Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii na mimi nichangie mambo machache.

Mheshimiwa Spika, kwanza naunga mkono hoja iliyowekwa mezani kwetu na Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi pamoja na timu yake, ninampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya katika sekta hii ya Ujenzi. Sekta ya Ujenzi ni moja ya sekta ambayo ina miradi mikubwa, miradi yote inaendelea kutekelezwa na tumeshapiga hatua kubwa sana katika utekelezaji wake.

Mheshimiwa Spika, katika mchango wangu naomba nichangie mambo matatu. Jambo la kwanza ambalo ningependa kulichangia ujenzi kwenye sekta hii ya ujenzi, sekta zote ambazo zimetajwa na Mheshimiwa Waziri una bajeti takribani za aina tatu, nne hivi. Bajeti mojawapo ni bajeti hii ambayo tunapitisha, bajeti nyingine ni zile ambazo ziko kwenye mifuko mahsusi, bajeti nyingine ni zile barabara ambazo zinapata udhamini kutoka kwa wabia wetu wa maendeleo, bajeti nyingine ni hii ambayo tumeiongelea ya EPC+F.

Mheshimiwa Spika, niliona Waheshimiwa Wabunge baadhi katika kuchangia akiwepo Mheshimiwa Halima jana wakati anachangia alianza kupiga hesabu kana kwamba barabara zote tunazoenda kuzijenga zinajengwa kwa bajeti hii ambayo inapitishwa kwa maana ya kipengele kimoja kimoja kwa maana ya cash budget ambayo inapitishwa makusanyo ya kila mwezi.

Mheshimiwa Spika, nikaona nipate fursa ya kufafanua huu utaratibu tunaosema wa EPC + F maana yake nini na kwa nini tumebadili utaratibu tukasaini barabara yote kwa urefu wake.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara hizo hazitajengwa ndani ya mwezi mmoja na kwa kufatana na urefu zingine hata hazitajengwa ndani yam waka mmoja. Utaratibu wa EPC+F kwa jinsi ambavyo unatumika ni kwamba Wizara ya Ujenzi ikishafanya utaratibu wa kumpata mkandarasi na mkandarasi akaja na finance award Wizara ya Fedha inafanya terms zile, ina- negotiate zile terms inafanya majadiliano ya vile vigezo vya kupata mkopo wa kifedha ambavyo vinazingatia mambo ya riba pamoja na masuala mengine ya gharama za ukopaji, baada ya hapo kinachofata ni mkandarasi anaanza kulipwa kufatana na utekelezaji wa mradi na fedha zinatoka kwa yule ambaye ni financier wa mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo tulibadili utaratibu huu ili tuweze kupunguza utaratibu huu wa certificate kujazana. Maana yake natolea mfano, kama barabara ya Liwale – Nachingwe - Masasi labda financier wake ni Benki ya CRBD ama City Bank, ama itaje benki yoyote natolea mfano. Maana yake tukishakubaliana terms hiyo fedha itakuwa inatoka kadri anavyotekeleza mradi. Akishatekeleza hatua fulani Wizara inakagua inakubaliana kwamba hii imeshatekelezwa Wizara inatuarifu kwamba huyu hapa ameshatekeleza sisi tunawapa ruhusa benki wanalipa hiyo fedha ambayo imepitishwa kwa ajili ya mradi huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo kwa mazingira hayo hatutarajii hiyo ya kusema kwamba zitatumika bilioni mbili, zitatumika kilometa 200, tutalipa kufuatana na kasi ya utekelezaji tu wa Mkandarasi anavyojenga hiyo ndiyo dhana ya EPC+F.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ziliongelewa barabara ambazo Waheshimiwa Wabunge walikuwa wanafuatilia, barabara zipo ambazo tunaendelea na majadiliano tuko hatua za mwisho. Timu yangu iko Egypt kwenye annual meeting ya African Development Bank na barabara hizo tuna-conclude tunaamini kwamba zitafanyiwa marekebisho ziingie kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ili ziweze kutekelezwa. Tuna barabara ya Magu – Isandula - Bukwimba kwenda Hungumalwa, tuna barabara ya Kahama kwenda Geita ambayo tunaweka nyongeza kwenye ile fedha ambayo ilishatolewa na mgodi.

Mheshimiwa Spika, tuna barabara ya Iguguno -Nduguti kwenda Sibiti kwa jirani yangu Mheshimiwa Francis Isack naona ameamua kuwa jirani mpaka hapa. Tunayo barabara ya Singida - Ilongero - Haydom ambayo Mheshimiwa Mbunge aliongea kwa nguvu kubwa sana na tuna barabara ya Chunya - Makongorosi kwenda Itigi. Hizi ni barabara ambazo zilishafanyiwa mazungumzo kwa ufadhili wa Benki ya Maendeleo ya Afrika na sasa hivi timu iko kule Egypt kukamilisha namna ya utekelezaji wa miradi mingi ikiwemo na hiyo ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho yamekuwa yakitokea pia maswali kuhusu certificate zinazoiva. Kwa utaratibu pale ambapo kasi ya utekelezaji wa mradi inakuwa kubwa sana kama hivi ilivyo sasa hivi, kasi ya utekelezaji wa miradi mingi ni kubwa, inatokea certificate zinakuja kwenye tarehe ambapo kuna commitment zile ambazo ni first charge, kwa hiyo ni kweli ikiangukia kwenye commitment ambayo ni first charge kunakuwepo na utaratibu wa kupitisha kwanza malipo yale yakiwemo ya mishahara ya watumishi wa umma, malipo ya Deni la Taifa, lakini mara zote tunaongeaga na Wizara kuangalia zile deadline ambazo zinajitokeza.

Mheshimiwa Spika, kuna mazingira ambapo mradi unafadhiliwa kwa mkopo ambao unaenda moja kwa moja kwenye utekelezaji wa mradi, mradi ule kama ni wa mkopo tutakuwa tunatekeleza mradi lakini mradi ule lazima utakuwa na riba kwa sababu mradi wenyewe ulikuwa unatekelezwa una mkopo kwa hiyo tunapotekeleza mradi panakuwepo pia na riba kwenye mradi huo.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla wake niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge barabara hizi zitajengwa na zile ambazo zilikuwa zinaendelea kujengwa zitaendelea kujengwa na hata hivi sasa Mheshimiwa Rais pamoja na Wasaidizi wake anaendelea kututuma baadhi ya maeneo ili kuweza kuhakikisha tunatafuta fedha nyingi zaidi ili kuweza kutekeleza miradi hiyo ya maendeleo. Tuna majadiliano tumeshafanya hatua ziko za kimikataba na wenzetu wa European Investment Bank, ambayo inahusisha viwanja vya ndege pamoja na baadhi ya barabara na yenyewe ikikamilika Waheshimiwa Wabunge mtaarifiwa miradi ambayo inapatikana katika Majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunatekeleza mirdi hii ya barabara kwa sababu ni moja ya nguzo muhimu ambazo zinafungua uchumi wetu na wananchi waendelee kuiamini Serikali yao, waendelee kumwamini Mheshimiwa Rais, waendelee kuwaamini Waheshimiwa Wabunge ambao wao wenyewe wameshuhudia jinsi wanavyoisimamia Serikali na jinsi ambavyo wanasimama kidete kwa ajili ya kuomba barabara hizo ili ziweze kupitika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona kengele ya pili imeni-alert basi naunga mkono hoja na nawapogeza Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake. (Makofi)