Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema kwa kutujalia afya njema na kutuwezesha kukutana katika Bunge hili tukufu la bajeti hii kukamilisha kazi tuliyoianza jana tarehe 22 Mei, 2023 ambapo niliwasilisha hoja hii.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii pia kukushukuru wewe binafsi, Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wenyeviti wote wa Bunge kwa jinsi mlivyoliongoza na kusimamia majadiliano ya hoja hii. Aidha, nachukua fursa hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote wa Bunge letu Tukufu kwa kuwa wazi na kutoa maoni na michango yao ya kina wakati wa majadiliano haya. Ninawathibitishia kwamba michango yenu yote tumeichukua kwa uzito mkubwa na kwenda kuifanyia kazi ili kuendelea kuleta ufanisi wa utekelezaji wa majukumu ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Spika, kipekee naomba nimshukuru Mwenyekiti wetu wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Mheshimiwa Selemani Moshi Kakoso na Waheshimiwa Wajumbe wote wa Kamati kwa hoja nzuri zilizotolewa na Kamati yake. Nakiri kwamba hoja hizo ni muhimu sana kwa maendeleo na ukuaji wa sekta ya ujenzi na uchukuzi hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliyochangia katika bajeti yangu. Waheshimiwa Wabunge 75 wamechangia wakati wa majadiliano ya hoja hii ambapo Waheshimiwa 67 wamechangia kwa kuongea na Waheshimiwa nane wamechangia kwa maandishi. Waheshimiwa Wabunge, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja kuu zilizowasilishwa katika majadiliano haya ni kama ifuatavyo:- Kwanza kabisa ni ujenzi na ukarabati wa barabara mbalimbali nchini ambayo imezungumzwa kwa kina Mheshimiwa Naibu Waziri anayesimimia Sekta ya Ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili lilikuwa ni utekelezaji wa miradi kwa utaratibu wa EPC + Finance ambao leo ndiyo mpango mzima katika Bunge letu. Hii imezungumzwa kwa kina na Mheshimiwa Naibu Waziri anayesimamia sekta ya ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, masuala ya fidia kwa wananchi waliyoathirika na ongezeko la upana wa eneo la hifadhi ya Barabara. Kuna suala la ongezeko la gharama ya miradi ya barabara (variation) kwenye miradi ya barabara, kuna suala la ushirikishwaji wa sekta binafsi katika uendeshaji na uendelezaji wa bandari zetu hasa Bandari ya Dar es Salaam. Pia kuna suala la marekebisho ya Sheria ya Reli ya TAZARA na Reli ya TRC ambalo limezunguzwa kwa kina na Mheshimiwa Naibu Waziri anayesimamia sekta ya uchukuzi.

Mheshimiwa Spika, la saba usimamizi, uendeshaji na uendelezaji wa viwanja vya ndege ambayo imezungumzwa kwa kina na Mheshimiwa Naibu Waziri anayesimamia sekta ya uchukuzi. Kuna hoja nyingine ya ukamilishaji wa ujenzi wa Reli ya SGR na kuanza kutoa huduma kwa vipande vilivyokamilika; na hii imeshazungumzwa; na kuna umiliki wa Shirika letu la Ndege la Air Tanzania; na mwisho, kuna suala la ujenzi na ukarabati wa meli katika Ziwa Tanganyika ambapo na yenyewe imeshazungmzwa na Mheshimiwa Naibu Waziri anayesimamia sekta ya uchukuzi.

Mheshimiwa Spika, muda mchache uliopita kama nilivyosema Waheshimiwa Naibu Mawaziri wa Wizara yangu wamemaliza kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge kwa kuzingatia maeneo ya kisekta kwa ufasaha na weledi mkubwa, ahsanteni sana Waheshimiwa Naibu Mawaziri, ninashukuru sana kwa jinsi ambavyo mmejibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge na mimi nitajaribu kujibu hoja chache zilizobakia. Aidha, naomba kulihakikishia Bunge lako tukufu kwamba Wizara itajibu hoja zote za Waheshimiwa Wabunge kwa maandishi na kuziwasilisha Bungeni kabla kuhitimisha kwa Mkutano wa Bunge hili la Bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nianze kuhitimisha hoja yangu kwa kutoa ufafanuzi wa kiujumla kwa baadhi ya hoja zilizojitokeza kwenye maeneo makubwa yaliyojitokeza. Kwanza kwenye sekta ya uchukuzi; hoja kubwa ambayo imejitokeza kwenye mjadala wetu huu ni ushirikishwaji wa sekta binafsi katika uendeshaji na uendelezaji wa bandari nchini.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge takribani 80% waliochangia sekta ya uchukuzi wamejikita zaidi kwenye ushirikishwaji wa sekta binafsi kwenye uendeshaji na uendelezaji wa Bandari ya Dar es Salaam. Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia wamekubaliana na hoja hii na wengine wamechangia kwa hisia kali sana na wamesema tumechelewa kuleta sekta binafsi kwenye uendeshaji na uendelezaji wa Bandari ya Dar es Salaam. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge tumewasikia, Serikali tumewasikia tunaenda kulifanyia kazi mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa wamefanya hivyo kwa sababu wanajua Bandari ya Dar es Salaam ndio lango kuu la uchumi wa nchi yetu. Asilimia 37 takribani trilioni 7.78 ya makusanyo ya mapato ya kiforodha ya TRA yanakusanywa kwenye Bandari ya Dar es Salaam. Hili ni jambo kubwa na hili ni jambo muhimu na lazima tulisimamie kwa nguvu zetu zote. Aidha, mara nyingi Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amesema kwamba bandari inaweza kuchangia asilimia kubwa sana ya bajeti ya nchi yetu kama tutaisimamia vizuri na kwa uadilifu mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niwapitishe haraka kwa utendaji usioridhisha wa Bandari ya Dar es Salaam; TPA mwaka 2015/2016 ilihudumia mizigo tani 15,670,000; na mwaka 2020/2022 ilihudumia takribani mizigo tani 20,730,000 sawa na ongezeko la asilimia 30.5. Kiwango hiki kinaonekana ni kikubwa ambacho ni wastani wa ongezeko la asilimia 4.3 lakini ni kidogo kutokana na mpango mkakati wa TPA ambayo ilisema kwamba lazima ongezeko la bandari la mizigo liwe kati ya asilimia 10 mpaka asilimia 12.9 kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, kuna sababu ambazo zimechangia kutofikia lengo hili; sababu ya kwanza ni changamoto ya uendeshaji. Sababu ya pili kubwa ni changamoto ya ucheleweshaji wa mizigo pale nangani Bandari ya Dar es Salaam. Meli inakuwa-charged demurrange charge ya takribani dola 25,000 kwa siku ikichelewa na gharama hizi zote zinakwenda kwa mlaji yaani mimi na wewe.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya tatu ni changamoto ya uwekezaji mdogo kwenye ununuzi wa mitambo, bandari zozote ni lazima uwe na mitambo ya kisasa na mitambo mikubwa sana.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya nne ni usimikaji wa mifumo ya TEHAMA ambayo imesababisha ucheleweshaji mkubwa wa utoaji wa mizigo bandarini;na changamoto ya tano ni ukarabati na ujenzi wa magati mapya. Bandari ya Dar es Saalam ina magati kumi na mbili tu, lakini bandari nyingine mtaona zina magati karibuni hamsini. Pia mwisho kulikuwa hakuna ufumbuzi katika mnyororo mzima wa usafirishaji wa mizigo kuanzia kwenye meli mpaka kwa mdau ambaye unampelekea huduma hiyo.

Mheshimiwa Spika, Bandari ya Dar es Salaam ina ushindani mkubwa kwenye bandari nne duniani hasa kwenye mizigo ya Zambia, Malawi, Rwanda, Uganda na DRC. Bandari ya kwanza ambayo inatupa pressure kubwa na ushindani mkubwa ni Bandari ya Mombasa. Bandari ya Mombasa inamilikiwa na Mamlaka ya Bandari ya Kenya. Bandari hii ina gati kumi na saba, Dar es Salaam tuna gati kumi na mbili. Magati kumi na tatu ni ya mizigo ya kawaida, magati sita ni kwa ajili ya kuhudumia makasha na kati hiyo bandari ya kuhudumia makasha, Container Terminal Two inaendeshwa na private sector, haiendeshwi na Kenya Port Authority, private sector. Inaendeshwa na Mediterranean Shipping Company hii ni kampuni ya Kiitaliano, hakuna suala la usalama, hakuna suala la nini, inaendesha hiyo kazi.

Mheshimiwa Spika, bandari ya pili ni gati maalum kwa ajili ya kushushia nafaka (Grain Terminal) ambayo inaendeshwa na private sector, Grain Bulk Handler Limited ya Kenya ndio inaendesha, ni private sector. Kwa hiyo, tusiogope private sector kwenye kuendesha bandari. Tusiwe waoga, ni aibu kuona mtu anasimama anasema anaogopa private sector, inaonekana mtu wa ajabu kwenye kuendesha bandari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bandari nyingine ambayo inatupa pressure kubwa ni bandari ya Durban. Bandari ya Durban inamilikiwa na Transnet National Port Authority ya South Africa. Bandari hii ina magati 50. Magati 31 ni ya kawaida, magati ya kuhudumia makasha ni kumi na magati kwa ajili ya mafuta, makaa ya mawe na chuma ni tisa. Magati 31 ya kawaida na magati kumi ya kuhudumia makasha inaendeshwa na Transnet Port Terminal siyo Transnet National Port Authority, hii ni kampuni tofauti. Magati tisa ya mafuta na makaa ya mawe na biashara au bidhaa za chuma na saruji yanaendeshwa na private sector, Durban Bulk Spring Company inaendeshwa na Spring Leaf na Total Bad Freight ni private sector.

Mheshimiwa Spika, kwa vile duniani kote unapokwenda ni private sector inaendesha bandari hasa maeneo ya kontena.

Mheshimiwa Spika, Bandari ya Beira, Msumbiji; hii ni bandari inayotupa ushindani mkubwa. Bandari hii inamilikiwa na Shirika la Bandari na Reli la Msumbiji na ina magati kumi na moja. Magati ya shehena za mchanganyiko na magati ya kushushia kontena. Gati hizi zote za shehena ya mchanganyiko na magati ya kushushia makontena au makasha inaendeshwa na kampuni ya Gold Elder Mozambique ambayo yenyewe ni private sector.

Mheshimiwa Spika, ukienda bandari inayotupa pressure tena ya Namibia Bandari ya Walvis Bay ya Namibia. Bandari hii inamilikiwa na Mamlaka ya Bandari Namibia na gati ya kushushia makontena au makasha inaendeshwa na kampuni ya Terminal Investment Limited ni private sector na hakuna issue ya security, watu wanaogopa; tunaogopa nini Watanzania? Ni aibu kuwa tunaogopa ogopa, ni aibu sana.

Mheshimiwa Spika, natoa mifano ya bandari mbili za mwisho; Bandari ya Tanger Med Port ya Morocco. Bandari hii inamilikiwa na Mamlaka ya Bandari ya Tanger Med ya Morocco, ina magati manne ambayo yanafanya kazi ya kushusha makontena ambayo yana uwezo wa kushusha kontena 9,900,000 kwa mwaka, wakati bandari ya Dar es Salaam inashusha makontena 760,000; hii inashusha 9,900,000 na ina terminal nne au ina magati manne makubwa. Gati ya kwanza inaendeshwa na private sector ambaye anaitwa MPM Terminals, gati ya pili inaendeshwa na private sector inaitwa Euro Gate ya Europe; gati ya tatu inaendeshwa na private sector na gati ya nne inaendeshwa na private sector. Zote zinaendeshwa na private sector.

Mheshimiwa Spika, naweza kutaja yaani bandari nyingi duniani zinaendeshwa na private sector na hatujawahi kusikia issue ya security na hizi kampuni zinafanya vizuri lazima Watanzania tubadilike.

Mheshimiwa Spika, tuna uzoefu sisi wa kuendesha TICTS katika endeshaji wa Bandari ya Dar es Salaam. Itakumbukwa kuwa kwa mara ya kwanza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliingia mkataba na TICTS mnamo mwaka 2000 wa kukodisha Kitengo cha Makasha cha Bandari ya Dar es Salaam, kuanzia gati namba nane mpaka namba kumi na moja. Mkataba ule kwanza ulikuwa na shida, lakini mwaka 2017 tulikaa sisi na timu ya wataalam, tulibadilisha mkataba ule na ndiyo iliyotusaidia tukaweza kumalizana nao mwezi Desemba mwaka huu.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na mapungufu mengi kwenye utendeshaji wa TICTS. TICTS haikuweza kuleta ufumbuzi katika mnyororo mzima wa usafirishaji wa mizigo na matokeo yake kwanza ilitokea alishindwa kufikia viwango vya kimataifa vya ushushaji wa mizigo na matokeo yake meli zilikaa nangani kati ya siku kumi mpaka siku kumi na nne. Kulikuwa na ucheleweshwaji mkubwa wa mizigo kutoa bandarini na tukalazimika tusiendelee tena na ule mkataba wa TICTS.

Mheshimiwa Spika, tunahitaji wawekezaji mahiri kwenye Bandari za Dar es Salaam. Tunahitaji au Serikali inahitaji waendeshaji na wawekezji wa bandari ambao wana ujuzi wa kimataifa ambao tunawaita Global Port Operators wenye uwezo na sifa zifuatazo; kwanza wawe na uwezo wa kufikia viwango vya kimataifa pamoja wawe na ufanisi utakaowezesha Bandari ya Dar es Salaam kuwa washindani na bandari nyingine; hiyo ni condition ya kwanza.

Pili, wawe na uwezo wa kutoa ufumbuzi katika mnyororo mzima wa usafirishaji (end to end total logistic chain solution) kutoka toka mzigo unaingizwa kwenye meli mpaka unafika kwa mteja.

Tatu, wawe na mtandao mpana wa kupata mizigo kwenye soko la usafirishaji mali duniani. Hatutaki mtu ambaye hata kutafuta mzigo hawezi, hapana tupate kampuni kubwa ya kimataifa amabyo inajulikana duniani; na nne, wawe na uwezo wa kimataifa katika kuendeleza na kuendesha shughuli za kibandari.

Mheshimiwa Spika, kama tutapata wawekezaji kama hao matokeo yake ni kama ifuatavyo; kwanza kupunguza muda wa meli kukaa nagani kutoka siku tano za sasa mpaka kufikia saa 24 au siku moja. Hii itaongeza idadi ya meli zinazokuja bandari ya Dar es Salaam.

Pili, kupunguza muda wa ushushaji wa makasha kutoka siku nne za sasa mpaka kufikia siku moja na nusu; tatu kupunguza muda wa uendeshaji mizigo (truck turn around) kutoka saa mbili za sasa hadi kufikia dakika thelathini. Gari inaingia within thirty minutes inatoka bandarini. Huyo ndiyo mtu tunayemtaka.

Mheshimiwa Spika, nne, kuongeza shehena ya mzigo kutoka tani 20,108,000 za sasa mpaka kufikia tani 47,570,000 mwaka 2033; tano, kuongeza mapato yanayotokana na kodi ya forodha kutoka shilingi trilioni 7.756 mwaka 2022/2023 mpaka kufikia trilioni 26.709 mwaka 2030, tunamtaka mtu kama huyo. Tukifikia hapa 70% au 80% ya bajeti itakuwa inatoka bandarini; na sita, kulinda ajira zilizopo na kuongeza mnyororo wa ajira mpya mpaka kufikia 28,990 tunataka mtu kama huyo.

Saba, kushusha kwa gharama ya usafirishaji kupitia bandari ya Dar es Salaam ambapo itachangia kupunguza gharama za bidhaa zinazoingia nchini; na nane, tunataka mtu ambaye kuchagiza ukuaji wa sekta nyingine za usafiri kama vile reli, mnajua tumetumia pesa nyingi kujenga reli, tunataka mtu atakayeleta mzigo wa kutosha ili kuipa reli yetu mzigo wa kutosha, huyo ndio muwekezaji tunayemtaka.

Mheshimiwa Spika, suala la uwekezaji halina mjadala, Serikali imeamua inakwenda mbele lazima Bandari ya Dar es Salaam tuweke wawekezaji ambao wataleta maslahi mapana ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo; Bandari ya Dar es Salaam ina limitations zake na limitations za Bandari ya Dar es Salaam inakuja kwa sababu kila siku kuna meli mpya za teknolojia mpya. Kwa mfano, meli ambayo inaweza kubeba makontena 18,000 yenyewe kwenye entrance channel inatakiwa mita 250, Bandari ya Dar es Salaam sasa hivi entrance channel pale inapovuka ferry ni mita 170, hatuwezi ku-extend tena itafika wakati.

Mheshimiwa Spika, sasa tukitaka meli kubwa zenye urefu wa mita 370 lazima twende Bandari ya Bagamoyo na ndugu zangu Serikali imeshaamua mwaka huu wa fedha kwenye bajeti tumezungumza ukienda kwenye ukurasa wa 117 kifungu cha 11 tumesema tunaenda kuanza Bandari ya Bagamoyo. Bandari ya Dar es Salaam itafanya kazi, lakini kwa zile meli kubwa ambazo zitashindwa kuingia kwenye Bandari ya Dar es Salaam itakwenda Bandari ya Bagamoyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri alilizungumzia hili la reli ya Mchuchuma, hili jambo limezungumzwa mara nyingi na Mheshimiwa Kingu amelizungumza leo hapa na amelizungumza kwa uchungu mkali na hisia kali na kwa kweli feasibility study imeshafanyika. Lakini Waheshimiwa Wabunge ninaomba sana Sheria yetu ya PPP sasa hivi ni ngumu sana kuleta mwekezaji, lakini tumepata fursa nimeshasema mara ya kwanza, mara ya pili nategemea itakuja, ninaomba sana tufanye maboresho makubwa ili tuweze kufungua nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutasema, tutazungumza lakini bila ya kufanya mabadiliko kwenye Sheria yetu ya PPP hatutoweza kuwafanyia watanzania haki. Waheshimiwa Wabunge tuna jukumu kubwa na sheria hiyo itakuja ninaomba tuifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala la umiliki wa ndege, tumekubaliana na Wabunge wote kwa kweli suala la umiliki wa ndege ni sahihi liende Air Tanzania na Serikali imeunda timu ya wataalam, inajumuisha wataalam hapa nchini na kutoka nje wenye uelewa wa masuala ya usafiri wa anga na uendeshaji wa mashirika ya ndege ili kupitia muundo wa sasa wa Air Tanzania ikiwa ni pamoja na suala la umiliki wa ndege. Timu hiyo tayari imekamilisha kazi yake na itawasilisha taarifa yake kwenye kikao cha Baraza la Mawaziri wakati wowote na uamuzi utatoka. Naomba niwahakikishie tu kwamba tutafanya maamuzi sahihi kwa maslahi ya Air Tanzania na kwa maslahi ya Watanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye sekta ya ujenzi; kupanda kwa gharama kwneye miradi ya maendeleo TANROADS; kuna mambo ya msingi ambayo yanasababisha kupandisha gharama za miradi. Jambo la kwanza kabisa ni mabadiliko ya usanifu (poor design), miradi mingi inapandisha hela ama miradi mingi inaongezeka hela kwa sababu ya poor design, hili tumelijua ndani ya TANROADS tumejipanga sasa kwamba tuhakikishe kuwa design tunazozifanya zinaenda na viwango vinavyotakiwa.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo linasababisha kupanda kwa gharama za ujenzi ni mabadiliko kwenye site. Unaweza ukaanza site yako ya ujenzi, ukafika pahala ukakutana na mwamba, hiyo lazima itabadilisha gharama za ujenzi.

Mheshimiwa Spika, ya tatu ni mpangilio mbovu wa kazi; kama unaenda kufanya kazi, lakini mpangilio wako siyo sahihi hiyo definitely itabadilisha gharama za ujenzi na hili tumelijua TANROADS tunajipanga vizuri.

Suala la nne ni ucheleweshwaji wa kutoa maamuzi; utoaji wa maamuzi ni muhimu kwenye kujenga, unaweza kufanya kazi mara TANROADS hajatoa, mara Meneja hajatoa, hiyo pia inasababisha ucheleweshwaji au uongezaji wa gharama ya kazi.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni hali ya hewa, kwa mfano pale Makete. Makete ukikosea muda wa kujenga karibuni miezi sita pale ni mvua. Usipokuwa makini hii italeta shida, sasa wakandarasi na wataalam wetu wa TANROADS hilo walijue na la mwisho linalosababisha ni mawasiliano mabovu kati ya mtaalamu yaani mshauri elekezi na mkandarasi na client yaani sisi TANROADS, hili tunalifahamu na yote haya tunayafahamu. Nawaomba Waheshimiwa Wabunge mtuamini, tunaenda kuyafanyia kazi ili kuhakikisha kwamba tunaenda ku–control hizi variation za miradi ya ujenzi wa barabara.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ni taa za barabarani; tunafahamu kwamba taa za barabarani ni muhimu sana kwenye usalama wa watumiaji wa barabara, pia zinatoa fursa wananchi kufanya kazi zao usiku na mchana. Serikali tumeamua kwamba barabara zote zitakazojengwa na TANROADS sasa tutafunga taa za barabarani na zile ambazo zilishajengwa tutakwenda kufunga taa za barabarani. Hatuwezi kuendelea tunatumia hela nyingi kujenga barabara lakini tunaacha giza, hilo halikubaliki. Tumeamua na tumeshatoa maelekezo kwamba barabara zote sasa zitafungwa taa ili wananchi wetu waweze kufanya kazi usiku na mchana.

Mheshimiwa Spika, kuna hoja ya EPC lakini sitaki niizungumze kwa sababu EPC ndio my baby, ndio kwa mara ya kwanza Serikalini Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi tumeanzisha EPC+Finance. Mwaka jana wote mlikuwa hamtuamini hapa, wengine mlisema tunasema tu lakini haitekelezeki, lakini leo mambo mmeyaona wenyewe. Baada ya miaka minne tutaandika historia ya nchi yetu. Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumza sana, sitaki kulizungumza jambo hili naomba hili jambo ni kubwa sasa sisi malengo yetu ni kuangalia Dar es Salaam Express Way kutoka Dar es Salaam, kutoka Kibaha - Chalinze na Morogoro. Hilo ndio lengo letu kubwa. EPC tumemaliza sasa tunaangalia Dar es Salaam Express Way.

Mheshimiwa Spika, kuna barabara za Waheshimiwa Wabunge hapa kwa mfano Mheshimiwa Ramadhani jana alisema kwa masikitiko makubwa mpaka alikuwa kidogo anataka kulia anasema Kinyaturu anasema kila lugha, kwa vile tumeamua kwamba tunaenda kujenga barabara hiyo kwanza tutaanza kwa kilometa 10. (Makofi)

Mheshimiwa Mbunge wa Nansio vilevile kuna changamoto kubwa kule kwake, hasa kwenye kupata material ya ujenzi. Kila siku kujengea changarawe inakuwa ni shida. Tumeamua kwenda kuijenga ile barabara kutoka Rugezi mpaka Nansio yenye urefu wa kilometa 12 kwa kiwango cha lami na tutaitangaza mapema mwakani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna Mheshimiwa Mbunge wa Sumve ambaye na yeye ana changamoto pale wilayani kwake, kwamba hakuna barabara yoyote ya lami. Tumeamua sasa nayo tunaenda kuijenga kwa lami. Mheshimiwa Gulamali vilevile na yeye kuna barabara yake tumesema kwamba tunaenda kujenga angalao kilometa 10, Puge – Ziba mpaka Chomo, lakini tunaanza kwa kilometa 10 tunahakikisha kwamba tunaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamesema barabara zao nyingi, zote tumezichukua na tunaenda kuzifanyia kazi kuhakikisha kwamba, tunazijenga kwa kiwango cha lami kwa asilimia 100. Mwisho kabisa napenda kuchukua fursa hii tena kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutupa fedha nyingi kwenye Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Tunaomba kumwambia tu kwamba, hatutamuangusha, kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naafiki.