Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya nadra kuniweza na mimi kuchangia katika hotuba ya Waziri wa Serikali za Mitaa, TAMISEMI, pamoja na Utawala Bora, pia ningependa kumpongeza Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mahali popote kwenye mabadiliko kibinadamu, lazima washtuke, ndiyo sababu namuomba Rais kazi anayoifanya ni nzuri sana na ukiona watu wanaanza kushtuka, penye changes yoyote kibinadamu lazima watu washtuke na kazi anayoifanya Mheshimiwa Rais ni nzuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais na Baraza lake la Mawaziri, kazi mnazozifanya Mawaziri ni nzuri sana, mmeleta mabadiliko kwenye nchi hii na wananchi wana imani kubwa sana na ninyi.
Katika ukurasa wa tatu Waziri wa TAMISEMI amejaribu kuainisha kazi za TAMISEMI ikiwemo usimamizi wa Halmashauri, vilevile, na kusimamia maendeleo vijijini. Kwa kweli Wizara mnafanya vizuri sana na tumeona Waziri pamoja na Naibu Waziri, jinsi mnavyofuatilia maendeleo na Naibu Waziri umetembelea Jimbo langu umekagua miradi na kweli nakushukuru sana na ninakuomba urudi tena na tena.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jukumu la Mbunge ni kushauri, pale unapoona kidogo kunahitaji ushauri ili Serikali iweze kufanya kazi zake vizuri. Katika suala la maji, kwenye Jimbo langu la Mbeya Vijijini toka mwaka 2010 miaka zaidi ya mitano sasa hivi, tulikuwa tumepewa miradi karibu ya bilioni nne, zimelipwa bilioni 2.5; katika miradi yote hiyo hakuna hata mradi mmoja unaotoa maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI pamoja na Naibu wako, jaribuni kuliangalia hili kwa sababu katika kazi zenu za kusimamia hizi Halmashauri pamoja na Utawala Bora, kuangalia Serikali imepeleka bilioni nne, Mbeya Vijijini wananchi wake miaka zaidi ya tano hawapati maji. Jana wenzangu wamekwenda kutembelea hiyo miradi wamekuta pesa zimelipwa shilingi bilioni 2.5 lakini makandarasi hawapo site. Kwa hiyo, nakuomba sana ndugu yangu Waziri ujaribu kuifuatilia hiyo miradi ya vijiji vya Swaya, Horongo, Izumbwe, Iwindi, Mbawi na Mshewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Waziri, katika Halmashauri yetu ya Mbeya tuna tatizo kubwa sana la maji, pamoja na kuwa tuna vyanzo vingi vya maji, ikiwemo vyanzo vile ambavyo vinapeleka maji katika Jiji letu la Mbeya, lakini hivyo vyanzo havinufaishi Halmashauri yetu. Kuna tatizo kwenye kata ya Mjele, hakuna maji kabisa na nikiangalia katika makabrasha haya sioni kama zimetengwa pesa zozote katika maeneo yote ya kata na vijiji vile ambavyo havina maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilitaka kuchangia, ni suala la usimamizi wa maendeleo ya Miji, ambayo iko kwenye ukurasa wa 16 wa hotuba ya Waziri. Upimaji wa ardhi ni mpango mzuri sana kwa sababu ardhi ndiyo utajiri wa Watanzania kwa ujumla, lakini kwa kiasi kikubwa ardhi hasa vijijini ilikuwa haijapimwa, wananchi hawajatumia ule utajiri wa ardhi kwa ajili ya maendeleo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba sana mipango miji ipate msisitizo na msukumo wa juu na kuhakikisha kuwa Miji midogo ambayo inajitokeza vijijini na inakuwa kwa haraka; iweze kupimwa. Maeneo yaweze kuainishwa ya mifugo, viwanda, vilevile viwanda vidogovidogo kwa ajili ya vijana wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kama Mji Mdogo wa Mbalizi hatuna hata sehemu ya kujenga maeneo ya ofisi za Serikali, hospitali, vituo vya polisi, vilevile kutokana na ongezeko la watu, kuna uhaba mkubwa wa maeneo ya ujenzi wa makazi, kwa sababu kadri ya Jiji la Mbeya linavyokua na watu wanaongezeka, ongezeko hilo linapumulia kwenye Halmashauri ya Mbeya. Kwa hiyo, nakuomba sana Serikali izingatie kupima haya maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri imeleta ombi Serikalini kwa eneo ambalo lilikuwa linamilikiwa na Tanganyika Packers ili hilo eneo ambalo liko ndani ya Mji sasa hivi ipewe Halmashauri na wananchi wapate fidia kwa wale ambao walikuwa hawajapata fidia zaidi ya miaka 40 na Tanganyika Packers, waweze kufidiwa na hili eneo ikishapewa Halmashauri liweze kupimwa viwanja na wale wananchi waweze kupata fidia, badala yake Halmashauri imetenga eneo kwa ajili ya mifugo na kwa ajili kujenga kiwanda cha nyama, kwenye kata yetu ya Mjele ambayo ina mifugo mingi na ardhi nzuri kwa ajili ya shughuli za ufugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilitaka kuchangia, ni suala la barabara za vijijini. Kama alivyosema kwenye hotuba yake ukurasa wa 20 miundombinu ni muhimu sana kwa maendeleo ya kilimo. Tunazalisha sana mazao kwenye Halmashauri yetu ya Mbeya ikiwemo viazi, mbao, kahawa, pareto na mazao mengine, lakini barabara za vijijini haziko katika hali nzuri. Kwa hiyo, naomba hilo lifikiriwe katika bajeti yako kwa namna gani wakati tunaangalia kukuza uzalishaji wa kilimo tuangalie na kuboresha miundombinu ya barabara zetu za vijijini zina hali mbaya sana, zikiwemo zile barabara ambazo zinaunganisha vijiji kwa vijiji kwenye kata zetu kama za Isuto, Ilungu na kadhalika pia zile barabara ambazo zinaunganisha Mkoa wetu wa Mbeya na Mkoa wa Njombe, kama barabara ya Isyonje kwenda Kikondo, kwenda mpaka Kitulo, Makete na Njombe. Vilevile tuna barabara ya Mbalizi, Mjele kwenda mpaka Mkwajuni ambayo inaunganisha na Mkoa mpya wa Songwe, hizi barabara haziko katika hali nzuri ungejaribu kuangalia namna gani ziweze kuboreshwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilitaka kulichangia kwa siku ya leo ni suala zima la elimu. Suala la elimu nashukuru sana kwa mpango wa elimu bure kwa shule za msingi na sekondari; limehamasisha na watu wamepata mwitikio mzuri, lakini kunachangamoto ndogo ndogo ambazo inabidi tuziangalie na kuzitatua. Changamoto hizo ni pamoja na upungufu wa waalimu kwenye shule zetu za vijijini, zote za sekondari pamoja na za msingi. Kwa shule za sekondari upungufu mkubwa uko kwenye walimu wa sayansi. Kwa hiyo, naomba uangalie hilo, tunapohamasisha elimu tuweze kuhakikisha kuwa elimu inakuwa bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilitaka nichangie ni suala la afya. Wananchi wa Halmashauri ya Mbeya kama ilivyo kwa Halmashauri zingine wamejitokeza sana kujenga zahanati kwa kila kijiji na vituo vya afya kwenye kata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo majengo ambayo mengine yamejengwa kwa muda mrefu sana…
MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umeisha naomba ukae.
MHE. ORAN M. NJENZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga hoja kwa asilimia mia moja. Naomba mchango wangu wa maandishi uingizwe kwenye Hansard.