Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa sikupata nafasi ya kuchangia kwa kuongea Bungeni, naomba nitoe mchango wangu kwa maandishi kwa kifupi sana.

Kwanza naipongeza sana Serikali kwa kazi nzuri iliyofanyika na inayoendelea kufanyika. Nilipata neema ya kutembelea miradi inayotekelezwa wakati wa ziara ya Kamati; SGR, Mamlaka ya Bandari Dar es Salaam, Mwendo Kasi Dar es Salaam, Bandari Kavu Kwala, Bandari ya Kalema - Katavi, Daraja la Busisi, ujenzi na ukarabati wa meli vivuko na chelezo na kadhalika. Kwa kweli Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi inafanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Spika, pamoja na shukurani na pongezi zangu, nasikitika kusema kwamba Serikali haitekelezi ahadi za viongozi wakuu ipasavyo. Kuna ahadi nyingi za viongozi wakuu ambazo zilitolewa mbele ya wananchi wengi ambazo bado hazijatekelezwa licha ya ukweli kwamba anachokisema mkuu wa nchi ni decree na inapaswa itekelezwe.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa kwenye Jimbo la Arumeru Mashariki ni barabara kwa kuwa sehemu kubwa ya jimbo ni Mlima Meru ambako wako wananchi wanaoishi kwenye miteremko ya huu mlima. Terrain si rafiki kwa barabara za udongo na changarawe.

Mheshimiwa Spika, nasikitika kusema kwamba jimbo hili lilikuwa limesahaulika kwa muda mrefu halijawahi kupewa hata mita moja ya barabara ya lami, lakini mwaka 2020 tulipata bahati ya kupewa ahadi ya ujenzi kwa kiwango cha lami barabara ya Kingori inayoanzia Malula Kibaoni hadi Ngarenanyuki iungane na barabara ya Usa River hadi Oldonyo Sambu.

Mheshimiwa Spika, ahadi hii ikitekelezwa tutakuwa na ring road ya kimkakati ambayo itaweka katikati vivutio vya utalii vya Hifadhi ya Taifa Arusha na msitu wa Mlima Meru, lakini pia itafupisha safari ya kutoka Moshi hadi Namanga kwa kilometa 33 na kuinua uchumi na ubora wa maisha ya wananchi wengi wa kata nane ambako imepita.

Mheshimiwa Spika, nashauri Serikali ifanye kila linalowezekana ahadi itekelezwe hasa ukizingatia kwamba tunaelekea kwenye Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 ambao tunauanza mwakani kwa Serikali za Mitaa. Wabunge tunapata mzigo yanapokuja maswali ya ahadi za Rais kutoka kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, ahadi ya ujenzi wa barabara ya Sangis kwenda Akheri hadi Ndoombo ni ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete aliyoitoa mwaka 2012; hii imeanza kutekelezwa lakini inafanyika kwa kusuasua sana. Nashauri Serikali iongeze nguvu hapa ikiwezekana imalizike kabla ya mwaka 2025.

Mheshimiwa Spika, ahadi ya ujenzi wa barabara urefu wa kilometa tano Mjini Usa River aliyotoa Rais wa Awamu ya Tano Hayati Dkt. John Pombe Magufuli mwaka 2025 bado nayo inangojea utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mbuguni kuanzia Tengeru inaunganisha Mikoa ya Arusha na Manyara, nasikitika haijaongelewa kwenye bajeti hii.

Mheshimiwa Spika, tunashukuru upembuzi yakinifu umeanza lakini nashauri Waziri aiongelee wakati wa kuhitimisha kwa sababu ilisahaulika kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.