hili tukufu, zirekebishe kasoro hizo mara moja, ahsante sana. (Makofi)