Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika bajeti hii muhimu. Napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya katika nchi yetu ya Tanzania. Hakika wananchi walio wengi wanamuunga mkono katika juhudi anazozifanya na wengi wanasema Wabunge tuweze kumuunga mkono katika shughuli zake anazozifanya hasa katika nchi hii ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo anaifanya katika Taifa hili, aliweza kupata fursa ya kutembelea Mkoa wetu wa Geita, kwa kweli mambo aliyofanya ni mambo makubwa tunaimani kubwa kwamba katika utawala huu tutaweza kuona mabadiliko makubwa sana katika nchi yetu, hasa katika maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri, Ofisi ya Rais – TAMISEMI pamoja na Utumishi na Utawala Bora kwa jinsi ambavyo wanafanya kazi zao vizuri. TAMISEMI tunaona jinsi ambavyo wanaangalia changamoto mbalimbali ambazo zinakabili hasa katika Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Wote tunafahamu kwamba Majimbo mengi tunategemea sana TAMISEMI kwa ajili ya maendeleo mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza katika sekta ya elimu, nilivyokuwa nikiangalia ile hotuba inaonesha jinsi ambavyo changamoto bado ni kubwa hasa katika upande wa elimu. Tumeona mwaka huu watoto wengi wamejiandikisha hasa darasa la kwanza, lakini miondombinu ni changamoto kubwa. Niiombe Serikali sasa iangalie uwezekano wa kuwekeza zaidi kwenye miundombinu ya madarasa, kwenye nyumba za walimu, yaani katika kila hatua, ili tuweze kuona kwamba watumishi ambao ni walimu na watumishi wengine wanafanya kazi zao kwa amani na utulivu kwa sababu wana sehemu nzuri ambapo wanaishi wanaenda kufundisha kwa amani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika upande wa elimu ninafahamu kwamba kweli Wizara imejipanga vizuri, nimeona jinsi ambavyo mmekusudia kujenga nyumba 183 katika Halmashauri 103. Ninapenda kujua je, Halmashauri yangu ya Geita imo katika mpango huo? Kama haimo naomba sasa Wizara iangalie namna ya kuweka pia Halmashauri yangu kwa sababu changamoto ni kubwa sana katika Halmashauri. Watumishi wa Halmashauri ambao ni walimu na watumishi mbalimbali kwa kweli wana changamoto kubwa sana na ndiyo maana naomba katika huu mpango wa nyumba 183 ambazo zinakaa watumishi sita kila nyumba, basi iwe pia katika Mkoa wangu na katika Wilaya yangu, Halmashauri ya Wilaya ya Geita ninaomba mpango huu pia uwe kipaumbele ili tuweze kuwawezesha watumishi waweze kufanya kazi zao vizuri kwa ajili ya ufanisi wa kazi zetu katika Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika upande wa elimu, watumishi wengi bado wanaidai Serikali, wanadai mishahara, wengine wamepandishwa madaraja lakini hawajalipwa mishahara wengine, wana changamoto aina mbalimbali. Napenda kusisitiza Serikali iangalie namna ya kuweza kuwalipa hawa watumishi ambao wana madai mbalimbali. Walipoona kwamba, tumekuja kwenye Mkutano huu wa Bajeti wengi wamenipigia simu, hasa katika Halmashauri yangu ya Geita na Jimbo la Busanda, wanasema sasa tunaomba kwa kweli jambo hili ulisemee. Naomba kama ni uhakiki wao tayari umeshafanyika, kilichobaki ni kulipwa tu madai yao. Ninaomba Serikali awamu hii ihakikishe watumishi wanalipwa madai yao vizuri kwa uhakika ili waweze kufanya kazi zao wakiwa na morali kubwa kwa sababu hawaidai Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, watumishi wengi ambao wanastaafu wana changamoto kubwa, wengi hawapati mafao yao. Nichukue fursa hii kuitaka Serikali iangalie namna ya kuweza kulipa madai haya hasa ya watu ambao wamestaafu, wengi wanafuatilia wanaenda pale wanakuta hawajawekewa fedha zao kwenye akaunti, hivyo niiombe Serikali, iweze kulifanyia kazi suala hili, watumishi waweze kulipwa stahili zao, hasa ambao wamestaafu waweze kupata haki zao kwa amani ili waweze kuendelea na maisha yao vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nizungumzie kuhusu TASAF. Nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa jinsi ambavyo imeanzisha utaratibu wa TASAF wa kuweza kuwajali wanyonge katika shida zao na kuwapa fedha. Jambo hili ni jema na litailetea baraka Serikali kwa sababu tumeweza kuwajali wanyonge. Nilichokuwa ninaomba sasa ni vile vijiji ambavyo hawajapata mpango huu nao wanahitaji waweze kuwepo katika mpango huu wa TASAF ili tuweze kuwasaidia hasa watu wanyonge ambao wanahitaji huduma hii ambayo ni ya muhimu sana.
Kwa hiyo, niiombe Serikali kwamba TASAF III ambayo imekusudia kuweza kusaidia wanyonge iongeze wigo, iangalie kata na vijiji mbalimbali, kwa sasa haifanyiki katika kila kijiji kwa hiyo, Serikali iangalie uwezekano kila kijiji watu wenye mahitaji maalum, watu ambao wana shida mbalimbali tuweze kuwaweka kwenye utaratibu wa TASAF. Hii itawezesha wananchi kuishi maisha bora na kuweza kufanya kazi zao, pia ambao hawana uwezo wataweza kusaidia watoto wao kwenda shule, lakini vilevile wataweza kuchangia katika shughuli mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika utaratibu mpya ambao Serikali imesema italeta shilingi milioni 50 kwa kila kijiji. Kama ni jambo ambalo Serikali imefanya jambo kubwa ni hili la kupeleka shilingi milioni 50 kwenye kila kijiji. Hizi shilingi milioni 50 watu wengi wanazisubiri, hasa vijijini, niiombe Serikali iweke utaratibu mzuri, mnafahamu hizi shilingi milioni 50 itakuwa ni ukombozi kwa wananchi wanyonge ambao wako vijijini. Wote ni mashahidi kulikuwa na mabilioni ya JK ambayo wengi waliweza kufaidika na bilioni hizo.
Kwa hiyo, hata katika hizi shilingi milioni 50 nilikuwa naiomba Serikali ijipange vizuri namna ya kuweza kuzipeleka kule la sivyo, hizi hazitaweza kunufaisha wananchi wenyewe wa hali ya kawaida, kwa sababu hizi shilingi milioni 50 kwanza watu ni wengi, sasa namna ya kwamba nani achukue hizi afanyie nini huo ni mtihani. Kwa hiyo, niiombe Serikali iweke utaratibu mzuri, lakini kikubwa iwekeze kwenye elimu, bila ya elimu haiwezekani kuweza kuzifanyia kazi hizi shilingi milioni 50 na wakaweza kuleta mnaendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe Serikali iwekeze kwenye elimu, ikiwezekana kupitia SIDO ambao wanatoa mafunzo mbalimbali ya ujasiriamali. Hizi shilingi milioni 50 ni jambo ambalo wananchi wamelifurahia na wengi wanasubiri jambo la msingi wekezeni sasa katika elimu, ili wananchi waweze kuelewa namna ya kuzitumia vizuri fedha hizi kwa ajili ya manufaa na familia zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika suala la kiutawala, maeneo ya utawala, napenda kuomba sasa kwamba katika Jimbo langu pale Katoro ni mji mkubwa, kwa sasa hivi ni Mamlaka ya Mji Mdogo, naomba Serikali ipandishe hadhi Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro iwe Mamlaka ya Mji kutokana na hali halisi, kuna watu wengi, yani tunahitaji kwa kweli, kufanya mipango miji mahali pale. Kwa hiyo, naomba sana wakati unapo-wind up nipate kusikia namna ambavyo mtaweza kupandisha hadhi Mji wa Katoro kuwa Mamlaka ya Mji, ni Mamlaka ya Mji Mdogo kwa sasa. Kwa hiyo, niiombe Serikali iliangalie, ilitilie maanani suala hili kwa sababu tumekusudia kupeleka maendeleo kwa wananchi wenyewe tunapoongeza Wilaya au Halmashauri, nina uhakika kwamba, tunaweza kupeleka maendeleo kwa wananchi wenyewe ili waweze kupanga shughuli zao kwa maendeleo ya wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa miundombinu, barabara za Halmashauri nyingi hazipitiki, nichukue fursa hii kuiomba Serikali mwaka huu iwekeze fedha nyingi za kutosha kwa ajili ya kutengeneza barabara za vijijini. Nasema hivyo kwa sababu wananchi wanazalisha lakini usafirishaji unakuwa ni mgumu sana. Unakuta kati ya kata na kata hazipitiki vizuri. Naiomba Serikali ijitahidi kwa awamu hii, zile bajeti ambazo zimewekwa kwenye bajeti zake tuhakikishe fedha hizi zinafika kule kwenye Halmashauri, ili barabara ziweze kutengenezwa, suala la maji na katika huduma zote ni muhimu liweze kufanyiwa kazi inavyostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa ni kuhusu suala la afya. Nimeangalia katika bajeti ya Serikali, inaonesha jinsi ambavyo Serikali imejipanga kujenga vituo vya afya kwenye kila kata, kujenga zahanati kwenye kila kijiji; nalipongeza suala hilo vizuri kabisa, naiomba Serikali sasa katika yale iliyozungumza iweze kuyafanyia kazi. Nikiangalia katika jimbo langu, jimbo ambalo lina kata 22, kuna vituo vya afya vinne tu. Bado kazi ni kubwa sana ambapo Serikali inahitajika ifanye kazi ya ziada ilete fedha, ihamasishe na wananchi tuko tayari kufanya kazi pamoja na Serikali iliyoko madarakani kuhakikisha kwamba, tunapata maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, nikiamini kwamba mtaenda kuyafanyia kazi yale yote niliyoyazungumza.